To Chat with me click here

Saturday, September 8, 2012

WAZEE, BAWACHA WALAANI MAUAJI


BARAZA la Wanawake la Chama cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA) na lile la Wazee kwa pamoja yamelaani vikali kitendo cha Jeshi la Polisi mkoani Iringa kumuua mwandishi wa habari wa kituo cha Channel Ten, Daudi Mwangosi.

Naibu Katibu Mkuu wa BAWACHA Taifa, Subira Waziri, alieleza kuwa wanalaani nguvu zote za mauaji yanayoendelea nchini yakifanywa na Jeshi la Polisi ambao waliamini kuwa ni walinzi wa wananchi na mali zao.

“Tulikuwa tunaliamini Jeshi la Polisi, lakini kutokana na nguvu zinazotumika za kuua watu wasio na hatia na kugeuka kuwa ndio wauaji wakubwa, hatuna tena imani nao,” alisema Subira.

Aidha, BAWACHA wameeleza kushangazwa na kauli ya Msajili wa Vyama vya Siasa, John Tendwa ya kutishia kuvifuta vyama vya siasa ambavyo vitasababisha vurugu na mauaji katika mikutano yao.

“BAWACHA tunatambua kuwa kauli hiyo inailenga CHADEMA ili kutekeleza dhamira ovu ya Tendwa aliyotumwa na Serikali ya CCM. Tunamtaka msajili awaeleze Watanzania iwapo kauli yake hiyo haitatumiwa serikali kupitia polisi ili kusababisha vurugu kwenye mikutano yetu?” alihoji.

Nalo baraza la wazee wa CHADEMA, limewataka wazee wote nchini kuungana pasipo kujali itikadi zao kwa ajili ya kumshinikiza Rais Jakaya Kikwete atoe tamko juu ya mauaji yanayoendelea nchini hususan yale yanayofanywa na vyombo vya dola.

Taarifa ya wazee hao kwa vyombo vya habari iliyosainiwa na Kaimu Katibu wa baraza hilo, Erasto Gwota, ilisema kuwa imeshangazwa na ukimya wa Rais Kikwete ambaye ndiye mkuu wa nchi hasa katika mambo mazito yanayoikabili nchi.

“Sisi wazee wa CHADEMA tunawaomba wazee wote nchi tuungane tumwambie kijana wetu kuwa hali inayoendelea haitaweza kuiacha nchi salama na yeye kama kiongozi wetu ana jukumu la kuingilia kati na kutoa kauli yake ili iwe faraja na njia kwa Watanzania,” ilisema.

Gwota alisema, baraza hilo linatambua kuwa kuna mpango madhubuti ambao umeandaliwa na CCM kuwadhuru wananchi wanaojitokeza katika mikutano ya vyama vya upinzani kwa lengo la kuwatisha.

Alieleza kuwa serikali ya CCM imeshindwa kusimama katika misingi iliyoachwa na Baba wa Taifa hayati Mwalimu Julius Nyerere ya kukubali kukosolewa na kujisahihisha na badala yake imeamua kutumia nguvu katika kujihalalisha kutawala.

Tanzania Daima

No comments:

Post a Comment