To Chat with me click here

Friday, August 24, 2012

MAANDALIZI YA SENSA UTATA MTUPU


IKIWA imebaki siku moja kuanza kwa sensa ya watu na makazi, kuna uwezekano wa shughuli hiyo ikakwama jijini Dar es Salaam kutokana na kuendelea kuwapo kwa mivutano ya malipo ya makarani watakaosimamia kazi hiyo.

Kampeni ya sensa ya watu na makazi ilizinduliwa na Waziri Mkuu, Mizengo Pinda wiki iliyopita katika viwanja vya Mnazi Mmoja na inatarajia kuanza kufanyika Agosti 26, mwaka huu na kudumu kwa wiki moja.

Kundi la makarani zaidi ya 30 jana liliandamana hadi katika ofisi za Wilaya ya Kinondoni likitaka kujua hatma ya malipo yao ya sh 240,000 za kuhudhuria semina kwa ajili ya mafunzo kwa siku saba.

Akizungumza kwa niaba ya wenzake, Judith John, alisema kuwa hadi sasa sensa hiyo ina uwezekano mkubwa wa kutofanikiwa kutokana na kuwepo kwa sintofahamu juu ya malipo yao.


Alisema baadhi ya makarani walipewa fedha nusu ya sh 140,000 badala ya sh 245,000 huku wengine wakiwa hawajui hatima ya malipo yao.

“Tunaona kuwa kuna watu wana lengo la kuharibu hii sensa isifanikiwe, haiwezekani tangu tuanze mafunzo hadi sasa tunahangaikia tu malipo bila kula kiapo wala kuingia mkataba kwa kazi hiyo,” alisema.

Alisema kuwa kwa sasa wamelazimika kurudi katika ofisi za wilaya ili kuendelea kusubiri kulipwa fedha zao ambapo hadi sasa hakuna hatua yoyote iliyochukuliwa.

Hata hivyo vyanzo vya habari hii vilifanikiwa kukutana na mtumishi mmoja wa wilaya hiyo (jina linahifadhiwa) ambaye alikiri kuwepo kwa uzembe katika mchakato huo na kwamba kuna uwezekano mkubwa wa kushindwa kufanikiwa.

Mtumishi huyo alisema kuwa kulikuwa na uwezekano wa kupata fedha mapema kutoka benki lakini baadhi ya viongozi wanaonekana kutaka kujinufaisha wao binafsi jambo ambalo linaweza kuleta matokeo hasi.

Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam, Said Meck Sadick, alifafanua kuhusu mvutano na kusema kuwa wanaoendelea kukosa malipo ya semina inawezekana si makarani halisi wa sensa kwani asilimia kubwa walilipwa nusu ya fedha zao.

Sadick alikiri kuwepo kwa kasoro katika suala hilo lakini akasema kwa sasa limerekebishwa na utaratibu wa malipo katika vituo vyote jijini humo unaendelea.

“Niseme kuwa benki haiwezi kuishiwa fedha, kilichojitokeza ni malipo tu kuchelewa kwani malipo yanayotakiwa kutolewa ni makubwa na lazima unapohitaji fedha nyingi upeleke mapema maombi yako,” alisema.

No comments:

Post a Comment