To Chat with me click here

Friday, August 17, 2012

VIGOGO WALIOFICHA FEDHA NJE WABANWA


TAKUKURU YASEMA IMEANZA KUWACHUNGUZA


SIKU moja baada ya Naibu Kiongozi wa Kambi ya Upinzani Bungeni, Kabwe Zitto, kutishia kuwataja vigogo wa serikali walioficha mabilioni ya fedha kwenye akaunti za nje ya nchi, ikiwa serikali haitawataja, Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (TAKUKURU), imeibuka na kudai kuwa inazifanyia kazi tuhuma hizo.

Zitto alisema kuwa wamepata taarifa kuwa mmoja  wa viongozi wa juu nchini na baadhi ya mawaziri wa serikali za awamu zilizopita ni miongoni mwa  wamiliki wa fedha hizo zipatazo sh bilioni 314.5.

Alisema sehemu kubwa ya fedha hizo zililipwa na kampuni za utafutaji wa mafuta  na gesi katika pwani ya Mkoa wa Mtwara, zilizopewa mikataba kati ya mwaka 2004 na 2006, hivyo akaitaka serikali iwataje wahusika na kuwachukulia hatua, vinginevyo atawataja kwa majina.

Hata hivyo, Mkurugenzi wa TAKUKURU, Dk. Edward Hoseah, jana alijitokeza katika Kipindi cha Baragumu kinachorushwa na kituo cha runinga cha Channel Ten na kusema kuwa tayari wameanza kazi ya kuchunguza tuhuma hizo.

“Jambo lolote likituhumiwa lazima lifuate taratibu, TAKUKURU imeshawasiliana na Mwanasheria Mkuu wa Serikali kwa sababu ndiyo mamlaka ya kuwasiliana na Uswisi, tufahamu ni kiasi gani benki za Uswisi zinacho na ni kina nani wamehusika, tumfuatilie nani amehusika na ufisadi huo na kupeleka hizo fedha huko,” alisema.

Alisema kwa sasa Uswisi wanayafanyia kazi madai hayo na wakikamilisha kazi hiyo watapeleka majibu kwa Mwanasheria Mkuu wa Serikali na kisha TAKUKURU watajua maeneo gani ya kuyafanyia kazi.

“Kumekuwapo na dhana kwamba hatuwafikishi mahakamani na kwamba kuna watu wametuhonga ili tusifanye hivyo; kama kuna ushahidi tutaachaje kumfikisha mtu mahakamani? Ni aibu kumfikisha mtu mahakamani halafu ionekane huna ushahidi, lakini tukubaliane kwamba kazi inafanyika,” alisema Dk. Hoseah. 

Tuhuma kwa wabunge
Kuhusu tuhuma za baadhi ya wabunge wa Kamati ya Bunge ya Nishati na Madini kudaiwa kujihusisha na rushwa, Dk. Hoseah alisema wanasubiri Bunge limalize kazi yake ndipo nao wafanye kazi yao.

“Itakumbukwa kwamba Mheshimiwa Spika aliunda kamati ya kushughulikia yaliyojitokeza kwa baadhi ya wabunge, tutakachofanya ni kusubiri Bunge lifanye kazi yake,” alisema.

Alisema hatua zitachukuliwa lakini lazima wapishe kamati ya Bunge ifanye kazi yake kwanza. Alisisitiza kuwa wanasubiri ripoti ya kamati hiyo ambayo ilipewa wiki mbili imalize kazi yake ili iwasaidie kuona maeneo gani ya kuyafanyia kazi.

“Sisi tunajikita zaidi kuona sheria ya kupambana na rushwa inavyokwenda, ikiwamo kuona kama kuna mtu alihongwa,” alisema Dk. Hoseah.
Alisema si kila tuhuma TAKUKURU inaweza kuibaini, lakini kuna zile ambazo wamekuwa wakizifanyia kazi ambapo tayari wameshaanza kuwahoji baadhi ya wabunge.
Alisema taasisi yake haiwezi kutangaza kwa umma kila kitu, kwani sheria inawabana, kwamba wanapokuwa wanamchunguza mtu yeyote au taasisi hawaruhusiwi kwenda kutangaza.

Gharama za uchaguzi
Alisema taasisi hiyo inafanya kazi na hadi sasa kuna kesi 24 mahakamani zinazowahusu wanasiasa mbalimbali kudaiwa kuhusika na vitendo vya rushwa wakati wa uchaguzi.

Alisema sheria hiyo ilianza kutumika mwaka 2010, dhana yake kubwa ni kuzuia vitendo vya rushwa wakati wa uchaguzi kwa kumzuia mgombea kutowarubuni wananchi kwa fedha ili washawishike kumchagua.

“Mwanasiasa yeyote anapotaka kuingia kwenye ulingo wowote wa siasa lazima awe na fedha ili aweze kufanya hivyo, vitu vyote vinakubalika, lakini asichoruhusiwa kufanya ni kuwarubuni wananchi kwa zawadi, usafiri, chakula na mengine ili wamchague,” alisema Dk. Hoseah.

Pamoja na mambo mengine, alisema kuna haja ya kuangalia mfumo mzima kwa vyama vya siasa ili kumudu gharama za uchaguzi wakati wa uchaguzi.
Aliweka wazi kwamba ni vigumu kushughulikia vitendo vya rushwa, kwa sababu ofisi za TAKUKURU hazijafika kwenye maeneo ya kata, bali wako kwenye wilaya.

Alisema ili kuvidhibiti ni jukumu la wanasiasa wenyewe kuheshimu suala hilo kwa kuepuka kutoa rushwa.

No comments:

Post a Comment