To Chat with me click here

Saturday, September 15, 2012

MAUAJI, VURUGU ZALITIKISA TAIFA


CHADEMA KUWASHITAKI RPC, MORO, IRINGA

MATUKIO ya kuuawa kwa raia, vitisho na vurugu zenye mwelekeo wa kumwaga damu, vimeliweka taifa katika mtikisiko mkubwa huku shinikizo la kuwataka Waziri wa Mambo ya Ndani, Emmanuel Nchimbi na Mkuu wa Jeshi la Polisi nchini, IGP Saidi Mwema wajiuluzu nyadhifa zao likizidi kuongezeka.

Katika mahoajiano maalum, viongozi mbalimbali wa dini na siasa wamesema kuwa, hali ya nchi imefikia mahali pabaya na watanzania sasa wanaishi kwa hofu kwa kuwa hawana uhakika na usalama wa maisha yao.

Askofu wa Kanisa la Kiinjili la Kilutheri Tanzania, Dayosisi ya Karagwe, Benson Bagonza alisema viongozi wa serikali na jeshi la polisi waliopewa dhama ya kulinda uhuru na maisha ya watu, wameoneshwa kushindwa kiasi cha kuifanya nchi kuwa katika hali ya mashaka makubwa.

Askofu Bagonza, alisema kuwa mauaji ya raia yanayaodaiwa kufanywa na jeshi la polisi katika mikoa kadhaa hapa nchini kwa visingizo mbalimbali, ni ishara ya wazi ya kukosekana kwa utawala wa sheria, pia dalili ya kutowajibika kwa viongozi.

Aliongeza kuwa, kuna ushahidi wa polisi kuua watu ovyo, lakini tume zinapoundwa hakuna jambo lolote la maana linalofanyika kutokana zaili ya kulindana huku raia wema wakipoteza uhai.

“Kwa mfano polisi analalamikiwa kuua…serikali inaunda hicho kilichoitwa kamati, ikija na majibu ikasema polisi aliyefanya tendo hilo alitumwa na mkubwa wake je, huyo mkubwa atakuwa tayari kuwajibika au ndiyo tunataka tu uundwaji wa tume tu,” alisema.

Akizungumzia siasa, kiongozi huyo alisema hafurahishwi na mwenendo wa kisiasa unaoendelea nchini kwa kuwa kuna kikundi cha watu ambacho kina haki ya kufanya shughuli za siasa yakiwemo maandamano na mikutano muda wowote na kisipatwe na madhara.

Kiongozi huyo alisema kuna ubaguzi wa waziwazi katika uendeshji wa shughuli za siasa, na kwamba wizara na jeshi la polisi limetumika kunyanyasa makundi mengine hasa chama kinachoonekana kukubalika na wengi.

“Kuna kikundi cha watu kinaweza kuandamana na bila kuwa na kibali na wala hakuna mauaji yanayotokea…lakini wengine wakiomba kibali wananyimwa je, huoni kuwa hapa tulipo sasa ni pa hatari zaidi kuliko huko tuendako,” alihoji.

Shinikizo la kumtaka Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi, Dk. Emmanuel Nchimbi, kujiuzuru nafasi hiyo limetolewa pia naKatibu Mkuu wa Chama cha CCK, Renatus Muabhi kutokana na kushindwa kwake kuwadabisha askari wake waliohusika na tuhuma za mauaji ya raia, likiwemo la kuuawa kwa mwandishi Daud mwangosi.

Muabhi alisema, mbali ya kujiuzulu kwa Nchimbi, pia makamanda wa polisi wa mikoana askari wao wanapaswa kuona umuhimu wa hatari ya uzembe na ukiukwaji wa sheria za polisi unaosababisha vitendo vya mauaji ya raia.

Alisema, watanzania bado wanalihitaji jeshi hilo, hivyo ni vema kutizamwa upya mfumo wa maadili ya taasisi hiyo ili kuondokana na wale wakorofi ambao hujichukulia sheria mkononi, lakini kwa mfumo mbovu wa kubebana na kufanya sifa ya idara hiyo kuporomoka na kupoteza imani kwa wananchi.

SAU yamshukia Tendwa
Nacho Chama Cha Sauti ya Umma (SAU), kimemshukia Msajili wa Vyama vya Siasa Nchini, John Tendwa kikimtaka afute kauli yake ya kutishia kukifuta Chama cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA) kwa madai ya kuhusika na mauaji ya raia.

Mwenyekiti wa taifa wa SAU, Paul Kyara alisema Tendwa anapaswa kutoa tafsiri ya sheria ya vyama vya siasa na ile ya polisi, kwa kuwa kukinzana kwa sheria hizo ndio chanzo cha vurugu na mauaji yanayotokea.

“Tangu kuanza kwa mfumo wa vyama vingi nchini mwaka 1992, idadi kubwa ya Watanzania wameshapoteza maisha kutokana na vurugu zinazoibuka katika mikutano ya hadhara, ikiwa ni pamoja na matukio ya hivi karibuni yaliyotokea mkoani Iringa, Morogoro, Singida na Arusha,” alisema.

Kyara alisema sura ya 258 ya sheria ya vyama vya siasa ya mwaka 1993 na ile ya polisi iliyofanyiwa marekebisho 2002, ndio chanzo cha tatizo.

Kyara alisema, moja ya kazi ya chama cha siasa ni kufanya mikutano, lakini vyama vimekuwa vikikutana na vikwazo, hivyo ni vyema kuweka utaratibu maalum hata kubadilishwa kwa sheria hizo mbili ili kuondoa tofauti inayojitokeza.

Alisema kuwa sheria ya vyama vya siasa inatoa uhuru kwa vyama vya siasa kufanya mikutano ya hadhara na maandamano na hutakiwa kutoa taarifa polisi ndani ya saa 48 kabla ya maandamano hayo kufanyika.

Alisema sheria hiyo ndiyo inayochangia kuwepo kwa mvutano unaopelekea kutokea kwa mgogoro kwa sababu chama hujiona kuwa na haki huku polisi nao wakijiona kuwa na haki ya kulinda amani ya raia.

Mwenyekiti huyo, alisema kuwa ni lazima ufumbuzi wa haraka upatikane kabla madhara hayajawa makubwa zaidi kwa kuwa hata Chama Cha Wananchi CUF nacho kimeanza mikutano yake katika mikoa mbalimbali.

Alisema suala hili lisipoangaliwa kwa upana kuna hatari ya taifa kukumbwa na maafa makubwa kwa kuwa vyama vya upinzani vitafanya mikutano yake kwa lazima, ambapo polisi nao wataonesha ubabe na hivyo kuzua balaa.

TEC wavuta pumzi
Wakati viongozi hawa wakieleza hofu yao, Baraza la Maaskofu Katoliki Tanzania (TEC), limekataa kusema lolote kuhusiana na hali tete katika taifa.

Katibu Mkuu wa baraza hilo, Padri Antony Makunde alipotakiwa kutoa msimamo wake, alisema kwa hali ilivyo katika nchi, hawezi kusema lolote.

Alidai kwamba mambo yanayoendelea katika taifa hili hususan mauaji ya raia yanahitaji kutolewa kauli na rais wa baraza lake, na sio mtu mwingine yeyote akiwemo yeye.

Hata hivyo, jitihada za kumpata Rais wa TEC, Askofu wa Jimbo la Iringa, Mhashamu Ngalalekumtwa zilikwamba baada ya simu yake kutopatikana.

Msimamo wa CHADEMA
Wakati hayo yakijiri, CHADEMA kwa upande wake, kimetoa msimamo wa kukataa kwanza, kamati ya uchunguzi iliyoundwa na Waziri Nchimbi kuchunguza mauaji ya Mwangosi huko Iringa, lakini pia kinakusudia kuwafungulia mashitaka ya mauaji makanda wa polisi wa mikoa ya Morogoro na Iringa.

Akizungumza hayo mbele ya waandishi wa habari jana mjini Morogoro, Ofisa Habari wa CHADEMA, Tumaini Makene aliongeza kufikishwa mahakamani kwa askari mmoja anayetuhumiwa kumuua Mwangosi hakuwezi kumaliza kiu ya wapenda haki, akidai kuwa watuhumiwa wengine bado wanatamba mitaani.
“Uamuzi wa Kamati Kuu iliyokaa karibuni ni kwamba RPC wa Iringa, Michael Kamuhanda akamatwe na afikishwe mahakamani kwa tuhuma za mauaji ya Mwangosi, kwa sababu yeye ndiye alikuwa akiongoza operesheni wakati polisi wanafanya mauaji hayo, alikuwa field.

“Lakini pia CHADEMA tunasema maaskari wote wanaoonekana kwenye picha wakati Mwangosi anakamatwa, kupigwa na kuuwawa ni watuhumiwa wanapaswa kukamatwa na kufikishwa mahakamani kwa mauaji, chini ya hapo ni kuwahadaa wapenda haki Tanzania na duniani kote ambao sasa wanaanza kuiangalia Tanzania kwa jicho la aina yake kutokana na mauaji yanayofanya na vyombo vya dola,” alisema Makene.

No comments:

Post a Comment