To Chat with me click here

Tuesday, August 21, 2012

MAHAKAMA KUAMUA UBUNGE IGUNGA LEO

Kushoto mwenye Skafu ni Dr. Peter Kafumu mbunge wa Igunga

MAHAKAMA Kuu Kanda ya Tabora, leo inatarajiwa kutoa hukumu katika kesi ya kupinga matokeo yaliyompatia ushindi Mbunge wa Igunga, Dk. Peter Kafumu (CCM) kwenye uchaguzi mdogo uliofanyika Oktoba mwaka jana.

Shauri hilo lilifunguliwa na aliyekuwa mgombea ubunge kwa tiketi ya Chama cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA), Joseph Kashindye dhidi ya Dk. Kafumu, Mwanasheria Mkuu wa Serikali na msimamizi wa uchaguzi huo, Protace Mgayane.

Shauri hilo lilianza kusikilizwa rasmi Machi 26 mwaka huu chini ya Jaji Mary Nsimbo Shangali.

Akizungumza na Tanzania Daima kwa njia ya simu, Hakimu Mkazi Mfawidhi wa Wilaya, Silvester Kainda, alisema kuwa Mahakama Kuu Kanda ya Tabora ilipanga hukumu hiyo isomwe Agosti 20 mwaka huu, lakini kutokana na tarehe hiyo kuangukia Sikukuu ya Idd, hukumu hiyo itasomwa leo.

Wakili wa mlalamikaji, Profesa Abdallah Safari, alizungumza na Tanzania Daima kwa njia ya simu jana na kusema kuwa zaidi ya malalamiko 13 waliyawasilisha katika mahakama hiyo.

Alisema kuwa kulingana na malalamiko hayo, wanaiachia mahakama itatoa uamuzi wake kwa vile kila kitu wamekiwasilisha na kwamba ushahidi wote umesikilizwa.

Dk. Kafumu anatetewa na mawakili wawili, Anthony Kanyama na Kayaga Kamaliza.

Mojawapo ya malalamiko katika kesi hiyo ni pamoja na vitisho vilivyotolewa na viongozi wa serikali, ahadi ya ujenzi wa daraja la Mbuntu pamoja na kugawa mahindi.

No comments:

Post a Comment