To Chat with me click here

Saturday, December 1, 2012

CHIKAWE AMGWAYA LISSU


Mhe. Tundu Lissu

Wakati Dk. Slaa akiibua tuhuma nzito kwa Serikali ya Rais Kikwete, zenye kuhitaji majibu stahili, Waziri wake wa Katiba na Sheria, Mathias Chikawe, ameshindwa kutolea ufafanuzi hoja zilizoibuliwa na Lissu kuhusu baadhi ya majaji, aliodai waliteuliwa bila kufuata utaratibu.

Chikawe ambaye kimsingi ni miongoni mwa wasaidizi wa Rais Kikwete, anayepaswa kuitetea serikali yake, alipoulizwa juu ya hoja hiyo aliishia kusema, “hoja za Waziri Kivuli wa Sheria na Katiba, Tundu Lissu nimezisikia, nimezisoma na sina maoni yoyote juu ya hilo.”

Akizungumza jana, Waziri Chikawe alisema: “Ungekuja ofisini, nipo safari kwa sasa, hata hivyo hoja za Lissu nimeziona, nimezisoma na sina ‘comment’ kwa sasa.”

Ni waziri huyo huyo, ambaye aliliambia Bunge kuwa Tume ya Mahakama inamshauri rais wakati wote na kwamba hakuna ukiukwaji wowote uliofanyika katika uteuzi wa majaji.

Alisema haijatokea hata siku moja rais akamteua jaji wa Mahakama Kuu bila kuzingatia mapendekezo ya Tume ya Uajiri ya Mahakama.

Awali akijibu hoja za Lissu bungeni, Mwanasheria Mkuu wa Serikali, Jaji Fredrick Werema, ambaye jana simu yake iliita bila majibu, alimuonya Lissu kuwa ataburuzwa kwenye Kamati ya Maadili ya Bunge kwa ‘taarifa potofu anazoziwasilisha bungeni’.

Lakini mapema wiki hii, Lissu alirejea hoja yake na kusisitiza kuwa alishatoa maelezo hayo hata katika Kamati ya Haki, Kinga na Madaraka ya Bunge inayoongozwa na Brigedia mstaafu Hassan Ngwilizi.

“Nilieleza jinsi rais alivyofanya uteuzi wa baadhi ya majaji pasipokupata ushauri wa Tume ya Utumishi wa Mahakama. Wamekuwa wakijibu kiujumla, mimi niliwataja kwa majina yao na hata hili nilieleza katika Kamati ya Ngwilizi ambayo taarifa yake haikuwekwa hadharani pasipo sababu za kueleweka,” alisema.

Alipotafutwa jana, Lissu ambaye pia ni mnadhimu wa kambi ya upinzani bungeni, alisema kuwa kwa sasa serikali haiwezi kusema chochote zaidi ya kukubali, kwani tayari ameshawapa ushahidi kwenye Kamati ya Bunge.

Alisema hoja yake kuwa kuna ukiukwaji wa katiba inaungwa mkono na nyaraka za ndani ya serikali na hasa Ofisi ya Rais, Ikulu yenyewe, ambayo Desemba 6, 2007, mkutano kuhusu ajira ya majaji waliostaafu ulifanyika Ikulu chini ya uenyekiti wa Katibu Mkuu Kiongozi wakati huo, Philemon Luhanjo.

Lissu aliongeza kuwa, wajumbe wengine walikuwa pamoja na Mwanasheria Mkuu, Johnson Mwanyika na Naibu wake, Sazi Salula, Katibu Mkuu Utumishi George Yambesi, Msajili wa Mahakama ya Rufani, Sophia Wambura na Susan Mlawi wa Sekretarieti ya Baraza la Mawazi.

“Serikali iseme suala hili ni la kweli au si la kweli, na wale niliowataja kuwa hawana sifa kwa mfano ya elimu serikali iseme wamesoma wapi, na kwanini kulikuwa na kikosi kazi kwa ajili ya majaji wanaoajiriwa kwa mkataba ikiwa mimi sijasema kweli,” alisema.

Alisema kuwa anazidi kuuliza inawezekanaje jaji asome shahada ya kwanza ya Sheria Chuo Kikuu Huria sasa, kwamba aliteuliwaje kuwa jaji, maana hiyo ndio sifa ya msingi?

No comments:

Post a Comment