To Chat with me click here

Tuesday, October 16, 2012

RIPOTI YA NGWILIZI YAIUMBUA SERIKALI

YAWASAFISHA WABUNGE WALIOTUHUMIWA KWA RUSHWA. WAZIRI MUHONGO, MASWI SASA WAKUTWA NA HATIA. LUKUVI ADAIWA KUHAHA KUIZIMA ILI KUINUSURU SERIKALI 

Mbunge wa Mlalo, Mhe. Brigedia Jenerali Hassani Ngwilizi
RIPOTI ya Kamati ndogo ya Bunge ya Haki, Maadili na Madaraka ya Bunge, imemuweka pabaya Waziri wa Nishati na Madini, Profesa Sospeter Muhongo na Katibu Mkuu wake, Eliakim Maswi.

Taarifa za ndani zinaeleza kuwa ripoti hiyo inadaiwa kuwakaanga viongozi hao, huku ikiwasafisha wabunge waliokuwa wakituhumiwa kwa rushwa.

Chanzo chetu cha habari kimeweka wazi kuwa umeibuka mvutano baina ya Serikali, ofisi ya Bunge na Kamati ya Nishati na Madini kuhusiana na ripoti hiyo.

Kamati hiyo iliyokuwa chini ya Mbunge wa Mlalo, Brigedia Jenerali Hassan Ngwilizi (CCM), imekamilisha kazi yake ya uchunguzi na tayari ripoti hiyo imekabidhiwa kwa Spika wa Bunge, Anne Makinda.

Kamati hiyo ilikuwa ikichunguza madai ya baadhi ya wabunge kuhongwa ili wakwamishe bajeti ya Wizara ya Nishati na Madini, jambo lililozua mjadala mkubwa.

Ripoti hiyo ilitarajiwa kusomwa wakati wa kikao cha Bunge kitakachoanza Oktoba 29, mwaka huu, lakini Serikali inadaiwa kuhaha kutaka kuizima ripoti hiyo isisomwe hadharani.

Baada ya uchunguzi uliofanywa na kamati hiyo, imebainika kuwa wabunge hao hawakuhusika na rushwa na badala yake ikawaweka hatiani Profesa Muhongo na katibu mkuu wake.

Pamoja na mambo mengine, ripoti hiyo inadaiwa kutoa mapendekezo ambayo yakitekelezwa kama yalivyo, itakuwa ni sawa na kuivua nguo Serikali.

Ripoti hiyo inamtaka Spika Anne Makinda kumpa dakika tano Waziri Muhongo ili aweze kuliomba radhi Bunge kutokana na kauli za uwongo ambazo zimeonekana kuwadhalilisha wabunge.

Mbali na hilo, ripoti hiyo pia imependekeza Katibu Mkuu wa wizara hiyo, Eliakim Maswi achukuliwe hatua za kinidhamu kwa kosa la kumpotosha waziri wake.

Mvutano baina ya Serikali, Bunge na Kamati ya Nishati na Madini umetokana na wajumbe wa kamati kubaini mkakati wa kutaka kuizima ripoti hiyo.

Chanzo hicho kilieleza kuwa mkakati huo ulianza kufahamika, kutokana na kupishana kwa taarifa kutoka Ofisi ya Bunge kwenda kwa wajumbe wa Kamati ya Bunge ya Nishati na Madini.

Inadaiwa kuwa Mwenyekiti wa kamati hiyo, Selemani Zedi, alipata taarifa kutoka ofisi ya Katibu wa Bunge Alhamisi wiki iliyopita, ikimuarifu kuwa anatakiwa kufika Dar es Salaam Jumatatu (jana) ili kupanga ratiba ya mkutano ujao wa Bunge.

“Sasa kilichotokea ni kwamba, wakati Zedi akijiandaa na ratiba hiyo, siku ya Jumamosi akapokea taarifa kutoka ofisi hiyo hiyo ikimpa taarifa nyingine.

“Taarifa ya pili ilimweleza kuwa kikao hicho kimeahirishwa na badala yake anatakiwa kuwajulisha wajumbe wa kamati yake wajichagulie kamati nyingine ili waweze kuingizwa humo,” kilisema chanzo hicho.

Chanzo hicho kilisema kuwa taarifa hiyo ya pili ilichangiwa na hoja zilizotolewa na Waziri wa Nchi Ofisi ya Waziri Mkuu (Bunge na Uratibu) Wiliam Lukuvi, ambaye alipinga ripoti hiyo kusomwa hadharani.

“Inavyoonekana Spika amekubaliana na hoja za Lukuvi za kwamba ripoti hiyo ni mbaya kwa Serikali na iwapo spika ataruhusu isomwe hadharani itaivunjia heshima.

“Ripoti imependekeza kuwa spika atoe dakika tano kwa Waziri Muhongo kuliomba radhi Bunge kwa kupotosha umma na kuwadhalilisha wabunge kwamba wamehongwa.

“Pili, ripoti imemtia hatiani katibu mkuu wa wizara kwa kutaka achukuliwe hatua za kinidhamu kulingana na taratibu za utumishi wa umma kwa kosa la kumpotosha ‘bosi’ wake.

“Wao walitaka ripoti hiyo isisomwe ili kuilinda Serikali. Utakumbuka Kamati ya Nishati na Madini ilivunjwa kutokana na tuhuma hizo za rushwa, sasa wakataka wajumbe hao wajichagulie kamati nyingine za kwenda.

“Wajumbe wote wa kamati hii wamekataa na walituma ujumbe kwenda Ofisi ya Bunge, kwamba suala hilo hawaliafiki na badala yake wanataka ripoti hiyo isomwe hadharani ili iwasafishe kwani walichafuliwa.

“Wabunge wamekataa kujichagulia kamati, kwani wao hawana mamlaka ya kujichagulia kamati, mwenye mamlaka ya kufanya hivyo ni spika, sasa iweje leo waambiwe wajichagulie kamati?” kilihoji chanzo hicho.

Hivi karibuni, Naibu Spika wa Bunge, Jobu Ndugai, alinukuliwa na vyombo vya habari akisema suala la ripoti hiyo kusomwa bungeni au vinginevyo inategemea uamuzi wa Kamati ya Uongozi ya Bunge.

Ndugai alisema baada ya kamati kuwasilisha ripoti kwa Spika, Kamati ya Uongozi ya Bunge itakaa kujadili na kama itaona kuna umuhimu ripoti hiyo itaingizwa katika ratiba ya vikao vya bunge ijadiliwe.

Wakati wa mkutano wa bunge la bajeti ya mwaka 2012/13, baadhi ya wabunge walidai kuwa kuna wenzao wamehongwa na kampuni za mafuta ili kukwamisha bajeti ya Wizara ya Nishati na Madini.

Pia katika mkutano huo ilidaiwa kuwa hatua hiyo ililenga kushinikiza Waziri wa Nishati na Madini, Prof. Sospeter Muhongo na Katibu Mkuu, Eliakim Maswi, wang’olewe katika nafasi zao kwa kukiuka Sheria ya Manunuzi wa Umma.

No comments:

Post a Comment