To Chat with me click here

Tuesday, September 4, 2012

LHRC KUISHITAKI POLISI ICC


Dr. Hellen Kijo Bisimba
Kituo cha Sheria na Haki za Binadamu (LHRC) kimesema kinajiandaa kulishitaki Jeshi la Polisi katika Mahakama ya Kimataifa ya Makosa ya Jinai (ICC) iliyopo The Hague, nchini Uholanzi.

Akizungumza na Tanzania Daima jana, Mkurugenzi wa kituo hicho, Hellen Kijo-Bisimba, alisema wamefikia hatua hiyo baada ya kuchoshwa na matukio ya mauaji yanayofanywa na polisi.

“Umefika mwisho wa kutoa matamko juu ya matukio ya aina hii. Tunaona ni vema kuyashughulikia kimataifa zaidi,” alisema.

Alisema katika kikao walichoketi jana walikuwa wakitafakari kuliburuza Jeshi la Polisi nchini mahakamani, lakini wameona hiyo haitasaidia kwa kuwa hadi sasa wana takriban kesi 17 walizofungua zenye kufanana matukio na zimekuwa zikipigwa kalenda kila uchwao.

“Tanzania ni mojawapo ya nchi mwanachama katika Fungamano la Haki za Binadamu Afrika, tutaangalia namna gani ya kuzungumza na Umoja wa Mataifa, ili tuone hatua zaidi zikichukuliwe,” alisema.

Kwa mujibu wa Kijo-Bisimba hali ya kukataza watu kufanya mijumuiko si haki ilimradi tu hawavunji sheria na kuhoji iweje hao wakamatwe wakati wengine wamezindua kampeni Bububu?

Alieleza walitegemea polisi wapo kwa ajili ya usalama wa raia, lakini kwa sasa hali imebadilika na hata raia nao wameanza kutokuwa na imani nao.

MCT, wahariri kutoa tamko
Katibu Mkuu wa MCT, Kajubi Mkajanga, alisema: “Kwa maana hii inatutaka wananchi na waandishi tuamini kuwa vitendo vya mauaji vinavyoendelea mikononi mwa vyombo vya dola hasa kwenye mikutano ya vyama vya sisa ni hatari na tusishiriki kutimiza wajibu wetu kikatiba.”

Mukajanga aliwataka waandishi wa habari kuchimbua na kuandika habari za kina hususan za kuuawa kwa Mwangosi, kwani kuna tofauti ya maelezo ya Kamanda wa Polisi wa Mkoa wa Iringa na Waziri wa Mambo ya Ndani, John Nchimbi.

“Jana nilipoongea na Waziri Nchimbi ambaye yupo safarini kuelekea Durban alisema taarifa alizopewa 'marehemu alilipukiwa na bomu la machozi ambalo halikulipuka kitaalamu’. Kamanda Kamuhanda asubuhi jana alisema kuna kitu kizito kilirushwa ama kuwadhuru polisi ama Mwangosi, hii ni ajabu isiyotakiwa kufumbiwa macho,” alisema Mukajanga na kuongeza kuwa kinachohitajika ni uchunguzi wa kina ili kupata ukweli.

Jukwaa la Wahariri lilisema dalili zote zinaonesha kuwa polisi wanahusika kwa namna moja, kwani kitendo cha kumzingira mtu na kumshambulia kinathibitisha kwamba hawakuwa na nia njema hata kidogo dhidi ya mwandishi huyu.

Katibu Mkuu wa TEF, Neville Meena, alisisitiza: “Kila mauaji yakitokea kumekuwa na visingizio vya watu kuuawa na vitu vizito, siku nyingine watauawa watu 100 tutaambiwa kulikuwa na vitu vizito...Tanzania ya leo si ya mwaka 1961 ambapo taarifa ilihitaji zaidi ya siku kuipata, leo tukio linatokea na muda huohuo watu wanapata taarifa,” alisema.

Akibainisha baadhi ya mambo yanayotia shaka katika tukio la mauaji ya mwandishi Mwangosi, Meena alitoa mfano wa picha zilizotolewa kwenye baadhi ya magazeti na majibizano baina ya Kamanda Kamuhanda na waandishi hususan Mwangosi kwenye mkutano na waandishi kuwa ni dhahiri kulikuwa na agenda ya siri nyuma ya pazia katika mauaji hayo.

“Kwa upande wetu tunasubiri taarifa ya muungano wa vyama vya waandishi wa habari nchini UTPC tutakapokutana tutaungana na makubaliano na uamuzi wa vyama vya waandishi nchini na duniani dhidi ya serikali na vyombo vya habari...tusubiri nadhani kesho au kesho kutwa tutawaambia,” alisema.

No comments:

Post a Comment