To Chat with me click here

Monday, October 22, 2012

VIONGOZI WA UAMSHO MBARONI

WAKABILIWA NA KESI YA KUCHOCHEA VURUGU, KUFIKISHWA MAHAKAMANI LEO KUJIBU MASHITAKA
Sheikh Farid Hadi Ahmed
JESHI la Polisi visiwani Zanzibar, limewakamata viongozi wa Jumuiya ya Uamsho, akiwemo Sheikh Farid Hadi Ahmed (41), kutokana na kosa la kuchochea vurugu.

Taarifa za kukamatwa kwa viongozi hao, zilitolewa na kuthibitishwa na Kamishna wa Jeshi la Polisi visiwani humo, Mussa Alli Mussa.

Mbali na Sheikh Farid viongozi wengine waliokamatwa ni pamoja na Mwenyekiti wa jumuiya hiyo, Sheikh Mselem Alli Mselem (52) na Sheikh Azan Farid Hamad (48). Wengine ni Sheikh Hassan Bakari Suleiman (29), Ustadh Mussa Juma Issa (33) na Sheikh Suleiman Juma Suleiman.

Kamishna Mussa, alisema viongozi hao wanashikiliwa kwa kosa la kuchoche vurugu, ghasia na kuharibu miundombinu ya barabara. Baada ya viongozi hao kuhojiwa juzi na kuruhusiwa, lakini jeshi lake limeamua kuwakamata tena viongozi hao kutokana na uchunguzi wao kubaini viongozi hao walihusika na kuchochea vurugu visiwani humo.

Kamishina huyo alisema, viongozi hao wanatarajiwa kufikishwa mahakamani leo kujibu mashitaka yanayowakabili, huku akiwataka wananchi visiwani humo kuwa watulivu.

“Baada ya kufanya mahojiano na viongozi hawa kwa siku ya juzi na uchunguzi wetu wa kina, tumebaini viongozi hawa walihusika na kuchochea vurugu zilizotokea Zanzibar. “Katika kipindi chote cha mahojiano, tuliweza kutoa haki ya kuwasilikiza kwa kina viongozi hawa. “Lakini baada ya uchunguzi wetu wa kina tumebaini kuhusika kwa viongozi hawa na matukio ya uvunjifu wa amani hapa Zanzibar. “Jeshi la Polisi tumejipanga vizuri katika kulinda usalama wa raia na mali zao, hasa katika kipindi hiki ambacho Zanzibar imerejea katika hali ya amani.

“Hivyo tumejipanga vema na wale ambao watajaribu kuvunja amani, tutapambana nao kwa kutumia nguvu.  “Mara baada ya kufanya mahojiano nao viongozi hawa na kujiridhisha kwa kina kesho (leo) tutawafikisha mahakamani kwa hatua zaidi. “Jeshi la Polisi tupo imara wakati wote katika kulinda amani na usalama, hivyo ninatoa wito kwa wananchi kuwa watulivu,” alisema Kamishna Mussa.

Walioua askari watiwa nguvuni

Wakati huo huo jeshi hilo limewatia nguvuni watu sita kwa tuhuma za kuhusika na tukio la kumuua askari Polisi Koplo Saidi Abdrahamani Juma (41).

Koplo Saidi, aliyekuwa askari wa Kikosi cha Kutuliza Ghasia Ziwani Mjini Zanzibar, aliuawa kwa kukatwakatwa mapanga na watu wanaosadikiwa kuwa ni wafuasi wa Jumuiya ya Uamsho.

Kamishna Mussa Ali Mussa, alisema watu hao waliokamatwa ni Abdallah Mohamed Said, Joli Ghasul na Bakarin Juma Yussuf. Watuhumiwa wengine waliokamatwa mkoani Tanga ni Ally Salum Seif, Abubakari Haji Mbaruk na ndugu yake Mohamed Haji Mbaruk.

“Hawa wengine tumewakamata mkoani Tanga baada ya kuweka mitego yetu ya kiitelijensia kwa nchi nzima, hivi sasa tumeshawarushisha wapo hapa Zanzibar, tunaendelea na uchunguzi dhidi yao ambapo wakati wowote kutoka sasa tunaweza kuwafikisha mahakamani,” alisema Kamishna Mussa.

“Tuelewe kuwa aliyeuliwa ni askari Polisi, ni raia wa Tanzania na ni muumini wa dini, ni lazima tuhakikishe waliofanya unyama huu wanakamatwa na kufikishwa mahakamani kama sheria za nchi zinavyotuelekeza,” alisema.

“Watu hao walitorokea huko na tunaendelea kuwahoji…tunawashukuru wananchi kwa ushirikiano wao mkubwa uliotuwezesha kufanikisha ukamataji huo,tunavishukuru vikundi vya ulinzi shirikishi vilivyo katika Shehia mbalimbali, kwa kuimarisha ulinzi wa maeneo yao katika kipindi chote cha fujo na vurugu hizo,” alisema Kamishna Mussa.

Oktoba 16, mwaka huu fujo zilizuka visiwani humo baada ya kupotea katika mazingira ya kutatanisha kwa kiongozi wa jumuiya hiyo, Sheikh Farid Hadi Ahmed, hali iliyosababisha vurugu.

Sheikh Farid ambaye amekuwa mwiba mkali kwa Serikali ya Mapinduzi Zanzibar (SMZ), alionekana saa 2:15 usiku wa juzi katika eneo la Mazizini, nje kidogo ya mji wa Zanzibar.

Watu 51 walikamatwa na Jeshi la Polisi, kutokana na vurugu zilizotekea visiwani humo, baada ya kuripotiwa kupotea kwa kiongozi huyo.

No comments:

Post a Comment