To Chat with me click here

Sunday, August 26, 2012

MAKADA CCM WAMNYOOSHEA KIDOLE MKAPA

KITENDO cha Mahakama Kuu Kanda ya Tabora kutengua matokeo ya ubunge Jimbo la Igunga yaliyompa ushindi Dk Dalaly Peter Kafumu (CCM), kimeibua mvutano mwingine ndani ya CCM, ambapo sasa baadhi ya makada wake wameanza kumnyooshea kidole Rais Mstaafu Benjamin Mkapa na baadhi ya mawaziri kuwa ndiyo chanzo cha kushindwa huko.

Baadhi ya makada maarufu na wenye uzoefu wa muda mrefu ndani ya chama hicho tawala, kwa nyakati tofauti kwenye mahojiano na Mwananchi Jumapili wamekiri kwamba, imefika mahali ambapo CCM inapaswa ijitazame na kuwa makini juu ya watu inaopaswa kuwatumia katika kampeni zake.


Katika tathmini yao, makada hao wamemtaja Rais Mstaafu Mkapa na mawaziri kadhaa, wakisema kuwa CCM haikuwa makini katika kuwateua wasimame kwenye majukwaa kupiga kampeni za kisiasa. Walitaja moja ya sababu kuwa ni Mkapa na baadhi ya mawaziri hao mashuhuri kuwa siyo wanasiasa wa jukwaani bali ni watendaji.


Licha ya CCM kujaribu kumtumia rais huyo mstaafu na mawaziri hao kutokana na heshima iliyojengeka kwao mbele ya Watanzania walio wengi, tathmini ya makada hao inaeleza kuwa hoja zao katika kampeni ama ziliwapa mwanya wapinzani, hasa Chadema kuiumbua CCM kwenye propaganda za majukwaani, hata kisheria.


Walikuwa wakizungumzia chaguzi ndogo zilizofanyika hivi karibuni katika Jimbo la Arumeru na ule wa Igunga Oktoba mwaka jana, ambao licha ya CCM kushinda, wiki hii mahakama kuu ilitengua ushindi huo. Kuanguka Igunga Dk Kafumu aliibuka mshindi kwenye uchaguzi mdogo uliofanyika Oktoba 2, mwaka jana kuziba nafasi ya Rostam Aziz aliyejiuzulu kwa madai ya kuchoshwa na kile alichoita siasa za majitaka ndani ya CCM, lakini mahakama imetengua ushindi wake.

Uchaguzi huo ulikuwa wa ushindani mkubwa kati ya Dk Kafumu na aliyekuwa mgombea wa Chadema, Joseph Kashindye ambaye aliamua kupinga ushindi wa Dk Kafumu mahakamani akidai hakuridhishwa na mwenendo wa uchaguzi huo. Kashindye alifungua kesi hiyo Machi 26, mwaka huu. Wakati wa kampeni za uchaguzi huo vigogo mbalimbali wa CCM akiwamo Mkapa walipiga kambi Igunga na kushiriki mikutano mbalimbali ya kampeni, ambapo pamoja na mambo mengine walitoa kauli tata zilizosababisha CCM kushindwa katika kesi hiyo.

Mbali na Mkapa viongozi wengine waliotoa kauli hizo na sasa wananyooshewa vidole ni Waziri wa Ujenzi, Dk John Magufuli, Katibu Mkuu wa CCM, Wilson Mukama na Mbunge wa Tabora, Ismail Aden Rage. Kauli tata ya Mkapa Wakili wa mlalamikaji, Profesa Abdallah Safari, Agosti 20 mwaka huu aliwasilisha mahakamani hapo zaidi ya malalamiko 13 dhidi ya Dk Kafumu na wenzake.


Mbali na kueleza yaliyozungumzwa na Dk Magufuli, Profesa Safari alidai hoja nyingine ni Baraza la Waislamu (Bakwata) Wilaya ya Igunga kuwakataza waumini wasiipigie kura Chadema na kwamba naye Rais Mstaafu Benjamin Mkapa alitoa ahadi ya kugawa mahindi kwa wananchi wa Igunga siku moja kabla ya uchaguzi ili waichague CCM. Makada waonya


Mbunge wa Kahama, James Lembeli alisema kuwa utaratibu wa sasa wa chama hicho kuwatumia viongozi wastaafu umepitwa na wakati kwa sababu Watanzania wa sasa hawahitaji kusikia maneno mengi, bali sera. Alisema kuwa CCM inatakiwa itazame ilipojikwaa na kuacha kutafuta mchawi kwa kuwa matatizo yaliyokifikisha chama hicho kilipo sasa yanajulikana.


“Kampeni za CCM hivi sasa hazina maandalizi, kila anayeweza kuzungumza anachukuliwa na kujumuishwa kwenye kampeni, jambo ambalo siyo sahihi,” alisema Lembeli na kuongeza: “Inatumia watu bila kuangalia kama wanakubalika, katika chaguzi zinazokuja, chama kiwatumie makada wanaopendwa na wananchi na wenye uwezo wa kuuza sera za chama.”


Alitaja sababu nyingine ya CCM kuanguka hasa Igunga kuwa ni pamoja na mgawanyiko uliokuwapo ndani ya chama hicho baada ya baadhi ya makada kuzuiwa kushiriki katika kampeni hizo wakati wana mvuto kwa wapiga kura. Akitolea mfano watu hao alisema kuwa ni pamoja na Mbunge wa Urambo Mashariki, Samuel Sitta, ambapo alibainisha kuwa waliotoswa katika kampeni hizo wasingeweza kuishiwa maneno ya kuzungumza na kuanza kutoa ahadi zinazovunja sheria ya uchaguzi.


Dk Kigwangallah Akizungumzia suala hilo, Mbunge wa Jimbo la Nzega, Dk Hamisi Kigwangallah alisema kitendo cha CCM kutumia vigogo akiwamo Rais mstaafu Mkapa katika uchaguzi wa Igunga, ndiyo chanzo cha kushindwa kwa kesi hiyo kwa kuwa walizungumza mambo yasiyo na msingi wowote.

Dk Kigwangallah ambaye Agosti 22 alichukua fomu za kuwania kiti cha Uenyekiti wa Jumuiya ya Wazazi Taifa alisema kuwa uchaguzi mwingine ukifanyika katika jimbo hilo, viongozi na wabunge kutoka mikoa ya Tabora, Mwanza na Shinyanga ndiyo waachwe kufanya kampeni.

No comments:

Post a Comment