To Chat with me click here

Wednesday, August 22, 2012

KADA CCM ATANGAZA KUMVAA JK


KADA wa Chama Cha Mapinduzi (CCM), Maliki Marupu kutoka wilayani Ulanga, mkoani Morogoro, ametangaza nia kuwania nafasi ya uenyekiti wa CCM taifa, inayoshikiliwa na Rais Jakaya Kikwete.

Marupu ambaye amejitambulisha kuwa ni Mjumbe wa Mkutano Mkuu CCM Taifa, alisema kuwa amefikia hatua hiyo ili kuleta mabadiliko ndani ya chama hicho tawala.

Wiki iliyopita, gazeti hili liliripoti taarifa za kuwapo kundi linalompinga Rais Kikwete kutaka kutenganisha kofia ili asiendelee kuwa Mwenyekiti wa CCM taifa, na kumpa nafasi ya kubaki kwenye kiti cha urais.

Akizungumza na waandishi wa habari jijini Dar es Salaam jana, Marupu alisema kama fomu za kuwania nafasi hiyo zitatolewa, ataandika historia mpya ndani ya chama hicho.
 
Hata hivyo, chini ya utaratibu wa sasa wa CCM, nafasi ya mwenyekiti taifa haigombewi, bali jina la mgombea ambaye kwa kawaida huwa ni Rais wa Muungano huteuliwa na Kamati Kuu (CC), kuthibitishwa na Halmashauri Kuu (NEC) na hatimaye kupigiwa kura na wajumbe wa mkutano mkuu.

Huku akinukuu Katiba ya CCM, alisema ibara ya 14 kifungu kidogo cha 3, kinampa nafasi mwanachama yeyote ndani ya chama hicho kuwania nafasi katika ngazi yoyote.

“Unajua lazima tuwe wazi. Kinachoogopwa hapa ni kama ikitokea mwenyekiti akawa sio rais, iwapo patatokea kutoelewana kati yao, basi mwenyekiti wa chama ana uwezo wa kushawishi wanachama wakamvua madaraka rais,” alisema.

Marupu alisema, utaratibu unaotumika wa kumpata mwenyekiti, umekuwa ukidumaza demokrasia ndani ya chama hicho.

Kada huyo alisema, wapo watakaomuona msaliti ndani ya chama, lakini amelazimika kuwania kiti hicho kuleta mabadiliko yanayoenda na wakati.

“Wajumbe wakinipitisha, mchuano wangu na Kikwete utakuwa kama ule uliowahi kutokea nchini Afrika Kusini kati ya aliyekuwa rais, Thabo Mbeki na rais wa sasa Jacob Zuma aliyeibuka mshindi,” alisema. 

Chanzo: Tanzania Daima

No comments:

Post a Comment