To Chat with me click here

Saturday, September 8, 2012

MAFISADI WAILIPE DOWANS - MNYIKA


SIKU moja baada ya Mahakama Kuu Kanda ya Dar es Salaam, kulitupilia mbali ombi la Shirika la Ugavi wa Umme nchini (TANESCO) la kutaka izuie utekelezwaji wa ulipwaji wa fidia ya Kampuni ya Dowans Tanzania Ltd, Waziri Kivuli wa Nishati na Madini, John Mnyika, amesema mafisadi waliohusika ndio wabebeshwe hasara hiyo badala ya wananchi.

Juzi, mahakama hiyo, ilitupa ombi la TANESCO lililokuwa likiomba itoe amri ya kuzuia utekelezwaji wa ukazaji wa hukumu ya mahakama hiyo iliyoruhusu tuzo ya dola 65,812,630.03 za Marekani iliyotolewa na Mahakama ya Kimataifa ya Usuluhishi wa Migogoro ya Kibiashara (ICC) mwaka 2010 kwa Kampuni ya Dowans Hodlings SA (Costa Rica), sasa Dowans Tanzania Ltd isajiliwe hapa nchini.

Mnyika ambaye pia ni Mbunge wa Ubungo (CHADEMA), alitoa kauli hiyo jana kupitia taarifa yake aliyoisambaza kwenye vyombo vya habari akisema kuwa serikali isitumie kizingizio cha uamuzi wa mahakama kuharakisha mpango wa kulipa Dowans kwa fedha za walipa kodi wa Tanzania.

Vile vile, Mnyika alisema kuwa ikiwa serikali ya Rais Jakaya Kikwete imezidiwa na Dowans kwa sababu ya kujiingiza katika mikataba mibovu, inapaswa kuwabebesha deni hilo wazembe, mafisadi na waliokuwa wakihujumiana na kusababisha hasara hiyo.

“Serikali kupitia Waziri wa Nishati na Madini, Prof. Sospeter Muhongo, anapaswa kueleza ni hatua gani ilichukua kutoka TANESCO ilipowasilisha Mahakama ya Rufani taarifa ya kusudio la kupinga hukumu iliyotolewa na Jaji Emilian Mushi, Septemba 28 mwaka jana ikiruhusu tuzo hiyo isajiliwe,” alisema.

Aliongeza kuwa, Mwanasheria Mkuu wa Serikali naye anapswa kueleza ni kiasi gani cha fedha kilichotumika kwenye kuendesha kesi za Dowans na IPTL mpaka sasa na hatua zilizochukuliwa dhidi ya mawakili wa TANESCO na makampuni binafsi yanayotuhumiwa kusababisha mzigo mkubwa wa gharama za kesi ambazo serikali inashindwa.

“Ni muhimu umma ukafahamu kuwa kwa mwaka wa fedha 2011/2012 pekee, jumla ya sh bilioni 10 zimetumika kwa ajili ya gharama za kuendesha kesi hizo kwa kuilipa Kampuni ya Rex Attorneys na makampuni mengine ambayo kwa nyakati mbalimbali yamekuwa yakiiwakilisha serikali na TANESCO,” alisema Mnyika.

Alishauri kuwa hukumu ya juzi inapaswa kuibua tena mjadala uliodumu kwa miaka minne, kuanzia mwaka 2008 tangu yalipopitishwa maazimio 23 ya Bunge juu ya mkataba baina ya TANESCO na Kampuni ya Richmond Development Company LLC ikiwamo kuhusu mkataba na Dowans.

Alisema katika mazingira hayo, Waziri Muhongo anapaswa kueleza kwa umma ni mabilioni mangapi yamelipwa na TANESCO mpaka hivi sasa kwa kampuni hiyo na nyingine.

“Kama hoja binafsi niliyoiwasilisha ofisi ya Bunge mwaka jana kutaka utekelezaji wa maazimio yote yaliyobaki kuhusu mkataba kati ya TANESCO na Richmond ingejadiliwa bungeni, hatua zaidi zingechukuliwa kwa mafisadi na wahujumu uchumi waliohusika,” alisema Mnyika ambaye pia ni Mkurugenzi wa Habari na Uenezi wa CHADEMA.

TANESCO wanena
Wakati huo huo, TANESCO imesema kuwa hakuna hukumu yoyote iliyotolewa na Mahakama Kuu kuamuru shirika hilo kuilipa Dowans dola za Marekani milioni 96.

Taarifa iliyotolewa jana jioni na ofisi ya uhusiano ya TANESCO, ilisema kuwa kilichoamriwa na Mahakama Kuu ni kwamba Mahakama Kuu haina mamlaka ya kusikiliza utekelezaji wa hukumu ya ICC, hivyo mamlaka hayo yapo katika Mahakama ya Rufaa.

“Kwa sasa TANESCO imepeleka ombi la kuzuia utekelezaji wa hukumu ya Mahakama ya ICC kwenye Mahakama ya Rufaa Tanzania na hatimaye kuendelea na taratibu za kukata rufaa,” ilisema taarifa hiyo.

Tanzania Daima

No comments:

Post a Comment