To Chat with me click here

Friday, October 5, 2012

MOTO WA CHADEMA KUWASHWA ARUSHA

WAJIBODOA KUIPIKU CCM UCHAGUZI WA MADIWANI



CHAMA cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA), kinatarajiwa kufanya mikutano mikubwa ya hadhara mkoani Arusha itakayohutubiwa na Katibu Mkuu wake, Dk. Willibrod Slaa, yakiwa ni maandalizi ya uchaguzi mdogo wa madiwani utakaofanyika Oktoba 28 mwaka huu katika kata 29.

Dk. Slaa atahutubia mkutano wa kwanza kesho mjini Arusha katika viwanja vya Ndarvoi Kata ya Daraja Mbili na kuzindua rasmi kampeni za udiwani, ukiwa ni mkakati wa kuinyakua kata hiyo iliyokuwa ikiongozwa na CCM.

Akizungumza na gazeti hili kwa njia ya simu jana, Mweyekiti wa CHADEMA Mkoa wa Arusha, Samson Mwigamba, alisema kuwa tayari maandalizi yote yamekamilika na kwamba wanataka kutumia uchaguzi huo kuidhihirishia CCM na wapambe wake kuwa kanda hiyo ni ngome ya CHADEMA.

Mwigamba alifafanua kuwa Jumapili, Dk. Slaa atahutubia mkutano mwingine katika kata ya Bangata jimboni Arumeru Magharibi, ambayo nayo ilikuwa ikiongozwa na diwani wa CCM aliyefariki.

“Tutafanya kampeni kwa kishindo kikubwa na kwa jinsi hali ilivyo hapa Arusha hakuna kata ambayo CHADEMA tutashindwa kuichukua. Na CCM katika kuogopa hili wameanza kutembeza fedha kununua shahada za kupigia kura kwa dau kubwa wakidhani watu wa hapa wanadanganyika,” alisema.

Hata hivyo, uchaguzi huo mdogo mjini humo, hautazihusisha kata nne ambazo madiwani wake walifukuzwa uanachama na CHADEMA na ile moja ya Sombetini ambayo aliyekuwa diwani wake kupitia CCM, Alphonce Mawazo, alihamia CHADEMA.

Madiwani hao waliofukuzwa na kata zao kwenye mabano ni Charles Mpanda (Karoleni), Estomi Mallah (Kimandolu), John Bayo (Elarai) na Ruben Ngowi (Themi).

“Kata hizi hazitafanya uchaguzi kwa sasa kwani utakumbuka baada ya madiwani hawa kufukuzwa walifungua kesi kupinga lakini wameshindwa na taarifa hizo zilikwenda Tume ya Uchaguzi wakati tarehe ya uchaguzi ikiwa imeshapangwa,” aliongeza Mwigamba.

Kuhusu mwenendo mzima wa uchaguzi, mwenyekiti huyo alisema wamejipanga vya kutosha, hivyo kuwa na matumaini makubwa ya kunyakua kata zote kutoka mikononi mwa CCM.

Alipoulizwa juu ya operesheni ya Chama cha Wananchi (CUF) maarufu kama Dira ya Mabadiliko (V4C) iliyofanyika hivi karibuni jijini humo imewaathiri kiasi gani, Mwigamba alitamba kuwa hawakuathirika kwa lolote kwa vile ilikufa kabla haijaanza.
 
“Niliwaambia CUF mapema kwamba ngome yao iko Pemba, hivyo V4C ilipaswa ianzie huko ndipo waisambaze huku Arusha lakini hawakufanya badala yake wameleta wafuasi kutoka Dar es Salaam, Tanga na Kilimanjaro ili kuvuta umati wa watu mkutanoni bila mafanikio,” alisema.

No comments:

Post a Comment