To Chat with me click here

Saturday, September 8, 2012

POLISI WAKOROGANA


ANAYETUHUMIWA KUUA MWANDISHI AKWAMA KUFIKISHWA MAHAKAMANI
 
WINGU jeusi limeendelea kutanda ndani ya Jeshi la Polisi mkoani Iringa baada ya baadhi ya askari mkoani humo kunyoosheana vidole kuhusu tukio la polisi kuua mwandishi, huku baadhi yao wakimlaumu Kamanda wa Polisi wa Mkoa (RPC), Michael Kamuhanda.

Askari kadhaa waliozungumza na gazeti hili kwa siri jana, walisema kama RPC angesikiliza ushauri wa Mkuu wa Upelelezi wa Mkoa (RCO) kuhusu namna ya kukabiliana na wanachama wa CHADEMA, maafa yasingetokea.

Walisema Kamuhanda ndiye aliwaamuru askari wake kuwakamata viongozi wa CHADEMA waliokuwa kwenye mkutano wa ndani wa ufunguzi wa tawi katika Kijiji cha Nyololo, kwa maelezo kuwa hakuwaruhusu kufanya hivyo.

“Kama mnakumbuka, RCO mwanzo alizielewa hoja za CHADEMA juu ya vikao vyao vya ndani, lakini alipokuja RPC hali ikabadilika kutokana na kupewa maelezo na mkuu wetu wa kikosi cha kutuliza ghasia mkoa,” alidokeza mmoja wao.

Walisema kwamba hata katika tawi la kwanza walilofungua viongozi wa CHADEMA, RCO alifika lakini hakuwashambulia. Wakati wakifungua tawi la pili, ndipo RPC akafika, na amri zikatolewa kuwashughulikia viongozi na wanachama wa CHADEMA.

Kwa maelezo ya polisi hao, viongozi na wanachama wa CHADEMA hawakuwa wameleta fujo yoyote, na kwamba kama polisi wangelinda tu mikutano yao yaliyotokea yangeweza kuepukwa.

Askari hao walisema inasikitisha kwamba uamuzi wa mtu mmoja umelifanya jeshi zima lionekane baya mbele ya umma; na kwamba hata wao wanatii amri kwa sababu kazi yao haiwaruhusu kuhoji amri za wakubwa wao.

Baadhi yao walisema hata maneno na vitisho vinavyofanywa na baadhi ya viongozi wa serikali, kwamba CHADEMA kina vurugu, ni uonevu na propaganda za kisiasa, kwani vurugu zilitokea pale CHADEMA walipoanza kutawanywa.

Habari ambazo hazijathibitishwa kutoka mkoani humo zinadai kuwa baadhi ya askari waliohusika kwenye vurugu hizo si polisi halali wa jeshi hilo, bali ni vijana wa mtaani ambao walivishwa sare kwa lengo la kuwadhibiti CHADEMA, ndiyo maana walikuwa wakibabaika katika matumizi ya silaha.

Wakati huo huo, jeshi hilo jana lilishindwa kumfikisha mahakamani askari polisi anayetuhumiwa kufyatulia bomu lililomchanachana na kumuua mwandishi wa kituo cha Channel Ten, Daudi Mwangosi.

Awali, taarifa za mtuhumiwa huyo kupandishwa kizimbani zilizagaa kila kona; gazeti hili likapiga kambi katika Mahakama ya Hakimu Mkazi wa Mkoa, lakini mtuhumiwa hakuletwa mahakamani.

Jana gazeti hili liliripoti taarifa za kukamatwa kwa siri na kuhojiwa kwa askari watano kati ya saba akiwamo yule anayetuhumiwa kumuua marehemu Mwangosi.

Tanzania Daima lilidokezwa kuwa askari wanaoshikiliwa kwa mahojiano zaidi ni wale walioonekana kwenye picha mbalimbali za magazeti na mitandao wakimpiga marehemu huyo kabla ya kumsababishia kifo.

Habari za ndani zilieleza kuwa mtuhumiwa huyo wa mauaji hakuweza kufikishwa mahakamani kama ilivyotarajiwa kutokana na kuendelea kutoa maelezo mbele ya mlinzi wa amani.

Chanzo cha taarifa kilidai kuwa utaratibu huo wa kutoa maelezo ulianza juzi na huenda mtuhumiwa atafikishwa mahakamani Jumatatu.

“Suala la mauaji ni kubwa, si kama mashitaka ya mwizi wa kuku au karanga. Hivyo, juzi na jana yule bwana alikuwa anaendelea kutoa maelezo yake kwa mlinzi wa amani. Sasa suala la kukiri kuua au kutokuua litabaki katika moyo wake,” kilisema chanzo hicho.

No comments:

Post a Comment