To Chat with me click here

Monday, September 24, 2012

SHIBUDA AWATAKA WANASIASA KUEPUKANA NA MDUDU SHETANI WA KUJINUFAISHA WENYEWE


Mo Blog: Shibuda umekuwa mwasiasa kwa siku nyingi nini rai yako kwa viongozi wenzio wa kiasiasa.?

Shibuda: Napenda kutoa rai kwa vyama na viongozi wa kisiasa ambavyo viko karibu 21 hapa Tanzania, la kwanza kila chama kijifanyie tathmini, kinawajibika vipi kutekeleza mipango ya kuendeleza amani na utulivu katika hii nchi.

Vinatekeleza mipango gani? Na kila chama kifanye tathmini kijiuze mambo gani ambayo ni makosa kwa ustawi na maendeleo ya nchi yetu inaoongozwa na kulindwa na tabia, mila na desturi za mtanzania.

Vyama vya siasa viwe na wito unaoitwa ‘kwa maslahi ya umma’ na viongozi pia watekeleze wito unaoitwa kwa maslahi ya umma.

Mo Blog: Kwani una shaka na baadhi ya vyama?

Shibuda:Vyama ambavyo vina mdudu shetani anayeitwa ibilisi wa kujenga tafrani, migongano, misuguano au vyama vinavyoitwa ‘chama kampuni’ kwa maslahi binafsi, havistahiki kuwa sehemu moja wapo ya mbegu ya kuzalisha amani.

Hivyo watanzania tutafakari, tusemezane, tutazame viwango vya kila chama, katika vyama 21 kwamba je? Tija ya kila chama ni kwa kujenga ustawi na maendeleokwa jamii? Ili mwaka kesho tusherehekee tena siku ya amani duniani.


Mo Blog: Lipi la msingi ungependa kusisitiza kwa watanzania?

Shibuda: Jambo la msingi ningependa kusisitiza ni kwamba watanzania tuanze kupambanua, tuanze kutafakari, tuanze kusemezana kuwa hivi vyama 21 ni mapumulio dhidi ya majinamizi na dhuluma ambazo taifa hili limekuwa nazo kwa muda mrefu dhidi ya ustawi wa jamii?

Mimi ningependa kusisitiza ya kwamba watanzania wenzangu tupokee vyama 21 kuwa ni changamoto ya mchakato wa kuwa tuna sauti ya umma, yenye mti mmoja wenye mchipuo unaoitwa uzalendo, uaminifu na utiifu kwa maslahi ya umma.
 Matawi haya 21 yaonekane kweli yanawakilisha maslahi ya umma.

Mo Blog: Lakini kwani una shaka na lipi au na nani?

Shibuda: Lakini kama kuna watu wamejiona tu ya kwamba wana mashinikizo na matatizo yao binafsi wakasema kwamba tunaanzisha chama, wajue kuwa hiyo ni SACCOS ambayo haina ustawi na maendeleo ya nchi bali wanatafuta michango, wanatafuta wapate ruzuku wapate kuchangiwa kwa maslahi yao binafsi.

Chama lazima kitambulishe juhudi zake, jitihada zake, dhamira, azma ya kuhakikisha ya kwamba wana wito wa kuwatumikia watanzania kwa ari moja, nguvu mpya na kuhakikisha kweli ni uamsho kwa ustawi na maendeleo ya Tanzania.

 
Mo Blog: Kwani unashaka kuwa nini kitatokea yasipofanyika hayo unayoyasema?

Shibuda: Ninachokisema ni kwamba la si hivyo tutakuwa na vyama vingi ambavyo ni sawasawa na nyumba ambayo ina bati moja lakini limetoboka toboka na linaingiza mifereji ya maji ndani ya nyumba, badala ya kupata sakafu iliyokavu, tunajikuta tunahamisha vitanda kupeleka huku na kule lakini kila unakopeleka kitanda chako kunavuja, hatutaki watanzania imani zao ziwe za kutangatanga.

Mo Blog: Kwa kumalizizia lipi neno unaachia watanzania?

Shibuda: Kila mtanzania apate mgutuko anapoona viongozi wa chama hawana maadili mema, hawana wito, hawana vitendo, hawana kauli zinazoshabihiana na mtu mwenye wito wa kutumikia au kama shekhe ama askofu hana vitendo vinavyoshabihiana na imani yake, basi ujue huyo ni mtu tu sawa na chui aliyevaa ngozi ya kondoo ili aingie kwenye zizi lakini dhamira yake ni kuwatafuna.

Tujitahadhari na watu ambao wamekuja na jina la siasa lakini kumbe ni chui mla watu.

No comments:

Post a Comment