To Chat with me click here

Tuesday, August 14, 2012

DK. ULIMBOKA AFICHWA


KATIKA kile kinachoonekana kama hofu ya kuuawa, Mwenyekiti wa Jumuiya ya Madaktari Dk. Steven Ulimboka, amefichwa kusikojulikana ikiwa ni siku moja baada ya kurejea kutoka nchini Afrika Kusini alikopelekwa kwa matibabu.

Kufichwa kwa Dk. Ulimboka kunadaiwa ni sababu za kiusalama ili kuwakwepa wabaya wake waliodaiwa kumteka na kumpiga, ambao inaelezwa kuwa wamekuwa wakihaha kutaka kukatisha uhai wake akiwa hospitali nchini Afrika Kusini bila mafanikio.

Dk. Ulimboka aliyefikia nyumbani kwa baba yake, mzee Steven Mwaitenda eneo la Ubungo Kibangu jijini Dar es Salaam baada ya kurejea nchini juzi alasiri, amefichwa kusikojulikana huku baba yake mzazi akieleza kuwa wanajiandaa kutoa tamko la familia.

“Kwa sasa Dk. hayupo hapa nyumbani… siwezi kusema alipo wala kutoa tamko langu ila muda ukifika tunamwandaa msemaji wa familia, vyombo vya habari mtajulishwa. Ninawapenda sana wanangu, lakini katika hili naomba tusubiri,” alisema baba wa Dk. Ulimboka aliyekutwa chini ya mti nje ya nyumba yake pembeni ya banda la kuku wachache wa kienyeji jana.

Kabla ya Tanzania Daima kuanza mazungumzo na baba huyo, ambaye awali alikuwa tayari kuzungumza, dada wawili wa Dk. Ulimboka waliingilia kati wakidai mzee huyo si msemaji wa familia.

Mmoja wa dada zake Dk. Ulimboka, aliyejitambulisha kwa jina moja la Hidaya, aliwataka waandishi wa gazeti hili kuondoka kwa sababu familia haijamteua msemaji wa suala hilo, hivyo muda ukifika, litawekwa wazi kwa vyombo vya habari.

“Kwanza, tutambuane nyie ni kina nani? Eee baba si msemaji wa familia… kwanza familia haijamteua msemaji wake kila mtu akisema tunaweza kupishana maneno, muda ukifika mtaambiwa tu.

“Hatuwezi kusema alipo, hayo yote subirini mtaambiwa tukiwa tayari na hata yeye Dk. mwenyewe anaweza kuzungumza, lakini si sasa,” alisisitiza Hidaya huku akionesha hofu na kuwataka waandishi hao kuondoka.

Hata gazeti hili lilipojaribu kutumia mbinu za kiuandishi ili kupata taarifa zaidi juu ya Dk. huyo, baba huyo alisisitiza kuwa hana taarifa zozote zaidi ya kuwasisitizia waandishi kuwa na subira.

Mzee Mwaitenda, alisema kuwa hata hatua ya kuruhusu waandishi hao kuingia ndani ya eneo la nyumba yake ilikuwa ni busara zaidi, la sivyo angeweza kuwarudishia nje ya geti la nyumba hiyo.

“Niwe mkweli, nimetumia busara tu kuwaacha muingie hadi ndani ya geti hilo …kwanza siwafahamu na wala sijawahi kuwaona, ningeweza kuwarudisha pale,” alisema huku akinyoosha kidole.

Mazingira ya nyumbani
Nyumba ya baba yake Dk. Ulimboka inatazamana na nyumba ya kulala wageni iitwayo Samaria, eneo hilo la Kibangu ambayo imezungukwa na ukuta wa matofali ya saruji.

Hata hivyo, Tanzania Daima ilikuta mafundi wawili wakiendelea na kazi ya kuchomelea geti jekundu la kuingilia ndani ya nyumba hiyo ambayo ndani yake kuna nyingine mbili.

Juzi Dk. Ulimboka alirejea kwa kishindo nchini kutoka Afrika Kusini alikokuwa anatibiwa, na kusema yupo tayari kendeleza mapambano na kazi baada ya kupona kabisa.

Dk. Ulimboka alikwenda Afrika Kusini Juni 30 mwaka huu kwa ajili ya matibabu bora zaidi baada ya kutekwa, kupigwa na kutelekezwa kwenye msitu wa Pande, nje kidogo ya Jiji la Dar es Salaam na watu wasiojulikana.

TUCTA watoa neno
Katibu Mkuu wa Shirikisho la Vyama vya Wafanyakazi (TUCTA), Nicholaus Mgaya, ameeleza kufurahishwa na hatua ya kurejea salama kwa Mwenyekiti wa Jumuiya ya Madaktari nchini, Dk. Steven Ulimboka, akisema anaamini hataogopa kuendeleza ujasiri wake katika kupigania haki za madaktari. Akizungumza na Tanzania Daima kwa njia ya simu jana, Mgaya alisema akiwa kama kiongozi wa wafanyakazi, anatambua ujasiri wa Dk. Ulimboka katika kutetea masilai hayo.

“Kama Mtanzania, nimefurahi kwa sababu Ulimboka ni mtu msomi, ni daktari na sisi tuna shida ya madaktari katika nchi hii, kwa hiyo namshukuru Mwenyezi Mungu kwa kumjalia afya njema akarejea salama. “Nikiwa kama kiongozi wa wafanyakazi na nikitambua ujasiri wake katika kupigania haki za madaktari wenzie, nimeguswa sana na kurudi kwake salama na katika afya nzuri, naamini hatakuwa mwoga bali ataendelea na ujasiri aliokuwa nao tangu mwanzo kwa sababu haki siku zote haiji kwenye sahani,” alisema Mgaya.

Mgaya alisisitiza kwamba, anaamini Dk. Ulimboka ataendelea kushirikiana na madaktari wenzie kudai haki zao za msingi ambazo hadi leo hazijalipwa.
Alisema, ni wazi kwamba madai ya madaktari hasa kutaka wapewe vitendea kazi ni halali kwa sababu wanataka iwe hivyo ili waweze kuwatumikia vizuri Watanzania.

No comments:

Post a Comment