To Chat with me click here

Wednesday, August 29, 2012

NITAISHI KUWA MELES ZENAWI


Mwaka 1975 Mwanafunzi wa mwaka wa Kwanza wa Chuo Kikuu cha Haile Selasie (sasa Chuo Kikuu cha Addis Ababa) Legese Zenawi, akiwa na umri wa miaka 19 tu, aliacha masomo yake na kujiunga na kikundi cha Ukombozi cha watu wa Tigray (Tigray Peoples Liberation Front). Legese alikuwa anasomea shahada ya kwanza ya udaktari. Hakurudi tena Chuoni kusomea Udaktari na hakuishi tena maisha ya ujana ambayo sisi wengine wote tumeishi na kuyafurahia. Mwaka 2012 Legese akiwa na umri wa miaka 57 alifariki dunia. Lakini aliaga dunia akiwa Meles Zenawi na sio Legese Zenawi, jina alilopewa na wazazi wake huko Adwa kaskazini mwa Ethiopia.

Legese alibadili jina lake kwa hiari yake kufuatia kuuwawa kwa rafiki yake na mpiganaji mwenzake Meles mwaka 1975. Aliamua kumuishi mpiganaji mwenzake kwa kuchukua jina lake na kuacha jina alilopewa na wazazi wake. Meles alifanikiwa kupigana dhidi ya utawala wa kiimla wa Mengistu Haile Mariam na kumtoa madarakani na kuingiza uongozi wa kimaendeleo chini ya chama cha Kitaifa cha Ethiopian People’s Revolutionary Democratic Front (EPRDF). Meles Zenawi aliahidi kumpigania rafiki yake Meles kwa faida ya wananchi wanyonge wa Ethiopia na akatimiza ahadi hiyo kwa mafanikio makubwa sana.

Mwanzoni Meles alipigana kwa lengo la kutaka uhuru wa eneo la Tigray kutoka Utawala wa Mengistu na kundi la wanajeshi chini ya Derg. Meles na wenzake waliamini kabisa kwamba utawala nchini mwao chini ya Mfalme Haile Selasie na hata chini ya utawala wa Derg uligubikwa na ukabila na ueneo kwa faida ya kabila kubwa nchini humo, Amhara.Aliamini kwamba makabila madogo kama kabila lake la Tigray kutoka kaskazini mwa Ethiopia na hata makabila mengine kama Wasomali walikuwa wanakandamizwa na kunyonywa ndani ya nchi yao. Aliamini kwamba utajiri wa nchi ulikuwa unatumika kwa faida ya kundi moja lililohodhimadaraka ya nchi na kabila lao. Akiwa na umri wa miaka 19 tu na mwanafunzi wa mwaka wa kwanza wa Chuo Kikuu aliamua kushika silaha na kupambana na ugandamizaji huu.

Hata hivyo Meles alibadili kabisa mtazamo wake alipogundua kuwa sio watu wa Tigray tu waliokuwa wakinyonywa na kugandamizwa na utawala wa Mengistu bali ilikuwa ni WaEthiopia wote bila kujali makabila yao. Mwaka 1985 alichaguliwa kuwa Mwenyekiti wa chama cha TPLF akiwa na umri wa miaka 29 tu.Alihakikisha anaikomboa Tigray kama mkakati wa kuikomboa Ethiopia yote. Alishirikiana na wakombozi wa Jimbo jirani la Eritrea ili kutetea Uhuru wao na kuwapa uhuru wa kuamua kama wanataka kubakia sehemu ya Ethiopia au kuwa Taifa huru ambapo waliamua kuwa Taifa huru. Akiwa kijana wa chini ya umri wa miaka 30 aliunganisha makundi mbalimbali yaliyokuwa na lengo la kuleta ukombozi na kujenga Ethiopia mpya chini ya mwavuli ya chama cha EPRDF. EPRDF ilikuwa ni umoja wa makabila yote nchini Ethiopia na walimchagua Meles kuongoza mapamabano ya ukombozi.

Mwaka 1991 Meles Zenawi aliongoza EPRDF kuingia Addis Ababa na kushika Dola huku Mengistu akikimbilia nchini Zimbabwe. Meles akiwa na umri wa miaka 36 tu alichaguliwa kuwa Rais wa muda wa Ethiopia na mkutano mkuu wa kitaifa ambao kwa mara ya kwanza ulikutanisha makabila yote nchini Ethiopia. Miaka mitatu baadaye kufuatia kura ya maoni Jimbo la Eritrea likajitenga kutokaEthiopia na kuunda Taifa huru. Meles alitimiza ahadi yake ya kuruhusu watu wa Eritrea kuamua kama wanataka kuwa Taifa linalojitegemea au kuwa sehemu ya Shirikisho la Ethiopia. Hata mahusiano kati ya Ethiopia na Eritrea yalipokuwa mabaya sana kiasi cha kupigana vita kugombea kijiji cha Badme, Meles hakuchukua fursa hiyo kuirudisha Eritrea kuwa mkoa ndani ya Ethiopia au hata kupata njia ya kwenda baharini, bali aliheshimu matakwa ya waEritrea ya kujitawala.

Ukweli ni kwamba vita kati ya Eritrea na Ethiopia ilikuwa ni vita isiyo na maana yeyote ile na itabakia kuwa doa katika historia ya uongozi wa Meles. Kitendo cha Meles kutoheshimu maamuzi ya Umoja wa Mataifa kwamba Badme ni sehemu ya Eritrea pia ni doa ambalo wafuasi wa Meles wataendelea kuwa nalo daima dumu na wakosoaji wa Meles wataendelea kujengea hoja kuonyesha kuwa Kiongozi huyu hakuwa anaheshimu maamuzi ya Taasisi za kimataifa. Hata hivyo doa hili haliwezi kufuta kabisa mafanikio makubwa ambayo kamaradi Meles ameyapata katika Ethiopia iliyokombolewa.

Meles alipochaguliwa kuwa Kiongozi wa chama cha TPLF mwaka 1985 Ethiopia ilikuwa kwenye ramani ya dunia kama Taifa lililoshindwa kulisha watu wake. Dunia nzima kulikuwa na kampeni za kusaidia kuondoa njaa nchini humo ambayo iliua zaidi ya watu milioni moja. Wakati mauaji ya kimbari nchini Rwanda yaliua watu milioni moja kwa mapanga na mashoka, njaa iliua watu kama hao hasa katika maeneo ya Tigray na Wollo kwa sababu ya uzembe wa Serikali ya Mengistu. Mmoja wa wajumbe wa Kamati Kuu wa chama cha Mengistu kilichokuwa kinatawala wakati ule (Workers Party of Ethiopia) bwana Dawit Wolde alimtahadharisha Mengistu kuhusu hali mbaya ya wananchi na kwamba Serikali ilipaswa kuchukua hatua na kujibiwa ‘kulikuwa na mabaa ya njaa miaka yote kabla sisi hatujatawala. Hiyo ni namna uasili (nature) inafanya kazi yake. Kuingilia uasili ndio maana leo tumefikia watu milioni 40’( Meredith in The State of Africa). Mengistu alilewa madaraka kiasi cha kusahau kwamba siku moja kabla ya kumvua madaraka Mfalme Haile Selasie walimwonyesha filamu (The hidden famine) ya namna yeye alivyokuwa anastarehe na pombe aghali na kulisha nyama mbwa wake ilhali wananchi wake walikuwa wanakufa kwa kukosa chakula katika baa la njaa la mwaka 1984 katika Wilaya ya Wollo. Haile Selasie baada ya kuonyeshwa filamu hiyo alipoteza fahamu kwa mawazo na siku iliyofuata tarehe 12 Septemba 1974 akavuliwa ufalme na vijana watatu wanajeshi akiwemo Mengistu Haile Mariam. Mengistu huyo huyo akiwa Rais wa Ethiopia akawa anajenga hoja kwamba njaa ni tukio la asili ili ‘kubalance’ idadi ya watu nchini mwake! Haya ndio mazingira ambayo Meles alichaguliwa kwayo kuongoza mapambano ya ukombozi akiwa na umri wa miaka 29 tu.

‘naomba vitabu vya Uchumi’ ndio ombi pekee Meles alilitoa kwa  mwanahabari wa kigeni aliyekwenda kumfanyia mahojiano mara baada ya kuchukua uongozi wa Taifa lake. Mwanahabari huyo alimwuliza ni msaada gani anataka kutoka kwa nchi za magharibi ili awaambie kupitia habari yake anayokwenda kuandika. Meles alijua kwamba ana ajenda moja kubwa nayo ni kuondoa njaa. Kuondoa Umasikini nchini mwake. Ajenda hii Meles aliifanyia kazi kwa nguvu zake zote kipindi chote ambacho yeye alikuwa Rais na Baadaye Waziri Mkuu wa Ethiopia.

Nakumbuka tulikuwa tunatania mtu yeyote aliyekondeana kwa kusema ‘ana njaa kama Ethiopia’ na hiyo ndio ilikuwa picha inayokuja machoni mwa watu wengi duniani kuhusu Ethiopia. Meles hakumaliza shida zote za Ethiopia, lakini alipambana nazo. Alizipunguza. Amelitoa Taifa lake kutoka Taifa la kupigiwa mfano kwa njaa na umasikini kwenda Taifa la kupigiwa mfano kwa maendeleo. Katika kipindi cha miaka ishirini ya utawala wake hatujasikia baa kubwa la njaa kama ilivyozoeleka kila muongo nchini humo. Mwana historia mmoja nchini humo alionyesha kuwa kila muongo ulikumbwa na njaa kali nchini Ethiopia, 1958, 1966, 1973 na 1984. Lakini toka Meles achukue uongozi wa Taifa la Ethiopia hatukusikia njaa miaka ya tisini wala miaka ya 2000. Ninaamini watakaomrithi Meles watahakikisha kuwa hakuna njaa tena ya kiwango kile nchini Ethiopia kwa miongo mingine yote ijayo. Mafanikio haya yanatokana na sera na maamuzi thabiti na ya dhati kutoka kwa kiongozi ‘Sitaki njaa nchini kwangu’. Pia usimamizi thabiti wa maamuzi sahihi yaliyotolewa.

Meles aliamua kupambana na umasikini na kujenga Taifa lenye nguvu za kiuchumi. Aliamua mapema kabisa kukataa ushauri wa IMF na Benki ya Dunia wa kuufungua uchumi wa Ethiopia haraka sana (liberalisation). Yeye na wenzake waliamua kuufungua uchumi kidogo kidogo kulingana na ratiba waliyojiwekea wao wenyewe. Kutokana na hali hiyo sehemu kubwa ya uchumi wa Ethiopia umeshikwa na wao wenyewe wananchi wa Ethiopia. Amejenga miundombinu kuunganisha uchumi wa nchi na hivyo kufungua masoko ya ndani licha ya yeye mwenyewe Meles kusisitiza sana mauzo ya nje. Kutokana na maamuzi yake, hivi sasa Ethiopia itaanza kuuza nje Viatu vya ngozi vilivyotengenezwa nchini humo vyenye thamani ya dola za kimarekani bilioni nne. Hii ni sawa na mara mbili ya mauzo ya dhahabu yote ya Tanzania kwenye soko la dunia. Ethiopia haina mafuta wala madini ya kutosha kama Tanzania, lakini uchumi wake umekuwa ukikua kwa zaidi ya asilimia kumi kwa miaka saba mfululizo. Ndio maana Meles ameweza kupunguza umasikini kutoka asilimia 45 ya watu waliokuwa wakiishi kwenye dimbwi la umasikini mwaka 1991 mpaka asilimia 29 mwaka 2011. Katika kipindi kama hicho (1991 – 2011) Umasikini Tanzania ulishuka kutoka asilimia 37 ya watu kuishi kwenye dimbwi la Umasikini mpaka asilimia 35 tu. Tanzania iliamua kufuata sera za kufungua uchumi wa nchi kwa haraka kama walivyoshauri Taasisi za IMF na Benki ya Dunia.

Wakati Meles anaaga dunia ameacha mradi mkubwa sana unatekelezwa nchini mwake. Mradi wa kuzalisha umeme 10,000 MW, Grand Millenium Project. Lengo lake ni kuzalisha umeme wa kutosha kufanya mabadiliko makubwa ya maisha ya wananchi wa Ethiopia na pia kuuza nchi jirani (Diplomasia ya Nishati). Benki ya Dunia ilikataa kufadhili mradi huu, yeye akaamua kila muEthiopia kutoa fedha za kufadhili mradi huu. Wananchi wa Ethiopia wote kila mmoja akajitolea mshahara wake wote wa Mwezi mmoja na fedha hii kugeuzwa kuwa dhamana. Pia wananchi wa Ethiopia wanaoishi nje ya nchi nao waliruhusiwa kununua dhamana hizi na kufadhili mradi huu kabambe. Mradi unatekelezwa kwa fedha za WaEthiopia wenyewe. Nina imani kuwa mradi huu utaendelezwa na viongozi wapya wa Ethiopia. Uzuri ni kwamba Meles alilea kizazi kipya cha uongozi. Aliamua kuchukua vijana wa rika mbili chini yake na kuwapa majukumu na kuwalea kiuongoni ili waweze kuwa tayari kurithi mikoba ya viongozi wanaomaliza muda wao. Waziri Mkuu mpya wa Ethiopia ana umri wa miaka kumi chini ya Meles. Meles alijua umuhimu wa kuandaa viongozi wa baadaye. Yeye hakuandaliwa. Mazingira ya ugandamizwaji, unyanyasaji na umasikini yalimwita kuchukua majukumu ya kiuongozi akiwa kijana mdogo sana wa miaka 19 alipoamua kujiunga na jeshi la ukombozi, miaka 29 alipochaguliwa kuongoza jeshi la ukombozi na miaka 36 alipochaguliwa kuwa Rais na baadaye Waziri Mkuu wa Taifa lake.

Meles ana makosa yake kama binaadamu. Amelaumiwa sana na mataifa ya magharibi kuhusu rekodi yake ya masuala ya haki za binaadamu na kidemokrasia. Lakini pia amelaumiwa na baadhi ya wanaharakati kwa kuuza ardhi ya wananchi kwa makampuni ya kilimo ya mashariki ya kati na mashariki ya mbali kama China. Hata hivyo sijawahi kusikia tuhuma zozote za Meles kuhusu ufisadi na kujilimbikizia mali. Siku zote aliamini kuwa cheo ni dhamana na hakutumia cheo chake  kwa faida yake tofauti na viongozi wengi sana wa kiafrika. Hapa nchini kwetu tunashuhudia watu wakitumia nafasi zao za uongozi kulimbikiza mali. Watu wana tamaa iliyokithiri ya mali. Ufisadi imekuwa ni hulka na sasa ufisadi unahusisha nafasi yeyote ya uongozi. Hata tuhuma za ufisadi na rushwa zimekuwa za kawaida mno mpaka unakuta wala rushwa wanatuhumu viongozi wenye maadili ili mradi tu ionekane rushwa ni ya kila mtu wa kila chama. Imekuwa kama Wezi kuungana kumkimbiza Polisi. Meles hakutaka Ethiopia ifikie hali hii. Alipambana na rushwa yeye mwenyewe kwa kujiwekea viwango vya kutokuwa na mawaa ya rushwa au matumizi mabaya ya Ofisi ya Umma.

Meles Zenawi ameacha mfumo wa Uchumi ambao haujapata fursa ya kujadiliwa vya kutosha. Mfumo ambao umeiweka Ethiopia kuwa moja ya mataifa yatakayokuwa na nguvu kubwa ya kiuchumi katika bara la Afrika ndani ya muongo mmoja na nusu ujao. Meles alipambana na umasikini kwa dhati na kwa nguvu inayostahili. Meles ametimiza wajibu wake.

Natamani kuwa Meles maana ameishi anachoamini kwa kupambana na ufisadi bila yeye kuwa fisadi ama kutumia vibaya Ofisi yake ya Umma. Nitaishi kuwa Meles maana adui wetu nambari moja ni Umasikini, umasikini wa vijijini. Meles alitangaza mwaka 1991 ‘our first enemy is poverty and backwardness’ na akapambana na adui umasikini kadiri ya uwezo wake. Hakuna namna bora zaidi ya kumuenzi Meles zaidi ya kutenda yale mema aliyoyatenda na kurekebisha yale aliyoyakosea.

Nilipata fursa ya kukutana na Meles mara moja. Nilikutana naye nchini Nigeria katika mkutano kuhusu mashirikiano ya kiuchumi kati ya nchi za Ulaya na nchi za Kiafrika mwaka 2009. Baada ya mkutano ule niliamua kumsoma Meles na misingi anayosimamia. Ni kama nilimwona Mahathir Mohamad wa Malaysia ndani ya Meles Zenawi kwa namna ya utendaji wao na uwezo wao wa kujenga hoja. Isipokuwa tu Meles hakumaliza shahada yake ya udaktari na Mahathir alimaliza yake. Ni dhahiri kwamba Meles Zenawi alikuwa ni kiongozi mwenye uwezo mkubwa sana kiakili pengine kuliko viongozi wote wa kizazi cha pili barani Afrika. Uwezo wake wa Akili uliwatisha viongozi wa mataifa ya Magharibi. Walimwogopa. Wenzake wa Afrika walimheshimu. Alikuwa sauti ya Afrika kutoka Addis Ababa, Makao makuu ya Afrika.Upumzike kwa amani Meles.

No comments:

Post a Comment