To Chat with me click here

Tuesday, October 23, 2012

KIONGOZI WA UAMSHO ASHTAKIWA

ULINZI MKALI WATANDA, APELEKWA RUMANDE



KIONGOZI wa Jumuiya ya Uamsho na Mihadhara ya Kislamu, Sheikh Faridi Hadi Ahmed, na wenzake sita jana walipandishwa katika Mahakama ya Wilaya Manakwerekwe visiwani hapa, wakikabiliawa na tuhuma za kufanya uchochezi na kusababisha vurugu.

Mwendesha Mashtaka wa Serikali kutoka ofisi ya Mkurugenzi wa Mashtaka (DPP), Maulid Ame, aliwataja viongozi wengine kuwa ni Sheikh Mselem Ali Mselem (Kwamtipua), Sheikh Musa Juma Issa (Makadara) na Sheikh Azani Khalid Hamdani (Mfenesini).

Wengine ni Sheikh Suleiman Juma Suleiman (Makadara), Sheikh Khamis Ali Suleiman (Mwanakwerekwe) na Hasan Bakari Suleiman mkazi wa Tomondo.

Wote kwa pamoja walidaiwa kuwa Agosti 17, mwaka huu, majira ya saa 11 jioni huko kiwanja cha Magogoni Msumbiji katika Wilaya ya Magharibi Unguja wakiwa wahadhiri kutoka Jumuiya ya Uamsho na mihadhara ya Kiislamu walitoa matamko ya uchochezi.

Kwamba maneno hayo yaliashiria uvunjifu wa amani na kusababisha fujo na maafa mbalimbali na mtafaruku kwa Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar (SMZ).

Mwendesha mashtaka huyo alisema kitendo hicho kilikwenda kinyume na kifungu cha 45 (1) (a) (b) sheria na 6 ya mwaka 2004 sheria za Zanzibar.

Hata hivyo wakili wa washtakiwa hao, Abdalla Juma, alisema kuwa makosa ya wateja wake si miongoni mwa yale yanayopaswa kunyimwa dhamana, hivyo aliomba mahakama kuwapatia dhamana kwa masharti mepesi.

Alisema kuwa kitendo cha kutaka barua ya sheha na wadhamini ambao ni watumishi wa serikali kwa ajili ya dhamana ni kuwakwamisha wateja wake kwani watu hao ni vigumu kuwapata.

Hata hivyo, mwendesha mashtaka wa serikali hakuwa na pingamizi na ombi la dhamana hiyo na kusema anaiachia mahakama itoe uamuzi. Naye hakimu anayesikiliza kesi hiyo, Ame Msaraka Pinja, alisema wa kuwa dhamana ni haki yao haitakuwa busara kwa mahakama yake kutoa uamuzi wa haraka wala kuchelewesha dhamana za washtakiwa hao.

Aliiahirisha kesi hiyo hadi Oktoba 25 mwaka huu ambapo itakuja kusikizwa uamuzi wa dhamana zao, na hivyo watuhumiwa wote walirudishwa rumande.
Hata hivyo, wakati wote kesi hiyo ikiendelea, ulinzi mkali wa polisi ulitanda kuzunguka mahakama hiyo, huku watu wakizuiwa kuingia ndani.

Sheikh Faridi na wenzake walifikishwa mahakamani hapo majira ya saa 5:00 asubuhi chini ya ulinzi mkali wa polisi wenye magari saba aina ya Landrover.

No comments:

Post a Comment