To Chat with me click here

Monday, September 10, 2012

MWANAHARAKATI ATAKA RAIS ASHITAKIWE


MWANAHARAKATI wa Kimataifa wa Haki za Binadamu nchini, Joram Kinanda, amependekeza katiba mpya ieleze ikiwa rais wa nchi atajihusisha na vitendo vya rushwa, kupora au kuhujumu uchumi, miradi ya maendeleo au kuhatarisha usalama wa taifa, achukuliwe hatua gani.

Kinanda ambaye ni Mjumbe wa Shirika la Kimataifa la Kutetea Haki za Binadamu (Amnesty International), alitoa mapendekezo hayo wakati akizungumza na Tanzania Daima, na akasema hatua hiyo itaiwezesha nchi kusimama katika misingi imara na inayokubalika na jamii.

“Tunataka katiba ieleze kwamba rais wa nchi atachukuliwa hatua gani ikiwa kama atajihusisha au atakiuka Katiba ya Tanzania, kuiba, kuchukua, kuchota au kusogeza vitu vyovyote ili mradi ni wizi tu, kujipatia mapato isivyo halali na kudhalilisha kiti anachokalia (urais),” alisema.

Kinanda ambaye mwaka 2010 alitaka kugombea urais kama mgombea binafsi alipendekeza pia katiba itamke kwamba uteuzi wa majaji wa Mahakama Kuu na Mahakama ya Rufani, Jaji Kiongozi, na Jaji Mkuu uthibitishwe na Bunge baada ya rais kuwateua.

Alipendekeza pia, tume huru ya uchaguzi na wajumbe wake wathibitishwe na Bunge, na wajumbe wa Tume ya Uchaguzi wasitoke chama kimoja hata kama wamevaa kivuli cha watumishi wa serikali.

“Katiba tunayoitaka Watanzania ni ile itakayorudisha haki za watu zilizopotezwa au kuporwa, ilete matumaini kwa waliovunjwa mioyo na kupoteza matumaini, iwe dira ya kutufikisha tunapotaka kwenda kwenye maisha bora na sio bora maisha,” alisema Kinanda.

Alisisitiza kuwa, katiba hiyo iwe mali ya Watanzania wote na sio viongozi wa CCM peke yao kama wanavyojinasibu kwa sababu waliitengeneza wao.

Alisema kuna malalamiko mengi kutoka kwa raia juu ya kero za muungano na tatizo kubwa la kupatikana haki kwa raia na ndio chanzo cha kushika kasi kwa dhuluma.

No comments:

Post a Comment