To Chat with me click here

Saturday, September 22, 2012

MWANAMAMA AUKWAA URAIS WA AFRIKA


Jaji Sophia Akuffo
JAJI Sophia Akuffo kutoka Ghana amechaguliwa kuwa Rais wa Mahakama ya Haki za Binadamu ya Afrika akichukua nafasi ya Jaji Gerard Niyungeko kutoka Burundi aliyemaliza muda wake baada ya kutumikia nafasi hiyo kwa vipindi viwili tofauti.

Mwanamama huyo ambaye alikuwa makamu wa rais wa mahakama hiyo katika muhula uliopita, alichaguliwa kushika nafasi hiyo juzi mara baada ya kumalizika shughuli ya kuwaapisha majaji wapya wawili: Ben Kioko kutoka Kenya na El Hadji Guissé kutoka Senegal kwenye makao makuu ya mahakama hiyo yaliyoko jijini hapa.

Taarifa iliyotolewa kwa vyombo vya habari na afisa habari wa mahakama hiyo, Jean-Pierre Uwanone, ilisema kuwa uchaguzi wa makamu wa rais ambao ulikuwa uende sanjari na huo wa rais utafanyika baadaye ingawa hakutaja ni lini hasa.

Jaji Akuffo aliteuliwa kuwa jaji wa mahakama hiyo mwaka 2006 kwa kipindi cha miaka miwili kabla ya kuteuliwa tena kwa kipindi kingine cha miaka sita mwaka 2008 ambapo mwaka huohuo alichaguliwa kuwa makamu wa rais wa mahakama hiyo kwa kipindi cha miaka miwili, mwaka 2010 alichaguliwa tena kuendelea na wadhifa huo mpaka juzi alipochaguliwa kuwa rais wa mahakama hiyo.

Jaji huyo kutoka mahakama ya juu ya Ghana (Supreme Court of Ghana) pia ni mjumbe wa taasisi mbalimbali ikiwemo Kamati ya Ushauri ya Taasisi ya Elimu ya Masuala ya Mahakama ya Jumuiya ya Madola (Committee of the Commonwealth Judicial Education Institute).

Rais aliyemaliza muda wake, Jaji Niyungeko (Burundi), alitumikia mahakama hiyo kama rais kwa vipindi viwili tofauti kikiwemo kile cha 2006/08 ambapo alichaguliwa tena kushika nafasi hiyo 2010/12 ambapo kwa mujibu wa taratibu za mahakama hiyo nafasi hiyo huweza kushikiliwa kwa vipindi viwili tu.

Awali uchaguzi huo ulitanguliwa na zoezi la kuwaapisha majaji wapya wawili, Kioko kutoka nchini Kenya na Guissé kutoka nchini Senegal zoezi lililoshuhudiwa na wageni mbalimbali ambapo kwa sasa mahakama hiyo itakuwa na majaji 10 kutokana na Jaji Joseph Mulenga kutoka Uganda kufariki mwezi uliopita.

Kwa mujibu wa mkataba wa uanzishwaji wa mahakama hiyo mwenye jukumu la kuteua majaji wa mahakama hiyo ni mkutano wa wakuu wa nchi za Afrika ambapo majaji hao hutumikia mahakama hiyo kwa kipindi cha miaka sita.

No comments:

Post a Comment