To Chat with me click here

Tuesday, August 21, 2012

WAZIRI MKUU ETHIOPIA AFARIKI DUNIA



Sasa ni sahihi kwamba Zenawi hayupo tena duniani. Televisheni ya taifa ya Ethiopia imetangaza mapema leo kwamba kiongozi huyo aliyekuwa na nguvu sana nchini humo, amefariki dunia mjini Brussels, Ubelgiji, alikokuwa akitibiwa. Televisheni hiyo imesema Zenawi amefariki dunia wakati akiwa anapata afuweni kutokana na maambukizi ya ghafla. 

Tangazo la televisheni hilo limesema na hapa ninanukuu: "Waziri Mkuu Zenawi amefariki ghafla usiku wa jana. Meles alikuwa akipata afuweni katika hospitali moja ughaibuni kwa miezi miwili, lakini alifariki kutokana na maambukizi ya ghafla saa 5 na dakika 40." Mwisho wa kunukuu.

Uvumi kwamba kiongozi huyo wa zamani wa vita vya msituni alikuwa akiumwa sana, ulianza kusambaa tangu aliposhindwa kuhudhuria mkutano wa kilele wa Umoja wa Afrika mjini Addis Ababa mwezi uliopita. Tangu hapo wasiwasi ulikuwa umezuka juu ya nani hasa anaiongoza nchi hiyo, baada ya Zenawi kuchukuwa likizo ya kutokuwapo kazini. 

Serikali ilikanusha ugonjwa wa Zenawi
Siku ya Alhamis, msemaji wa serikali, Bereket Semon, alirejelea kauli yake ya mara kwa mara akikanusha kuwa Zenawi alikuwa mgonjwa sana. Serikali ilikuwa imesema kuwa Zenawi alilazimika kuchukua likizo kwa ushauri wa daktari.

Kwa ujumla, ni shida kujuwa hasa ugonjwa uliomaliza maisha ya kiongozi huyo ambaye amekuwa madarakani tangu kumpindua Megistu Haile Mariam hapo mwaka 1991, lakini inaaminika kwamba alikuwa akisumbuliwa na uvimbe kwenye ubongo. 

Zenawi atakumbukwa kwa sera yake ya kiutawala ambayo ilijuilikana kama shirikisho la makabila, akitoa mamlaka fulani mwa mamlaka za mikoa zenye misingi ya kikabila, lakini akisalia na nguvu kubwa kwenye serikali chini ya chama tawala. Nafasi ya uraisi inachukuliwa kama heshima tu, na Zenawi ndiye hasa aliyekuwa na nguvu za kisiasa. 

Naibu Waziri Mkuu Hailemariam achukua madaraka
Kwa mujibu wa katiba ya Ethiopia, naibu waziri mkuu ndiye anakuwa na wajibu wa kukaimu nafasi ya uwaziri mkuu, ikiwa waziri mkuu hayupo. Hata hivyo, sheria haisemi wazi na mahsusi ikiwa naibu huya wa waziri mkuu anachukuwa pia majukumu yote ya waziri mkuu.

Kwa kifo hiki cha Zenawi, kitu cha mwanzo ambacho kinaweza kushuhudiwa haraka nchini Ethiopia, wanasema wachambuzi, ni ombwe la kiuongozi, ikihofiwa kwamba hakuna yeyote katika watu wake wa karibu aliyetayarishwa vyema kujaa kwenye kiti cha uwaziri mkuu.

Baadhi ya wanadiplomasia wamesema kwamba hawana hakika ni nguvu kiasi ambazo Naibu Waziri Mkuu, Hailemariam Desalegn, anazo hivi sasa. Hailemariam alikuwa nchini China hadi hivi karibuni kabisa katika mkutano wa kilele na China. Taarifa za kibalozi na wachambuzi zinaonesha kuwa bado hakujawa na vita vya kugombea madaraka ndani ya chama tawala hadi sasa. 

Source: DW

No comments:

Post a Comment