To Chat with me click here

Tuesday, October 23, 2012

RUSHWA ITAITUMBUKIZA CCM KWENYE SHIMO-JK


Rais  Jakaya Kikwete ameonya kwamba vitendo vya rushwa vinavyojitokeza katika chaguzi za ndani ya Chama Cha Mapinduzi (CCM) visipodhibitiwa  vitakitumbukiza chama hicho kwenye shimo.

Rais Kikwete alitoa angalizo hilo ikiwa ni siku moja tu, baada ya Mkutano Mkuu wa Umoja wa Wanawake wa CCM (UWT)  kumchagua Sophia Simba kuwa Mwenyekiti wake katika uchaguzi unaodaiwa kugubikwa na rushwa, vijembe na tambo.
Kikwete, amesema suala la kuuza na kununua kura lisiposhughulikiwa litakitumbukiza chama kwenye shimo. Kikwete aliyasema hayo juzi usiku alipokuwa akifunga Mkutano Mkuu Maalum wa uchaguzi wa UWT uliofanyika katika ukumbi wa Mwalimu Nyerere uliopo Chuo cha Mipango mjini hapa.
Rais Kikwete alisema kuwa wakati huu kuna mambo mengi ambayo baadhi yake yanasikitisha na kwamba hata kuyasema yanatia aibu.
“Kuna mambo mengi, mengine yanasikitisha hata kuyasema ni aibu, na wakati wote naendelea kukumbusha. Ndugu zangu haya tukiendelea nayo sura tunayoijenga kwa wananchi ya chama chetu… tunaona sisi tunapata, lakini athari yake kwa wananchi na ndani ya chama ni mbaya sana, tena sana, sina namna ya kutafuta maneno mazuri ya kulieleza hilo ya kununua na kuuza kura ,” alisema Rais Kikwete ambaye alionyesha kukerwa sana na jambo hilo na kuongeza:
“Nimeyasema haya ni lazima tufike mahali tutambue kuwa haya si mazuri na yanapohusisha mpaka wanawake, maana zamani nilidhani haya mambo ni ya wanaume tu, lakini sasa hadi wanawake ndio tena tumekwisha. Tunakoelekea sio kuzuri sana na kama hatutafanya jitihada ya makusudi kubadiliks, tupo hapa mtakuja kunieleza jinsi mtakavyoelekea kwenye shimo.”
NYUFA ZA UCHAGUZI
 
Alisema kazi ya timu iliyochaguliwa katika uchaguzi huo ni kuziba nyufa za mgawanyiko wa uchaguzi.
“Maana kuna watu wengine wanaondoka na mfundo, sina neno la kulielezea, lakini anaondoka na kitu amekifunga, ana hasira ndio mfundo. Ukomavu na ustahimilivu ni jambo linalohitajika sana,” alisema na kuongeza:
“Jambo hili lazima mtambue kuwa kugombea ni haki ya kila mwanachama, hakuna ambaye ana haki zaidi ya mwenzake, maadam ulikuwa kiongozi miaka mitano haki yako inaishia siku ile muda wako unapoisha baada ya hapo kila mwanachama anayo haki ya kugombea nafasi ya uongozi uliyokuwa unashikilia.”
Rais Kikwete alisema pia mwanachama anayo haki ya kumuunga mkono mtu yoyote ambaye anaona anafaa na kwamba kuna watu wanaweza kuchukiana kwa sababu ya mwanachama kugombea nafasi aliyokuwa anashikilia.
“Kwa nini kagombea nafasi yangu? Yako kivipi? Katiba inasema utakuwa kiongozi kwa muda wa miaka mitano, imeisha! Sasa unaomba upya, huyu Sophia ni Mwenyekiti mpya alikuwepo huwezi kumchukia mwanachama anayegombea nafasi unayoiita yako si yako,” alisema na kushangiliwa.
Alisema nafasi hiyo ni haki ya kila mwanachama na kuwataka kutowachukia wale ambao hawakuwaunga mkono katika uchaguzi na badala yake kuwaunga wagombea wengine.
“Mkiendekeza hilo hakutakuwa na demokrasia katika chama chetu, ukitoka hapo kwanini aligombea nafasi yangu, mkitoka hapa mnanuniana kwanini yule alimuunga mkono fulani, kama walikuwa wanataka wote wakuunge mkono wewe wasingewaruhusu wengine waje,” alisema na kushangiliwa na wajumbe wa mkutano huo.
Rais Kikwete alisema kumchukia ama kumnunia mtu ambaye ameamu kutumia haki yake ya kidemokrasia katika uchaguzi ni kuonyesha kiwango cha juu cha udhaifu.
Alisema pia kiongozi wa namna hiyo atakuwa hatoshi, hajiamini  na ataendesha chama kimakundi.
“Hawa wangu, hawa si wangu, hakuna mtu wa mtu binafsi hawa wote ni wa chama, lazima wote wapewe fursa ya kutumikia jumuiya yao kwa uwezo  wao, sifa yao isiwe hakuniunga mkono ama ameniunga mkono mtaiua  jumuiya hii,” alisema.
NAFASI ZA UONGOZI
Alitolea mfano wa siku moja alipokuwa katika kikao cha Halmashauri Kuu ya Taifa (Nec) kuwa wakati mwingine vineno vya kipuuuzi vilitoka. “Nikawaambia jamani baada ya kuchaguliwa kuwa Rais, mwaka 2005, nimeunda serikali akiwemo Mwandosya (Profesa Mark Mwandosya ambaye ni Waziri asiyekuwa na Wizara Maalum).
Profesa Mwandosya alikuwa miongoni mwa makada 11 waliomba kuwania urais ndani ya chama hicho katika uchaguzi mkuu uliofanyika mwaka 2005.
“Nimeunda serikali ambayo ina mawaziri ambao walikuwa wanawaunga mkono wagombea wenzangu katika uchaguzi huo, na wengine walikuwa wananifanyia mambo ya ovyo kweli, lakini yameshapita, sasa tuko katika hatua ya kujenga nchi yetu, nchi haijengwi na marafiki zangu tu,” alisema.
“Hiyo nchi mnaweza kuifikisha hata shimoni kwa sababu ya urafiki, nina mchanganyiko mle ndani, utakuta mle ndani kila mmoja katika wagombea wale 11 kila mmoja alikuwa na mtu wake,” aliongeza.
 Alisema baada ya kuweka watu mchanganyiko katika serikali yake, alijenga utulivu ndani ya chama, ingawa baadaye aligundua kuwa wanaogombana ni rafiki zake.
“Wanagombana wao wananipa kazi kubwa, jamani tunagombea nini mbona katika uchaguzi huo tulikuwa pamoja?” alihoji.
Alisema amelisisitiza hilo ili Simba na wenzake waepuke kulitenda na pia akilifanya wanachama wa umoja huo wasiseme atakapowachagua waliompinga katika uchaguzi huo.
Aliwataka kukusanya nguvu ili kuiwezesha jumuiya hiyo kujenga nguvu kwa ajili ya ushindi katika uchaguzi wa Serikali za Mitaa wa mwaka 2014 na Uchaguzi Mkuu wa mwaka 2015.
Aliwataka walioshinda kuanza kufanya kazi ya kuunganisha jumuiya hiyo na kuacha kuwabeza wale walioshindwa.
“Lakini sisemi hivyo kwamba watu wa ovyo nao tuwakusanye hapana, majitu ya ovyo, watoa rushwa, wezi, wenye muonekano  mbaya katika jamii achaneni nao hawatuongezei chochote, tunataka mtu ukimsimamisha mbele ya jamii, waseme yes (ndiyo) huyu ni mtu safi,”  alisema.
“Huyu anaweza kuwa kiongozi wa nchi, kiongozi wa  wanawake na si kiongozi ninayemtaka mie, uwe na mtu unayetaka wewe na mtu anayetakiwa na jamii.”
WANACHAMA WAPYA
Alisema wakiendelea na wanachama waanzilishi tu bila wapya jumuiya  itachosha na kwamba wakati alipopitia majina ya watu wanaogombea uongozi ndani ya chama hicho, aliona uwepo wa idadi ndogo ya wasomi walioomba nafasi za uongozi ndani ya jumuiya hiyo ikilinganisha na  Jumiiya ya Vijana wa chama hicho (UVCCM).
MALALAMIKO YA RUSHWA
Katika uchaguzi huo ambao Sophia Simba aliibuka kidedea kwa kupata kura 715, Anne Kilango Malecela 310 na Mayrose Majinge kura saba, ulidaiwa kugubikwa na rushwa.
Ilidaiwa kuwa wajumbe waligawiwa fedha katika nyumba za kulala wageni na kwenye vyoo vya ukumbi wa mikutano wa Chuo cha Mipango.
Mmoja wa wagombea anadaiwa kuwasafirisha wajumbe kutoka mikoa mbalimbali na kuwalipia gharama zote.
Malalamiko mengine kuhusu rushwa yametolewa na baadhi ya wagombea wa uenyekiti wa mikoa. Waliolalamika ni Clement mabina (Mwanza), John Guninita (Dar es Salaam), Thomas Ngawaiya (Kilimanjaro), Makongoro Nyerere (Mara) na William Kusila (Dodoma).

CHANZO: NIPASHE

No comments:

Post a Comment