To Chat with me click here

Wednesday, August 15, 2012

JK ATISHIWA KUNG’OLEWA CCM


KUNDI LAIBUKA KUTAKA AACHIE CHAMA, ABAKI NA URAIS

WAKATI uchaguzi ndani ya Chama Cha Mapinduzi (CCM) ngazi ya taifa ukikaribia, kundi linalopigania mabadiliko kutaka kutenganisha kofia ya urais na uenyekiti limeibuka upya kutaka mabadiliko hayo. Hoja hiyo imeibuka sasa wakati zimebaki siku saba kabla ya CCM kuanza kutoa fomu za kuwania uongozi ngazi ya taifa.

Mtandao wa kundi hili pana unaunganisha baadhi ya vigogo wa CCM, wakiwamo wenyeviti na makatibu wa mikoa na wilaya na makada maarufu ambao hujulikana kama majeruhi wa kisiasa waliotokana na makundi yenye uhasama ndani ya chama hicho tawala.

Kundi la mlengo huo wa mabadiliko hayo linataka Rais Jakaya Kikwete ambaye pia ni mwenyekiti wa chama hicho taifa, aachie nafasi ya uenyekiti ili abaki kuwa rais, kumalizia muda wake. Hata hivyo, kwa mujibu wa Katiba ya CCM ya sasa, nafasi ya mwenyekiti na makamu wake hazigombewi, bali hutokana na uteuzi wa Kamati Kuu (CC) ambayo chini ya utaratibu wa sasa, rais ndiye anayekuwa mwenyekiti wa chama taifa.

Muundo huo wa uongozi uliasisiwa na Mwalimu Nyerere wakati ule, kwa hofu kwamba kama rais na mwenyekiti wanakuwa watu tofauti, ikitokea kwamba hawaelewani, nchi haitatawalika. Sababu kubwa inayotajwa na kundi linalotaka mabadiliko hayo, ni kutaka kumpunguzia majukumu rais ili abaki kuiongoza serikali na shughuli za chama zisimamiwe na mtu mwingine, ambaye atakuwa na nafasi ya kutosha kukisimamia na kukiendesha.

“Baadhi ya wana CCM wanatuelewa vibaya kwamba tunataka kufanya uasi ndani ya chama, hapana. Huu ni muundo mzuri unaotumika katika nchi nyingi duniani, na mfano ni Afrika Kusini. Lengo letu tunataka kumpunguzia rais majukumu na chama kibaki na mtu mwingine,” alisema mmoja wa vigogo wa mkakati huo.

Uchukuaji wa fomu kuwania nafasi za uongozi wa CCM taifa, unatarajiwa kuanza Agosti 22 hadi 28. Akizungumzia tishio la kutaka kumng’oa Rais Kikwete, Katibu wa Itikadi na Uenezi wa CCM, Nape Nnauye, alisema kundi hilo linajidanganya kwani mkakati huo hauwezekani kwa sasa.

“Ni kweli tunajua kuna presha hiyo. Lakini ni mambo ya kushangaza, kwa sababu nafasi ya mwenyekiti na makamu hazigombewi, hao wanaotaka mtu mwingine agombee nafasi hiyo hizo fomu anazipata wapi na nani atakayempa?” alihoji Nape.

Alisema fomu za ngazi ya taifa zitakazotolewa kuanzia Agosti 22, zinahusu wajumbe wa halmashauri kuu pekee na si nafasi ya mwenyekiti wala makamu wake. “Kwa kawaida nafasi ya mwenyekiti na makamu wake inapendekezwa na Kamati Kuu na kisha majina yao yanathibitishwa na NEC. Na hata kwenye kuomba kura, anaombewa na wajumbe wa Kamati Kuu,” alisema Nape.

Kwa mujibu wa Nape, kundi linalotaka mabadiliko hayo kwanza lijitokeze na kisha lilete hoja hiyo katika utaratibu unaopaswa, na si kujificha na kutaka kufanya uhaini, jambo ambalo halikubaliki ndani ya chama.

No comments:

Post a Comment