To Chat with me click here

Monday, September 24, 2012

CCM YAWASUTA SITTA, LEMBELI


NAPE ASEMA KAULI ZAO HAZIWEZI KUSIKILIZWA KWANI HAWAJIAMINI

CHAMA cha Mapinduzi (CCM) kimesema hakitishwi na baadhi ya viongozi wake ambao wamekuwa wakitoa kauli zao barabarani kwa ajili ya kulalamika na kukikosoa chama badala ya kupeleka malalamiko yao katika vikao husika.

Kitendo cha viongozi hao kuendelea kutoa taarifa zao za malalamiko barabarani ni dalili za kutojiamini na kuonyesha udhaifu wa kuhimili mikiki ya uchaguzi ndani ya chama hicho na inawezekana wana agenda zao za siri.

Kauli hiyo ilitolewa jana na Katibu wa Halmashauri Kuu (NEC) Taifa ya chama hicho, Itikadi na Uenezi, Nape Nnauye, alipokuwa akizungumza na waandishi wa habari juu ya vikao vya chama ambavyo vinaendelea mjini hapa.

Licha ya Nape kutowataja vigogo hao kwa majina, lakini ni wazi kuwa walengwa ni pamoja na Waziri wa Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Samuel Sitta, ambaye kwa siku za karibuni amenukuliwa akilalamikia vitendo vya ufisadi kwenye mchakato wa uchaguzi ndani ya CCM na hivyo kuibua mjadala mzito kwa baadhi ya makada akiwemo Mwenyekiti wa Mkoa wa Shinyanga, Hamis Mgeja, wakimtaka awataje kwa majina anaowatuhumu.

Wengine waliosikika hivi karibuni wakilalamikia mchakato huo wa uchaguzi unaoendelea ni Mbunge wa Kahama, James Lembeli na Nimrod Mkono wa Musoma Vijijini ambao inasemekena majina yao yamekatwa kwenye orodha ya wagombea, huku wakisema hapatatosha iwapo wataenguliwa kweli kimizengwe.

Nape alisema kuwa CCM inashangazwa na baadhi ya wanachama wake ambao wanaonyesha woga wa kushindwa kuhimili mikiki ndani ya chama, hususan katika kipindi hiki cha uchaguzi na badala yake wamekuwa wakitishia kujitoa kama majina yao hayatarudishwa kwa ajili ya kuchaguliwa katika nafasi zao walizoomba.

Alisema kuwa chama hakiwezi kuwasikiliza viongozi ambao wamekuwa na tabia ya kutoa matamshi yao barabarani na kwamba kama wanataka kutoa kauli hizo, watumie fursa ya kuwasilisha hoja zao katika vikao.

“Chama hakiwezi kusikiliza kauli za barabarani ambazo zinatolewa na viongozi hao, kama wana hoja wazilete katika vikao kwa maana nao ni viongozi, wasipofanya hivyo basi huenda wana agenda zao za siri, ambazo wanazijua wao,” alisema.

Kuhusu baadhi ya wagombea ambao walisikika wakidai kuwa majina yao yasiporudishwa patachimbika, alisema kuwa inaonyesha ni jinsi gani hawajiamini kwani kiongozi ni lazima awe mvumilivu na mwenye kuhimili mikiki ya siasa za sasa ambazo zina ushindani mkubwa.

“Kama kiongozi anaanza kusikia tetesi kuwa jina lake halitarudishwa halafu anaanza kusimama barabarani na kudai kuwa hapatatosha, ni wazi kuwa ni mwoga wa kuhimili ushindani, lakini nataka kusema kuwa haki itatendeka na busara zitatumika.

“Hakuna mtu ambaye jina lake litakatwa kwa ajili ya mizengwe, bali vigezo vitazingatiwa ili kila mmoja apate haki yake, na lazima wagombea watambue kuwa kwa vyovyote vile lazima apatikane kiongozi ambaye ataweza kuongoza jumuiya husika,” alisisitiza Nape.

Aliongeza kuwa kutokana na kuwepo kwa wingi wa wagombea katika nafasi mbalimbali, kuna uwezekano wa kutokea msuguano mkubwa kwa wanachama kutokana na kila mmoja kutamani kushika nafasi aliyoiomba.

“Kimsingi wanachama waliojitokeza kuwania nafasi mbalimbali ni wengi zaidi ya mahitaji, hii ni ishara kuwa chama bado kinapendwa… kunawezekana kukatokea msuguano wa ndani kutokana na wingi wa wagombea, lakini chama kina utaratibu wa kumaliza mambo kama hayo,” alisema.

Kuhusu vikao kwenda kinyume na ratiba, Nape alisema kuwa kutokana na wingi wa wagombea wa nafasi mbalimbali, imelazimika sekretalieti kukaa siku tatu badala ya moja na kamati ya maadili ilitakiwa ikae siku moja, lakini imekaa mbili tofauti na matarajio.

Nape alisema kutokana na wingi wa wagombea, imewalazimu vikao kuchukua muda mwingi kujadili kwa makini ili kuhakikisha haki inatendeka na kuongeza kuwa, kwa nafasi ya wenyeviti wa mikoa zinazotakiwa ni nafasi 31 ila walioomba ni 187, katibu siasa na uenezi mkoa zinatakiwa nafsi 31 walioomba pia ni 187.

Alisema kuwa makatibu wa uchumi/fedha wa mkoa nafasi zinazohitajika ni 31 ila walioomba ni 170, wenyeviti wa wilaya nafasi ni 31 walioomba 148, wenyeviti wa wilaya wanahitajika 161 walioomba ni 965, wajumbe wa NEC taifa wanahitajika 221, lakini walioomba ni 1,380 na wajumbe wa NEC taifa wanahitajika 20 bali walioomba ni 89.

Nape alisema kuwa nafasi nyingine ni wenyeviti wa Jumuiya Taifa ya UVCCM ambayo inahitajika nafasi moja ila imeombwa na wagombea 47, UWT nafasi moja nayo inagombewa na watu 9, Jumuiya ya Wazazi nafasi moja imeombwa na watu 22 na makamu mwenyekiti UVCCM inahitajika nafasi moja, lakini walioomba ni 27, UWT nafasi ya makamu imeombwa na watu watatu huku ile ya wazazi ikiombwa na watu 10.

Hata hivyo, Nape alisema kuwa hatua ya mwisho ya kupitisha majina ya wagombea hao ni NEC na kwamba vikao vingine vinapitisha na kutoa alama za sifa ya wagombea.

Wazee wamvaa Sitta
Wazee wa CCM mkoani Shinyanga, wametishia kufanya maandamano ya amani kuhusiana na kauli tata zinazoendelea kutolewa na Waziri wa Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Samuel Sitta.

Katika tamko lao, wazee hao walisema wakati umefika sasa Sitta awaeleze Watanzania juu ya kauli zake hizo, ikiwemo ile ya kuwepo kwa mafisadi ndani ya chama na aliyoitoa hivi karibuni akiwa Karagwe, ya maisha bora kwa kila Mtanzania hayatawezekana.

Kwa niaba yao, Shomvi Ibrahimu Saidi, alisema kuwa waziri huyo ambaye pia ni mjumbe wa NEC na mbunge wa Urambo Mashariki, amekuwa akikaririwa akitoa tuhuma nzito ndani ya serikali na chama, hivyo ni vema akaweka wazi majina ya watuhumiwa wa ufisadi.

Pia walikumbushia jinsi kiongozi huyo alivyowahi kuitolea maneno makali Kamati Kuu ya CCM katika kipindi cha ‘Dakika 45’ kinachurushwa na Televisheni ya ITV, akisema kwamba ilihongwa na mafisadi ikabadili utaratibu wa kuchagua Spika wa Bunge.

Wazee hao wamemuomba Waziri Sitta kama hana ushahidi wa kutosha wa kuupeleka kwenye vikao vya chama na vyombo vya dola kama TAKUKURU, polisi na mahakama, ni afadhali akae kimya kuliko kuendelea kuwachanganya watu.


No comments:

Post a Comment