To Chat with me click here

Tuesday, September 4, 2012

POLISI YAJITETEA


Ndg. Paul Chagonja
Mkurugenzi wa Operesheni wa Jeshi la Polisi, Paul Chagonja, amesema jeshi hilo halina bomu lililotumika kumuua mwandishi huyo.

Akizungumza katika kituo cha radio cha Magic FM jijini Dar es Salaam, Chagonja, aliwataka wananchi kuwa watulivu wakati jeshi hilo likifanya uchunguzi wa kifo hicho.

Alisema timu itakayofanya uchunguzi itaongozwa na Mkuu wa Jeshi la Polisi (IGP), Said Mwema pamoja na Mkurugenzi wa Makosa ya Jinai (DCI), Robert Manumba na maofisa wengine wa jeshi hilo.

“Tunawaomba wananchi wa Iringa wawe watulivu wakati Jeshi la Polisi likifanya uchunguzi wa tukio hili,” alisema Chagonja.

Pamoja na hayo, alivitaka vyama vya siasa kutii sheria zilizowekwa katika kufanya maandamano, ili kudumisha amani nchini.

Kwa upande wake, Mchungaji na Mwalimu wa neno la Mungu katika Kanisa la Evangelist Asembless of God (EAGT) Jimbo la Dodoma Magharaibi, Emanuel Msengi, amekemea tabia ya Jeshi la Polisi kutumia nguvu na silaha za moto na kusababisha vifo vya watu wasiokuwa na hatia.

“Sasa taifa linaanza kupoteza mwelekeo, kwani inaonesha wazi kuwa nguvu ya Mungu imetoweka katika taifa na roho ya mauaji kwa watu wasiokuwa na hatia inatawala,” alisema.

Kuhusu kuunda tume ya kuchunguza mauaji hayo, alisema ni matumizi mabaya ya fedha za walipakodi, kwani inaonesha wazi kuwa waliohusika ni askari wa Jeshi la Polisi na hakuna sababu yoyote ya kuunda tume.

MAONI YA WADAU MBALIMBALI
Watu wa kada mbalimbali wamelaani tukio la mauaji ya mwandishi wa habari wa Televisheni ya Channel Ten, Daudi Mwangosi.

Akizungumza katika ofisi za Tanzania Daima, Sifa Majura, alieleza kushangazwa na kitendo cha kikatili kinachodaiwa kufanywa na jeshi hilo.

Alisema ni uonevu uliopitiliza, askari polisi kwa makusudi kukatisha uhai wa mwandishi huyo aliyekuwa akitimiza majukumu yake.

“Uko wapi utawala bora tunaouhubiri kila mara…hakuna bali kinachofanyika ni kuudanganya ulimwengu, ili tuendelee kupata fedha za wahisani hao,” alisema.

Alihoji kuwa ni kitu gani cha dhambi alichotenda mwanahabari huyo hadi jeshi hilo lifikie hatua ya kutenda unyama wa aina hiyo.

Aliutaka umma wa Watanzania kuamka na kuacha kukaa kimya, ili kupinga unyama huo ambao hauvumiliki.

Huku akiifananisha nchi ya Marekani alisema pamoja na kuwa na maadui wengi lakini katika mikusanyiko na maandamano ya raia polisi wake hawaendi na risasi za moto.

“Nashangaa hapa nchini Jeshi la Polisi ni wapi wanataka kutupeleka…wenzetu kule pamoja na vurugu lakini hawabebi risasi za moto zaidi ya virungu na mabomu ya machozi,” alisema.

Naye, Mchungaji wa Kanisa la Pentekoste Mbeya, William Mwamalanga, alisema Jeshi la Polisi linapoteza dira kwa kuwa linashindwa kulinda raia na sasa limegeuka kuwa la kiuaji.

Alisema hatua hiyo inajenga chuki miongoni mwa jamii, kwani jeshi hilo linaonesha wazi kuwa linatumiwa na vyama vya siasa.

Alisema hali iliyoanza kujionesha sasa hivi kuna hatari kubwa kuja kuibuka wakati wa uchaguzi mkuu wa mwaka 2015. Mwamalanga, aliwataka viongozi wa jeshi hilo kukubali kuwajibika na kujiuzulu kutokana na kushindwa kazi.

“Katika muda mfupi tu mauaji yanaibuka kila mahali, nadhani wakati umefika wa viongozi wakuu wa jeshi hilo kukubali kujiuzulu bila shuruti,” alisema.

Naye Mkurugenzi Mtendaji wa asasi inayojihusisha na masuala ya afya ya Sikika, Irenei Kiria, amelaani kitendo hicho na kusema ana matumaini waliohusika katika mauaji hayo watachukuliwa hatua kwa kufikishwa katika vyombo vya dola, ili sheria ichukue mkondo wake.

Naye Mkurugenzi Mtendaji wa Mtandao wa Jinsia nchini (TGNP), Ussu Mallya, alisema, kitendo kilichofanywa ni cha kusikitisha, kuhuzunisha na kushangaza kwa kuwa, polisi sasa wameacha kufanya kazi yao ya kulinda raia na kufanya mauaji.

“Msingi wa polisi wa kulinda raia unaanza kuporomoka, ni vitendo vinavyozidi kuendelea bila kuchukuliwa hatua madhubuti ya kuvikomesha raia wengi watapoteza maisha,” alisema.

Alisema anapouawa mwanahabari ambaye amejitolea kuhabarisha wananchi hicho ni kitendo cha kutisha waandishi wengine na kuwanyamazisha washindwe kufanya kazi zao kwa uhuru.

Alisema wanaohusika wafanyiwe uchunguzi kwa kuwa vitendo hivi visipodhibitiwa vitazidisha vurugu.

No comments:

Post a Comment