To Chat with me click here

Thursday, December 27, 2012

SUGU AMUUMBUA WAZIRI WA JK


Mhe. Joseph Mbilinyi (Sugu)
MBUNGE wa Mbeya Mjini, Joseph Mbilinyi (CHADEMA), amemuumbua Naibu Waziri wa Elimu na Mafunzo ya Ufundi, Philip Mulugo, akidai hatishwi na kauli zake kwani ana elimu ya kuungaunga akiwa ametumia jina la mtu mwingine.

Kauli ya Mbilinyi maarufu kama Sugu, inakuja siku chache tangu Mulugo atangaze kuwa Chama Cha Mapinduzi (CCM), kitayarejesha majimbo yaliyoko mikononi mwa CHADEMA mkoani Mbeya, likiwemo la Mbeya Mjini.

Akizungumza jana kwa simu na Tanzania Daima, Mbilinyi alisema anamshangaa Mulugo kwa kauli hiyo wakati akiwa na hali mbaya kisiasa jimboni kwake Songwe, kiasi cha walimu kulalamika kukosa hata chaki shuleni.

“Mimi Mulugo hanitishi hata kidogo maana mambo yake yote ni ya kuungaunga, kuanzia elimu yake hadi siasa jimboni. Huyu nimesoma naye Sekondari ya Mbeya Day nikiwa namtangulia, na jina lake alikuwa akiitwa Amim si hili la Philip Mulugo,” alisema.

Mbilinyi aliongeza kuwa amefanya ziara jimboni kwa Mulugo na kuelezwa matatizo mengi yanayowakabili wapiga kura wake, na kwamba alishangazwa na hatua ya kuona walimu wakilalamika kukosa chaki wakati mbunge wao ni naibu waziri wa elimu.

“Haya mambo hatuyasemi kwa sababu ya kuwachukia CCM, bali wanatuletea wenyewe malalamiko wakitaka tuwasaidie kusema. Sasa Mulugo kashindwa kwake anakuja Mbeya Mjini kujitapa kuwa wataning’oa,” alisema.
Aliongeza kuwa, kutokana na ubabaishaji wa Mulugo, kuanzia sasa ataanza kumuita jina lake halali la Amim ili watu wafahamu kuwa hata kweli elimu aliunga licha ya kuteuliwa kuwa naibu waziri.

“Kila mtu anakuwa na ndoto, haikataliwi, hata yeye alipotoka hadi kuwa Naibu Waziri wa Elimu ni ndoto pia, hakutegemea kutokana na kusoma kwa kuungaunga kwa kutumia jina na cheti cha mtu, hakuwa na uwezo,” alisema.

Mbilinyi alifafanua kuwa Mulugo amemchokoza mwenyewe na kumtaka atambue kuwa yeye si wa kuchezea wala chama chake cha CHADEMA, na kwamba chama hicho chini yake au mtu mwingine kuliacha Jimbo la Mbeya Mjini ni baada ya miaka 25 ijayo.

Alisema kutokana na kupendwa na watu na kuwapa changamoto katika halmashauri licha ya kwamba CCM wana madiwani 22 na CHADEMA 14, anaamini kabisa kwa sasa atajipanga kugombea umeya badala ya ubunge.

“Yaani Mulugo amechemsha, hakuna namna ya kumtoa Sugu wala chama chake, na sasa itafika wakati nitakuwa meya, tena pale ndio wamechemsha kabisa kumweka mwenyekiti asiyekubalika, na sasa wakifanya mikutano yao hawapati watu.

“Mulugo ndiyo maana hata historia ya nchi haijui kwa kuwa elimu yake yenyewe ina utata, aanze kuchunguzwa, mtaniambia kafanya jambo la ajabu sana, mwenzake alifaulu, lakini kutokana na kutokuwa na uwezo wa kuendelea na shule yeye akanunua jina lake,” alisema.

Mbilinyi alisema kama Mulugo anahitaji kuendelea na siasa, basi aende Mbeya Mjini ili wamfundishe jinsi ya kuishi na watu jimboni kwake na kujua kero zao.

Hata hivyo, Mulugo alipotafutwa kufafanua madai hayo, alikwepa kulisemea sakata la kutumia jina lingine wakati akisoma sekondari, akisema kuna vitu ni stori, lakini fitina hizo za kisiasa ni majungu ya mtu na mtu.

Aliongeza kuwa, Mbilinyi aliwahi kwenda jimboni kwake Songwe na kusema madai hayo pamoja na kumtukana, lakini wananchi walimzomea wakisema wao ndio wanamfahamu mbunge wao kuanzia elimu ya msingi mpaka shahada.
“Matusi yale yalisababisha vurugu mpaka CHADEMA wakapata kura 19 dhidi ya kura 365 za CCM. Nilichokisema kwenye mkutano wa Mbeya ni jambo la kawaida kwa mwanasiasa yeyote aliye makini, tena mjumbe wa NEC.

“Nilisema majimbo yote ya CHADEMA Mkoa wa Mbeya tutayarudisha. Sasa kwani mbona wao kila siku wanasema watachukua majimbo yote ya Mkoa wa Mbeya?” alisema Mulugo kupitia ujumbe mfupi wa sms.

No comments:

Post a Comment