To Chat with me click here

Friday, August 31, 2012

CCM YAFIKA PABAYA


DK. KIGWANGALA, BASHE WATISHIANA BASTOLA NZEGA

KATIKA kile kinachoonekana kama vita ya urais wa mwaka 2015, makundi yanayokinzana ndani ya Chama Cha Mapinduzi (CCM), yamedaiwa kuanza mkakati wa kujiimarisha kwa kutumia uchaguzi wa ndani unaoendelea sasa.

Hatua hiyo vile vile inaelezwa kuwa ni mwendelezo wa visasi vya Uchaguzi Mkuu uliopita katika baadhi ya maeneo, ambapo wagombea wanaokubalika waliachwa na kuchukuliwa wengine.

Mathalani katika Jimbo la Nzega, mkoani Tabora, visasi hivyo vimedumu baina ya Mbunge wa sasa, Dk. Hamis Kigwangala na kada aliyeenguliwa na Halmashauri Kuu ya Taifa, Hussein Bashe, akidaiwa si raia wa Tanzania.

Wawili hawa juzi wanadaiwa kutishiana bastola katika ofisi ya CCM wilayani humo wakati wakirejesha fomu za kuomba kuwania nafasi mbalimbali.

Taarifa kutoka vyanzo vyetu vya ndani ya chama hicho, zinaeleza kuwa miongoni mwa vigogo wanaotajwa kuutaka urais, makundi ya Waziri Mkuu wa zamani, Edward Lowassa na lile la Waziri wa Mambo ya Nje, Bernard Membe, ndiyo yanamsuguano mkali.

Wakati uchaguzi wa ndani wa CCM ukizidi kupamba moto, makundi hayo yanadaiwa kuwa kila moja linahaha kuhakikisha wale wanaoliunga mkono wanaibuka kidedea katika nafasi za ujumbe wa Halmashauri Kuu, Mkutano Mkuu na jumuiya za Wanawake, Wazazi na Vijana kuanzia ngazi ya wilaya hadi taifa.

Tanzania Daima limedokezwa kuwa katika kuweka mambo sawa, mmoja wa vigogo hao amebaini kutoungwa mkono na wenyeviti wanaomaliza muda wao katika mikoa ya Shinyanga, Mwanza, Dar es Salaam na Arusha, hivyo amesuka mkakati ili wasichaguliwe tena.

“Mkakati huu mchafu na hatari kwa ustawi wa demokrasia unatumia mamilioni ya fedha, maarufu kama ‘mamilioni ya Gadaffi’ na unaratibiwa na mmoja wa vigogo anayetajwa kuwa na lengo la kuwania urais mwaka 2015 kupitia CCM,” kilisema chanzo chetu.

Mabilioni hayo ya fedha yanadaiwa kuanza kumwagwa katika mikoa husika ikiwa ni lengo la kuhakikisha wenyeviti hao, Clement Mabina (Mwanza), Hamis Mgeja (Shinyanga), John Guninita (Dar es Salaam) na Ole Nangole wa Arusha hawarudi tena katika nafasi zao.

Baadhi ya makada wa CCM waliozungumza na gazeti hili, wamewaomba wenyeviti wastaafu wa chama hicho, Ali Hassan Mwinyi na Benjamin Mkapa kuingilia kati na kumsadia Rais Jakaya Kikwete kudhibiti matumizi ya fedha katika uchaguzi.

“Ili kuinusuru CCM katika anguko la kihistoria, tunawaomba sana Mwinyi na Mkapa waingilie kati kuhakikisha wanadhibiti kabisa matumizi ya fedha katika chaguzi zote za ndani,” alisema kada mmoja.

Chanzo chetu kimebaini kuwa kundi hilo limeanza kujipenyeza mikoani kuwachafua viongozi wa CCM wasiofungamana nao, hivyo kuandaa safu yao mpya.

Kigwangala vs Bashe
Kuhusu wawili hawa wanaowania ujumbe wa NEC Wilaya ya Nzega, taarifa zinasema kuwa tukio hilo la aibu lilitokea katika ofisi za CCM saa 09:30 alasiri baada ya Dk. Kigwangala kumwambia Katibu wa wa chama wa Wilaya, Kajoro Vyohoroka, asiipokee fomu ya Bashe kwani alikuwa amechelewa kuijaza na kuirejesha.

Tanzania Daima lilitonywa kuwa baada ya Dk. Kigwangala kumwambia katibu maneno hayo, Bashe akatoa lugha ya matusi kwa mbunge huyo.
“Kufuatia matusi hayo, Dk. Kigwangala alinyanyuka ghafla na kutaka kumpiga Bashe huku akimtishia kumtandika bastola...lakini baadhi ya wanachama wakawaamulia,” kilisema chanzo chetu.

Katibu wa CCM wa Wilaya ya Nzega, Vyohoroka, alikiri kutokea kwa tukio hilo ofisini kwake juzi na kwamba awali Dk. Kigwangala alikuwa akijaza fomu hiyo ofisini hapo na Bashe alikuwa ofisini kwa Mwenyekiti, Francis Shija.

Alifafanua kuwa Bashe alirejesha fomu saa 09:50 na Dk. Kigwangala naye alirejesha saa 09:48 lakini kwa mshangao mbunge huyo alitamka kuwa fomu ya Bashe imechelewa hivyo isipokewe.

Alisema kuwa baada ya hapo ndipo maneno makali yalipoanza hadi kufikia vitisho vya silaha.

Bashe alizungumza na gazeti hili akisema kuwa Dk. Kigwangala alimtishia kwa bastola akidai fomu yake isipokewe kwani muda wa kurejesha ulikuwa umekwisha.
“Si kweli kuwa muda ulikuwa umeisha, bali huyu ndugu yangu ana visa na chuki dhidi yangu, ni kweli alichomoa bastola yake lakini wanachama walituamua,” alisema Bashe.

Naye Dk. Kigwangala alikanusha akisema hakuna kitu cha namna hiyo, bali Bashe ni mzushi anayetaka kuyakuza mambo hayo.

“Si kweli na hamna kitu cha namna hiyo…Bashe anataka kuyakuza tu, ni kweli katibu amembeba muda wa kurejesha fomu ulikuwa umekwisha,” alisisitiza.

Kamanda wa Polisi wa Mkoa wa Tabora, Anthony Rutta, aliliambia gazeti hili kuwa taarifa za tukio hilo anazo lakini atafuatilia kujua chanzo.

Arusha waenguana
Mizengwe ya uchaguzi wa ndani ya CCM imeanza mkoani Arusha ambapo Halmashauri Kuu (NEC) ya  mkoa huo, imepinga uteuzi wa wagombea wa nafasi za uongozi wa jumuiya katika wilaya tatu.

Wilaya hizo ni pamoja na Monduli, kwa madai kuwa waliopitishwa ni watiifu wa kundi fulani la kisiasa ndani ya chama mkoa.

Akizungumzia uamuzi huo, Katibu wa CCM Mkoa wa Arusha, Mary Chatanda, alisema kwa Monduli NEC imeukataa uteuzi wa wagombea wa Jumuiya ya Vijana (UVCCM).

Alisema Wilaya ya Longido na Karatu, NEC imeukataa uteuzi wa wagombea wa nafasi za Jumuiya ya Wazazi kutokana na sababu za mgawanyiko wa makundi.

Kufuatia kasoro hizo, kikao hicho kimeagiza vikao husika vya uteuzi katika wilaya hizo kupitia upya na kuzirekebisha ndani ya wiki moja na kisha kukabidhi mapendekezo hayo kwa kamati ya siasa ya mkoa.

Chatanda aliongeza kuwa kikao hicho pia kilipitisha majina ya wagombea watano wa nafasi ya uenyekiti wa CCM Mkoa wa Arusha, ambao ni Dk. Salash Toure, Hamis Shaaban, Onesmo Metili, Adam Chora na anayetetea nafasi yake, Onesmo Nangole.

Dodoma watishana
Mkoani Dodoma, wagombea wameanza kutishia kuburuzana katika kamati za nidhamu kutokana na baadhi yao kudaiwa kukiuka taratibu za uchaguzi.

Mbunge wa Afrika Mashariki, Adam Kimbisa, ambaye pia ni mgombea uenyekiti wa mkoa, alisema kuwa ikithibitika kwamba wajumbe wawili wa Kamati ya Siasa ya mkoa, walimsindikiza mwenyekiti anayemaliza muda wake, William Kusila, kuchukua fomu, atawashtaki katika vikao vya juu.

Akizungumza na Tanzania Daima kwa njia ya simu jana, Kimbisa alisema kitendo cha  kuonesha kumuunga mkono mmoja wa wagombea wakati wao ni watoa maamuzi katika kikao kinachowachuja, ni kumbeba.

Kauli hiyo inakuja siku moja baada ya Katibu Mwenezi wa chama hicho, mkoani hapa, Donald Mejetii, kusema kuwa wajumbe hao wamevunja kanuni na taratibu za uchaguzi kwa makusudi kwa kuwasindikiza wagombea kuchukua fomu.

Naye Mbunge wa Chilonwa, Ezekiah Chibulunje, alijitetea kuwa hakumsindikiza Kusila kama kiongozi bali kama ndugu yake.

Katibu wa CCM wa Mkoa wa Dodoma , Albert Mgumba, alipoulizwa juu ya sakata hilo, alisema halina umuhimu wowote kwani ni la kawaida. 

Diallo amvaa Mabina
Katika Mkoa wa Mwanza, jumla ya wanachama 53 walijitokeza kuwania nafasi mbalimbali, huku mchuano mkali kwenye nafasi ya uenyekiti ukiwa baina ya mwenyekiti anayemaliza muda wake, Clement Mabina na mbunge wa zamani wa Ilemela, Anthony Diallo.

Katibu wa CCM mkoani hapa, Joyce Masunga, alisema kuwa nafasi ya uenyekiti wa mkoa wameomba wanachama 23 waliochukua na kurejesha fomu hadi siku ya mwisho.

Aliwataja baadhi ya wanachama hao kuwa ni Mabina, Diallo, Evanus Laurian, Theodora Ihuya, Barnabas Mathayo, Alfred Wambura na Zebedayo Athumani.

Tanzania Daima

No comments:

Post a Comment