UAMUZI
wa Kamati Kuu ya Chama cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA) kukataa
kuwasilisha ushahidi wa mauji ya mlipuko wa bomu uliotokea jijini Arusha,
umeliweka njia panda Jeshi la Polisi na hivyo kushindwa kuchukua hatua.
Licha
ya jeshi hilo kumhoji Mwenyekiti wa CHADEMA, Freeman Mbowe, na kumtaka
awasilishe ushahidi huo, kiongozi huyo amekataa agizo hilo akisema kuwa
wamekubaliana kuutoa ushahidi huo kwa tume huru ya majaji endapo Rais Jakaya
Kikwete ataiunda kama walivyomuomba.
Chanzo
chetu ndani ya jeshi hilo, kimedokeza kuwa msimamo huo wa CHADEMA umeliweka
njia panda na hivyo kushindwa kuchukua hatua za kuwabaini watuhumiwa wa tukio
hilo na kuwafungulia mashtaka kutokana na mkanganyiko wa taarifa zinazotolewa.
Jeshi
hilo linadaiwa kuwa awali lilitaka kujiegemeza kwenye kauli za kisiasa za
baadhi ya viongozi wa Chama cha Mapinduzi (CCM) na serikali ili kuonyesha kuwa
CHADEMA ilisababisha mlipuko huo yenyewe kwa ajili ya kuwahadaa wafuasi na
kujitafutia umaarufu.
Hata
hivyo, mbinu hiyo ya kutaka kuwasakama baadhi ya viongozi na wafuasi wa CHADEMA
inadaiwa kufifishwa na tamko la Mbowe pamoja na mbunge wa Arusha Mjini,
Godbless Lema, kwamba chama kina ushahidi unaoonyesha kuwa tukio hilo
lilifanywa na polisi.
“Hapa
kuna mkanganyiko hasa baada ya Mbowe kudai wanao ushahidi wa video ya tukio
hilo. Wakubwa wetu wamegawanyika na kujikuta wakitoa kauli za kukinzana maana
wanahofia wakiwafungulia kesi watu wengine mashtaka halafu CHADEMA ikaonyesha
ushahidi tofauti itakuwa ni aibu,” kilisema chanzo chetu.
Kwa
mujibu wa chanzo hicho, jeshi hilo mkoani Arusha lilikuwa limewakamata watu
wawili raia wa kigeni likiwatuhumu kuhusika na mlipuko huo lakini baada ya
Mbowe kugoma kupeleka ushahidi huo, watuhumiwa hao hawakuweza kufunguliwa
mashtaka.
Pia
katika hali ya kushangaza Mkuu wa Mkoa wa Arusha, Magesa Mulongo, alikaririwa
na baadhi ya vyombo vya habari kuwa makachero wa Taasisi ya Uchunguzi ya
Marekani (FBI) wamefika mkoani Arusha kuchunguza jambo hilo.
Hata
hivyo taarifa kutoka ubalozi wa Marekani zilikana FBI kuingia nchini kuchunguza
jambo hilo hivyo kusababisha mkanganyiko wa tukio hilo lililovuta hisia kubwa
ndani na nje ya nchi.
CHADEMA
mara kwa mara imekuwa ikilituhumu jeshi la polisi na makada wa CCM kuendesha
harakati za kukidhoofisha kwa kutumia matukio mbalimbali yanayofanywa na chama
hicho cha upinzani.
Mmoja
wa viongozi wa CHADEMA aliviambia vyanzo vyetu vya habari, kuwa polisi walikuwa
wamepanga kuwatumia FBI kuuhabarisha umma kuwa CHADEMA ilihusika na ulipuaji
huo bomu lakini kutokana na mazingira yaliyopo wameshindwa kutekeleza uovu huo.
“Unajua
hila za polisi na CCM kila siku zinabadilika lakini kwa bahati mbaya hawajui
kuwa wananchi wanajua kinachofanyika, kuna askari hawaridhiki na uovu
unaofanywa na wenzao,” alisema kiongozi huyo.

