To Chat with me click here

Monday, May 14, 2012

Uchaguzi wa Arumeru kuitikisa Kamati Kuu ya CCM

 Hali ya kisiasa nchini ambayo inajumuisha chaguzi mbalimbali zilizofanyika ukiwemo ule wa Arumeru Mashariki ambao Chama cha Mapinduzi (CCM) kilipoteza jimbo, ni miongoni mwa mambo ambayo yanatarajiwa kuvitikisa vikao vya Kamati Kuu, (CC) na Halmashauri Kuu ya chama hicho.
Katika uchaguzi huo ambao ulifanyika baada ya mbunge wake Jeremia Sumari kufariki dunia, mgombea wa Chama cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema), Joshua Nassari aliibuka kidedea.
Kwa mujibu wa Katibu wa Itikadi na Uenezi, Nape Nnauye, jumla ya agenda 14 zitajadiliwa katika kikao hicho ambacho kilianza jioni jana.
Alisema hali ya kisiasa nchini ni miongoni mwa agenda ambazo zitakazojadiliwa katika kikao hicho.
Hata hivyo, alisema wanakusudia kuifanya agenda ya pekee ya hali ya uchumi ambayo kwa sasa huingizwa katika hali ya kisiasa. “Si mnafahamu kwamba hapa katikati kumefanyika chaguzi nyingi, zikiwemo za ndani ya chama ni miongoni mwa mambo tutakayojadili,”alisema Nape.
Alisema uchaguzi katika mashina na baadhi ya matawi umeshafanyika na kwamba watapokea taarifa ya maendeleo ya chaguzi hizo ili kama kuna jambo la kushauri wafanye hivyo.
Nape alisema agenda nyingine itakuwa itokanayo na vikao vilivyopita, taarifa mbalimbali na uchaguzi wa kujaza nafasi za makatibu wa mikoa.
Aliitaja baadhi ya mikoa hiyo kuwa ni Iringa na Dodoma.
Hadi tunakwenda mtamboni kikao cha Kamati Kuu kilikuwa kikiendelea baada ya kikao cha kamati ya maadili kilichokuwa kianze saa 4.00 asubuhi kuanza saa 7.30 na kumalizika saa 11.00 jioni.

No comments:

Post a Comment