To Chat with me click here

Monday, September 10, 2012

CHADEMA WAMSHUKIA JK KWA KUTOJUA ASEME NINI JUU YA MAUAJI YA MWANDISHI IRINGA


MKANDA WA MAUAJI WAWALIZA WAJUMBE

CHAMA cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA), kimemshukia Rais Jakaya Kikwete kikieleza kushangazwa na ukimya wake kuhusu mauaji ya aliyekuwa mwandishi wa Kituo cha televisheni cha Channel Ten, Daudi Mwangosi, yaliyofanywa na Jeshi la Polisi.

Akifungua kikao cha Kamati Kuu cha dharura jijini Dar es Salaam jana, Mwenyekiti wa CHADEMA, Freeman Mbowe, alisema chama hicho kimeshitushwa na kusikitishwa na hali hiyo hasa ikizingatiwa kuwa rais ni Amiri Jeshi Mkuu na kwamba moja ya chombo chake cha dola kimehusika katika tukio la kinyama la mauaji ya mwandishi wa habari.

Alisema inafahamika kuwa Rais Kikwete ni mwepesi kushiriki, kuhudhuria na kutoa salamu za rambirambi katika misiba mbalimbali, lakini katika tukio hili la mauaji ya kusikitisha na kutisha, amekuwa kimya kana kwamba hakuna jambo lolote lililotokea ndani ya nchi anayoiongoza.

“Tunasikitika kama chama katika msiba huu wa mwanahabari ambao umetokea katika mazingira ya kutatanisha na yeye akiwa amri jeshi mkuu, mkuu wa serikali, mkuu wa nchi ambaye majeshi yote yanawajibika kwake, ameweza kuona tukio kubwa kama hili lililogusa hisia za Watanzania mbalimbali, wanadiplomasia, wanaharakati ndani na nje ya nchi na vyombo vya habari vya kimataifa CNN, Al Jazira, lakini Rais Kikwete hajathubutu kutoa kauli.

“Rais yupo Kampala anasuluhusisha mgogoro wa Kongo wakati tuna migogoro ndani ya jamii yetu,” alisema.

Alisema katika siku za hivi karibuni kumeibuka migogoro mbalimbali hapa nchini ikiwamo ya madaktari na walimu na kwamba sasa imeingia kati ya Jeshi la Polisi na wananchi.

Mbowe alisema katika hali hii ya huzuni na hofu kubwa miongoni mwa waandishi wa habari na Watanzania wengi kutokana na kukithiri kwa mauaji ya raia yanayofanywa na polisi, CHADEMA imeshangazwa na kushitushwa na matamshi ya baadhi ya watendaji serikalini ambayo yanajaribu kuficha ukweli wa mauaji na uvunjaji makusudi wa haki za binadamu.

Aliongeza kuwa wakati watu wakiwa katika taharuki kutokana na mauaji hayo, ni jambo la kushangaza kuona baadhi ya watendaji wa serikali wakiibuka na kutoa kauli zilizojaa uchochezi na kuvunja amani.

Mbowe alitaja moja kwa moja matamshi ya Msajili wa Vyama vya Siasa nchini, John Tendwa, aliyotoa hivi karibuni akitishia kukifuta CHADEMA kwa kile alichosema ni kusababisha mauaji, kuwa ni za hatari na zilizolenga kuonesha kuwa mauaji hayo yanatokana na mgogoro kati ya polisi na chama hicho.

Picha zawaliza wajumbe
Baadhi ya wajumbe wa kikao hicho walishindwa kujizuia na kuangua kilio baada ya kuonyeshwa picha za mnato na video za mauaji ya Mwangosi.

Picha iliyowaliza wajumbe ni ile inayoonekana mabaki ya mwili wa marehemu Mwangosi baada ya kupigwa bomu la machozi tumboni ambalo lilisababisha utumbo kutoka nje.

Dk. Slaa afafanua SMS
Katibu Mkuu wa CHADEMA, Dk. Willibrod Slaa, amesema kuwa inawezekana IGP, Said Mwema na Waziri wa Mambo ya Ndani, Nchimbi ni mbumbumbu wa sheria kutokana na kudai ujumbe wake mfupi wa maandishi (SMS) ni wa kichochezi.

Alisema kama si mambumbumbu wa sheria, basi hawajui maana ya neno uchochezi na kuhoji kama ujumbe huo ni wa uchochezi kwa nini mpaka sasa hawajamkamata.

“Nilimtumia ujumbe ule IGP, lakini aliupeleka kwa Waziri Nchimbi maana yake anaomba ushauri ambao pia waziri ameshindwa kumpa mpaka mauaji yametokea.

“Nchimbi ameshindwa kutimiza wajibu wake, hivyo anatakiwa kujiuzulu kwa kushindwa kuufanyia kazi ujumbe wa thadhari,” alisema.

CUF: Kuuawa mwandishi ni aibu kwa taifa
Chama cha Wananchi (CUF) kimesema kuwa tukio la kuuawa kwa mwandishi Mwangosi ni aibu kwa taifa.

Akizungumza jana katika mkutano wa hadhara uliofanyika katika Viwanja vya Jangwani jijini Dar es Salaam, Mwenyekiti wa chama hicho, Professa Ibrahimu Lipumba, alisema kuwa mauaji hayo yamelichafua taifa zaidi na ni ishara ya serikali kuwafanya wananchi waogope kueleza mambo yanayowaumiza.

“Kuuawa kwa mwandishi wa habari kwa nchi isiyo na vita ni aibu kwa taifa na kuwafanya wananchi wasiweze kupata habari zinazoendelea katika taifa lao,” alisema.

No comments:

Post a Comment