To Chat with me click here

Wednesday, September 26, 2012

HIVI KWELI JK HAJUI KAMA CCM IMEKUFA?

MWENYEKITI wa Chama Cha Mpinduzi (CCM), Rais Jakaya Kikwete, bado haamini kama chama anachokiongoza kimekufa. Badala yake ametoa tambo kuwa wale wote wanaokichulia kifo, watakufa wao kabla ya chama.

Kikwete anapima uhai wa CCM kwa kuangalia wingi wa wanachama wanaojitokeza kuwania nafasi mbalimbali za uongozi ndani ya chama bila kujali kama wana sifa stahiki au hapana.

Kauli hii ya mwenyekiti ni nzito yenye kuhitaji ushupavu katika kuitamka hasa unapozungumzia na kusifu kitu dhaifu ukiamini kuwa bado kiko imara.

Pengine nikuulize wewe unayesoma makala hii, hivi ni kweli Rais Kikwete hajui kuwa CCM imekufa siku nyingi hasa baada ya yeye kuchukua wadhifa wa mwenyekiti?

Nauliza hivyo kutokana na utata wa kauli ya Rais Kikwete. Huyu anajaribu kujipa matumaini ambayo hayapo tena. Kama ni kupima uhai wa CCM kwa sasa ni sawa na mgonjwa aliyeko mahututi ICU akipumulia mashini yaani nusu mfu.

Kwanini Kikwete anasema CCM haitakufa wakati imekuta tayari. Hivi anaweza kuifananisha miiko ya chama kwa sasa na ili ya miaka kadhaa iliyopita. Kweli anaamini anaongoza chama cha wakulima na wafanyakazi wanyonge?

CCM aliyorithishwa Kikwete ilikuwa ya wafanyabiashara, mafisadi na uongozi wa kupokezana kifamilia? Kama si hivyo kwanini mwenyekiti huyo amediriki kuwahadaa wajumbe wa Kamati Kuu kuwa chama hicho hakitakufa, anataka kife mara ngapi?

Rais amesahau kuwa hata dhana ya kujitakasa upya aliyoiasisi mwaka jana ya kujivua gamba imeshindikana kutekelezeka kwa sababu mafisadi aliyokuwa amewalenga kuwang’oa wamejijengea mizizi kwenye chama kuliko yeye.

Jamani mwenyekiti huyu anataka tumpe mifano gani zaidi ili atambue kuwa CCM anayoiongoza imekufa, haina dira, mwelekeo na sasa imeishia kudandia hoja za wapinzani ndani na nje ya Bunge ikijitapa kuwa zimeasisiwa kwao?

CCM ya leo ambayo Kikwete bado haamini kama imekufa, ina muundo wa viongozi wasiyo na dira ya kuwaunganisha wanachama bali kutengeneza makundi ya uchaguzi ujao.

Wakati wa CCM hai, viongozi wake waliikwepa sana rushwa, walijali uzalendo na maadili ya taifa, hawakupena madaraka kifamilia, uwazi ulitawala hasa kwenye chaguzi za ndani na michango ya kuendesha chama. Rais Kikwete anataka kutuambia kuwa CCM ya sasa iko hivyo?

Leo CCM ambayo mwenyekiti wake haamini kama imekufa, mkewe anagombea ujumbe wa Halmashauri Kuu (NEC) kupitia Lindi na mwanaye anagombea kupitia wilayani Bagamoyo. Hivi ni kweli familia nzima ina wito wa siasa na lazima wote waingie huko?

Pengine Rais Kikwete haamini kifo cha CCM kwa vile anaiona bado iko madarakani. Lakini hakika hicho si kipimo kwani hata uchaguzi ujao wanaweza kushinda. Swali la msingi hapa ni wamefikaje uongozini, wana mipango endelevu, uwezo wa kusimamia sera na ilani yao?

Tangu mwaka 2005 kwenye uchaguzi mkuu, aliahidi maisha bora kwa kila Mtanzania, akatangaza kutengeneza ajira zaidi ya milioni mbili. Leo maisha ya Watanzania ni magumu kuliko alivyoipokea nchi kutoka kwa mtangulizi wake, Benjamin Mkapa. Sasa hapa Kikwete anataka CCM ife mara ngapi?

CCM iliyoaminiwa na kuahidi kupambana na rushwa, uhalifu, dawa za kulevya, umasikini, kuinua wakulima, kusomesha wanafunzi kwa kuboresha sekta ya elimu, afya, maji safi na salama mjini na vijijini halafu ikashindwa, Kikwete atasemaje haijafa?

Mwenyekiti wa CCM anataka maono gani kujua anaongoza chama mfu ikiwa hata uwezo wa wabunge wake bungeni umekuwa na shaka, kutokana na kupitisha kila kitu kwa makofi na vigelegele halafu baadaye wanajuta?

Kama kweli CCM ingekuwa hai kama anavyoamini Rais Kikwete, leo isingekuwa na makundi ya wabunge hadi ya mawaziri wanaosutana hadharani kwa tuhuma tofauti kwa sababu tu ya kupigania urais mwaka 2015.

CCM ingekuwa hai isingesita kuwachukulia hatua mawaziri na wanachama wake wanaotuhumiwa kwa rushwa na ufisadi, isingehonga mahindi kwenye kampeni za uchagzu mdogo kama ilivyofanya Igunga, Katibu Mkuu wake na baadhi ya mawaziri wasingewatisha wapiga kura.

Rais Kikwete anajua wazi kuwa kwa sasa ili uweze kuwavuta wananchi kuhudhuria mkutano wa CCM lazima ukodi wanamuziki au vikundi vya uchekeshaji kwaajili ya kutumbuiza, vinginevyo ni aibu tupu.

CCM kama ingekuwa imara inatenda yale iliyoahidi bila shaka Waziri Mkuu, Mizengo Pinda, asingezomewa mkoani Mwanza, badala yake angesomewa risala za pongezi na kupigiwa makofi. Tafakari!

No comments:

Post a Comment