To Chat with me click here

Monday, September 17, 2012

WABUNGE WA CCM KIKWAZO CHA MAENDELEO


Mbunge wa Viti Maalum-CUF, Mkoa wa Tanga Mhe. Amina Mwidau

Wingi wa wabunge kutoka Chama cha Mapinduzi katika Bunge la Tanzania, umechangia kwa kiwango kikubwa kukwama kwa maendeleo ya nchi.

Mbunge wa Viti Maalum, Amina Mwidau (CUF), amesema hayo juzi wakati akikabidhi mashine ya kusukumia maji yenye thamani ya sh milioni 5, kwa wananchi wa kijiji cha Mwera katika wilaya ya Pangani mkoani Tanga ikiwa ni sehemu ya utekelezaji wa ahadi zake kwa wakazi hao.

Alisema kukosekana kwa wabunge wengi wa upinzani, kumewafanya wabunge wa CCM kuyaacha mambo yaende jinsi yalivyo na hivyo kusababisha nchi kuwa na matatizo mengi.

“Leo nchi imekuwa na matatizo kila kona kutokana na kukosekana wabunge wa kweli ambao wana uchungu wa kupigania mgao wa rasilimali ulio sawa kwa wananchi pia kuwatetea wananchi na ninayasema haya mchana kweupe, idadi ya wabunge wengi wa CCM imekuwa ni kikwazo kwetu sisi wapinzani.

“Hata nanyi wananchi wa Mwera mnalitambua hilo, na hata mbunge mwenzangu wa CCM wa jimbo hili hana muda wa kurudi tena tangu mlipomchagua hata leo hii mna tatizo la maji kutokana na mota ya kusukumia maji kuungua na hana habari nanyi.

Amina alisema ili kupambana na mfumo huu mbovu ulioandaliwa na CCM kutokana na sera zake mbovu Watanzania wanahitaji kujenga nchi kwa kuwa na viongozi jasiri kama Profesa Lipumba ambao kwa muda mrefu wamekuwa wakipigania ustawi na haki za Watanzania.

Mbunge huyo aliwataka wananchi hao kukiunga mkono chama chake ili kiweze kujenga demokrasia na ukombozi wa kweli nchini.

Alisema amefikia hatua hiyo baada ya kutambua kero kubwa ya maji inayowakabili wananchi hao, ambapo hicho kilikuwa kipaumbele chake katika kampeni zake wakati alipokuwa akiomba nafasi hiyo.

Amina aliwaasa wananchi hao, kuhakikisha wanakikataa Chama cha Mapinduzi (CCM), katika masanduku ya kura itakapofika mwaka 2015 ili Bunge liwe na wabunge wengi kutoka vyama vya upinzani watakaoweza kuwakomboa wananchi kutoka kwenye umaskini uliokithiri, uliosababishwa na chama hicho.

“Ninakabidhi mashine hii yenye thamani ya zaidi ya sh milioni 5, ili kutatua kero ya maji katika kijiji hiki cha Mwera, ninajua uchungu kwani wanaopata taabu ni wanawake wenzangu na watoto ambao hutumia muda mwingi kutafuta maji badala ya kufanya shughuli za uzalishaji,” alisema Amina.

No comments:

Post a Comment