To Chat with me click here

Tuesday, October 9, 2012

CCM YAANGUKA TENA

SASA UCHAGUZI MDOGO WANUKIA SUMBAWANGA

Aeshi Hilaly Khalfan
KWA mara nyingine tena, Chama cha Mapinduzi (CCM), kimegonga mwamba baada ya Mahakama ya Rufaa Tanzania, kuitupilia mbali rufaa ya aliyekuwa Mbunge wake wa Sumbawanga Mjini, Aeshi Hilaly, aliyevuliwa ubunge na Mahakama Kuu Kanda ya Sumbawanga Aprili 30, mwaka huu.

Uamuzi wa kuitupilia mbali rufaa hiyo, umetolewa na jopo la majaji watatu, Januari Msoffe, Edward Rutakangwa na Engela Kileo, baada ya kubaini kasoro za kisheria.

Hilaly alivuliwa ubunge na aliyekuwa Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu Kanda ya Sumbawanga, Bethuel Mmila, kutokana na kesi iliyofunguliwa na aliyekuwa mgombea ubunge kupitia CHADEMA, Nobert Yamsebo.

Hata hivyo, Mei 28 mwaka huu, Hilaly alikata rufaa namba 55 ya mwaka 2012, dhidi ya Yamsebo, Mwanasheria Mkuu wa Serikali (AG), Justus Kalama na Vitus Kapufi, akipinga uamuzi wa Mahakama Kuu.

Rufaa hiyo imebainika kuwa na dosari kadhaa ambazo zimeishawishi Mahakama ya Rufaa Tanzania chini ya jopo la majaji hao kuitupilia mbali jana katika uamuzi uliotolewa jijini Dar es Salaam.

Dosari hiyo ni kutokuwepo kwa mwenendo wa maombi ya mlalamikaji katika kesi ya msingi ya kuomba mahakama impangie kiwango cha fedha ambacho alipaswa kulipa kama amana ya kufungua kesi hiyo kwa mujibu wa Kifungu cha 111 (3) cha Sheria ya Uchaguzi ya mwaka 2010.

Katika uamuzi wake uliosomwa na Naibu Msajili wa Mahakama ya Rufani, Zahra Maruma, mahakama hiyo ilirejea kifungu cha 111 (3) cha Sheria hiyo ya Uchaguzi.

Kwa mujibu wa kifungu hicho, Mahakama ilisema kwamba mtu anayefungua kesi ya uchaguzi, ni lazima awasilishe maombi ili mahakama impangie kiwango cha amana anachopaswa kulipa ndani ya siku 14 tangu kufungua kesi na kwamba ndani ya siku 14 nyingine tangu siku ya maombi hayo, mahakama hiyo iwe imeshapanga kiwango hicho.

Majaji hao waliongeza kuwa, ni muhimu kwa sababu kuu mbili, moja ni kuipa nafasi mahakama kuona kama maombi yaliwasilishwa ndani ya muda baada ya kesi kufunguliwa na pili kuona kama maombi hayo yaliamuliwa ndani ya muda tangu kuwasilishwa.

Kwamba kwa mujibu wa Kanuni ya 96 (1) na (3) za Kanuni za Mahakama ya Rufani, si jukumu la upande katika kesi kuamua kuwa nyaraka fulani ni muhimu au si muhimu katika rufaa, kama wakili wa Hilaly, Rweyongeza alivyodai.

Mbali ya kanuni hiyo, Mahakama hiyo pia ilirejea katika uamuzi wake katika rufaa namba 8 ya mwaka 2008, Fedha Fund Limited na wenzake wawili, dhdi ya George T.Varghese, pamoja na tafsiri ya Kanuni ya 85 (3) ya Kanuni za Mahakama ya Rufani ya Kenya za mwaka 1979.

"Kutokana na sababu hizo tulizokwisha kuzieleza hapo juu, tanarudia kusema kwamba kumbukumbu zinazohusiana na mwenendo wa maombi ya kupangiwa kiwango cha kulipa kama amana ni nyaraka muhimu katika rufaa.

Kutokuwepo kwa nyaraka hizo, rufaa haina nguvu chini ya Kanuni ya 96 (1) (k) ya Kanuni za Mahakama ya Rufani, hivyo rufaa inatupiliwa mbali," lilisema jopo hilo.

Hata hivyo, mahakama hiyo ilisema kuwa haiwezi kuamua upande wa warufani ulipe gharama za rufaa hiyo kwa kuwa kasoro zilizosababisha kutupiliwa mbali kwa rufaa hiyo ziliibuliwa na mahakama yenyewe.

Julai 3, 2012, AG na Kalama, nao walikata rufaa namba 65 ya mwaka 2012 dhidi ya Yamsebo wakipinga uamuzi wa Mahakama Kuu Kanda ya Sumbawanga.

Kutokana na rufaa hizo dhidi yake, Yamsebo kupitia kwa Wakili wake Victor Mkumbe, aliweka pingamizi la awali (PO) pamoja na mambo mengine akidai kuwa Hilaly hakuwa amelipia ada ya kufungua rufaa hiyo ya Sh 2000.

Hata hivyo, siku ambayo Mahakama ya Rufani ilipanga kusikiliza rufaa hiyo, iliamua kuziunganisha rufaa hizo mbili, ambapo Hilaly aliunganishwa na AG pamoja na Kalama wakawa waomba rufaa dhidi ya Yamsebo.

Kabla ya kuanza kusikiliza pingamizi la Yamsebo dhidi ya rufaa ya Hilaly, mahakama hiyo ilibaini kutokuwepo kwa mwenendo huo wa maombi ya Yamsebo kupangiwa gharama za kufungulia kesi hiyo ya msingi.

Kutokana na kasoro hiyo, mahakama ilihoji na kutaka maoni ya mawakili wa pande zote kuhusiana na kasoro hizo.

Wakili wa Serikali Mwandamizi, Mwema Punzi alijibu kuwa wao walimwandikia barua Msajili wa Mahakama ya Rufani Kanda ya Sumbawanga kumuomba mwenendo wa kesi hiyo pamoja na vielelezo vingine na kwamba walipopewa, mwenendo wa maombi ya gharama za kesi haukuwemo.

Wakili wa Yamsebo, Mkumbe, alidai kuwa kutokana na kutokuwepo kwa mwenendo huo, kunaifanya rufaa hiyo iwe batili, na akaiomba mahkama hiyo iitupilie mbali.

Hata hivyo Wakili wa Hilaly, Richard Rweyongeza, alidai kuwa kukosekana kwa mwenendo huo hakuwezi kuifanya rufaa hiyo iwe ni batili, badala yake aliiomba mahakama hiyo itumie mamlaka yake chini ya Kanuni ya 2 ya Kanuni za Mahakama ya Rufani, ili iweze kuendelea.

Wakili Rweyongeza aliongeza kwamba hata ikibainika kuwa hizo gharama za kufunulia kesi hazikulipwa, anayeathirika ni mjibu rufaa, hoja ambayo iliungwa mkono na Wakili wa Serikali, Punzi.

Katika kesi hiyo ya msingi namba 01 ya mwaka 2010, Yamsebo alikuwa akipinga ushindi wa Hilaly, akidai kuwa kulikuwa na ukiukwaji wa Katiba na Sheria ya Uchaguzi na hivyo kusababisha uchaguzi huo kutofanyika kwa haki na uhuru.

Pia, alikuwa akimtuhumu Hilaly na wafuasi wake kutoa rushwa kwa wapiga kura mbalimbali ili wamchague.
Tuhuma nyingine alikuwa akizieleka kwa Msimamizi wa Uchaguzi kuwa alibadilisha baadhi ya vituo vya kupigia kura kupelekwa mbali zaidi kati ya kilomita tano hadi nane, jambo ambalo ilichangia kuathiri matokeo ya uchaguzi huo.

Katika uamuzi wake, Mahakama Kuu ilikubaliana na baadhi ya hoja zilizotolewa na mlalamikaji na hatimaye kutengua ushindi wa Hilaly.
Akisoma hukumu hiyo, Jaji Mfawidhi Betwell Mmila, alisema kuwa baada ya kupitia hoja zote, anashawishika kusema kuwa uchaguzi katika jimbo hilo ulikuwa si wa haki na huru.

Jaji Mmila alieleza kuridhika kuwa kulikwepo na mazingira ya rushwa na kutokuwapo kwa mazingira huru katika kampeni kwa baadhi ya maeneo.
Katika uchaguzi huo, Hilaly alitangazwa kuwa mshindi kwa kupata kura 17,328, huku Yamsebo akipata kura 17,132.

Kwa uamuzi huo, Tume ya Taifa ya Uchaguzi (NEC), itapaswa kuitisha upya uchaguzi ndani ya siku 90 ikiwa Hilaly hatakata tena rufaa kupinga uamuzi huo wa jipo la majaji hao.

No comments:

Post a Comment