To Chat with me click here

Monday, August 27, 2012

MWAKYEMBE, KAGASHEKI WASIFIWA


Katika hatua nyingine Kamati Kuu ya CCM (CC), imeeleza kuridhishwa na utendaji wa mawaziri, Dk. Harrison Mwakyembe wa Ujenzi, Balozi Khamis Kagasheki wa Maliasili na Utalii na Dk. Abdallah Kigoda wa Viwanda na Biashara katika kuwachukulia hatua wakuu wa mashirika ya umma waliojihusisha na ubadhirifu.

Bila kuwataja kwa majina, Nape alisema kuwa CC ilipokea taarifa ya maendeleo ya utekelezaji wa maagizo yake juu ya kushughulikia mapungufu yaliyooneshwa kwenye taarifa ya Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali (CAG) na kamati mbalimbali za Bunge.

“CC imeipongeza serikali kwa hatua zilizoanza kuchukuliwa dhidi ya mapungufu hayo, hasa hatua dhidi ya wakuu mbalimbali wa mashirika kadhaa ya umma, kama vile Shirika la Ugavi wa Umeme (TANESCO), Shirika la Viwango (TBS), Mamlaka ya Bandari Tanzania (TPA), Shirika la Ndege Tanzania (ATC) na Wizara ya Maliasili na Utalii,” alisema.


Hata hivyo, licha ya kutotajwa kwa majina, mawaziri hao watatu wameanza kazi kwa vitendo ikiwa ni kuwasimamisha kazi baadhi ya vigogo kwenye wizara zao waliokuwa wakituhumiwa kujihusisha na ufisadi.

Dk. Mwakyembe ameanza kwa kumsimamisha kazi aliyekuwa Kaimu Mkurugenzi Mkuu wa ATC, Paul Chizi na wakurugenzi wanne kutokana na ukiukwaji wa sheria, kanuni na taratibu za utumishi wa umma. Na wiki aliyopita amemsimamisha kazi Mkurugenzi Mkuu TPA, Ephraim Mgawe na viongozi wengine watatu ili kupisha uchunguzi wa tuhuma mbalimbali za ufisadi zinazowakabili.

Waziri Kigoda yeye alianza kazi kwa kumsimamisha aliyekuwa Mkurugenzi Mkuu wa TBS, Charles Ekelege ili kupisha uchunguzi wa tuhuma za ufisadi zilizokuwa zikimkabili.

Agosti 13 mwaka huu, Waziri Kagasheki, alitangaza kuwatimua kazi vigogo watatu wa wizara yake akiwamo Mkurugenzi wa Wanyamapori, baada ya kubainika kuhusika katika kashfa ya utoroshaji wanyamapori hai kupitia Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Kilimanjaro (KIA) kwenda nje.

Vile vile wiki aliyopita, alitangaza kubadili utaratibu za kuwapata wajumbe wa bodi zilizoko chini ya wizara ambapo kuanzia sasa watapatikana kwa njia ya ushindani badala ya kuteuliwa moja kwa moja na waziri.

Nape aliongeza kuwa, itakumbukwa kuwa CC iliagiza pamoja na viongozi wa kisiasa kuchukuliwa hatua kwa mapungufu yale, ipo haja ya kuwachukulia hatua watendaji wakuu wa mashirika yaliyohusishwa na ubadhirifu mbalimbali.

“Kamati Kuu inawapongeza mawaziri husika na watendaji wote wa serikali walioanza kutekeleza agizo hili kwani mwisho wa siku maisha bora kwa kila Mtanzania yatawezekana,” alisema.

No comments:

Post a Comment