To Chat with me click here

Tuesday, July 31, 2012

CHADEMA: ZITTO ACHUNGUZWE


LISSU ATAJA WABUNGE WALA RUSHWA
 
KAMBI rasmi ya Upinzani Bungeni imetaka kuchunguzwa kwa madai ya Naibu Kiongozi wa wa kambi hiyo, Zitto Kabwe, kuhongwa.
Kambi hiyo pia imetaja majina ya wabunge sita wa Chama Cha Mapinduzi (CCM), waliokuwa wajumbe wa Kamati ya Nishati na Madini iliyovunjwa na Spika wa Bunge, Anne Makinda, mwishoni mwa wiki, ikidai kuwa kwa namna moja ama nyingine walihusika na vitendo vya rushwa.

Wabunge hao wanatuhumiwa kupokea rushwa kutoka kwa kampuni za mafuta ili kuipigia debe menejimenti ya Shirika la Ugavi wa umeme nchini (TANESCO).
Akizungumza jana na waandishi wa habari mjini hapa, Mnadhimu Mkuu wa kambi hiyo, Tundu Lissu, alisema wamesikia tuhuma nyingi dhidi ya Zitto lakini hawajamhoji kiongozi huyo.

Alisema wanaviomba vyombo vinavyohusika vimchunguze Zitto ili ukweli ujulikane na hatua zinazostahili zichukuliwe kama atathibitika kuwa na makosa. “Chama hatujakaa na Zitto kumsikiliza lakini tunataka achunguzwe, hatuna masilahi yoyote katika uchafu huu wa rushwa. “Uchunguzi huu utatupa msingi wa kumchukulia hatua kama chama ikiwa itathibitika amehongwa,” alisema.

Alibainisha kuwa, mbunge wao huyo amekuwa akihusishwa na kumtumia ujumbe mfupi wa vitisho Katibu Mkuu wa Nishati na Madini, Eliakimu Maswi.
Alisema ni vema Zitto achunguzwe na apewe nafasi ya kujieleza kama itakavyokuwa kwa wengine kuliko kuendelea kusambaza maneno ya kufikirika.

CHAMA CHA MAPINDUZI (CCM) CHAMJIBU LISSU


 *Yadai orodha ya Lissu inalenga kupotosha tuhuma za rushwa zinazowakabili baadhi ya wabunge *Anataka kuwaokoa wa Chadema katika sakata hilo.
*Yasema tuhuma za rushwa kwa wabunge lisigeuzwe suala la kisiasa Nape akizungumza na waandishi wa habari leo DAR ES SALAAM, TANZANIA

Chama Cha Mapinduzi (CCM) kimesema kinalaani juhudi zinazofanywa na baadhi ya wana siasa na vyama vya siasa kujaribu kupotosha na kuuficha ukweli juu ya tuhuma za rushwa zinazowakabili baadhi ya wabunge.

Akizungumza na waandishi a habari leo mjini Dar es Salaam, Katibu wa Halmashauri Kuu ya Taifa, ya CCM, Itikadi na Uenezi Nape Nnauye alisema, zipo juhudi za baadhi ya wanasiasa na vyama vya siasa kujaribu kulifanya suala la tuhuma za rushwa kwa baadhi ya wabunge kuwa la kisiasa kwa malengo yao.

"Mfano mzuri wa juhudi hizi ni kitendo cha Tundu Lissu, ambaye ni mbunge wa Chadema na Mnadhimu Mkuu wa Kkambi ya upinzani Bungeni cha kutoa aliyoiita orodha ya wabunge wanaotuhumiwa kufanya biashara na TANESCO na kwamba ndio watuhumiwa wa rushwa inayozungumziwa", Alisema Nape na kuongeza;
"Cha kushangaza orodha yake ilikuwa na wabunge wa CCM peke yake wakati wote tunajua kuwa yapo majina ya baadhi ya wabunge wa vyama vingine hasa Chadema, yanayotajwa katika orodha ya wabunge wanaotuhumiwa kwa rushwa hii".

Nape alisema juhudi hizo za Lissu na wenzake zinalengo la kuuficha ukweli na kujaribu kuwalinda watuhumiwa wa uhalifu wanaotokana na Chadema.
"Tunamtaka Lissu na wengine wanaofanya juhudi hizo kuacha mara moja, na badala yake tuvipe nafasi vyombo vinavyohusika vichunguze na matokeo ya uchunguzi huo yatangazwe hadharani ili tuwajue wabunge waliotusaliti", alisena Nape.

Alisema CCM inalaani vitendo vya rushwa hasa vinapohusishwa na viongozi ambao wanapaswa kuwa mfano wa kuigwa na kwamba rushwa ya namna hiyo inavuruga sana uchumi wa nchi, hivyo wanaohusika nayo haitoshi kuwaita wala rushwa tu bali ni zaidi ya wahujumu uchumi.

"Wakikithibitika ni muhimu hatua kali zichukuliwe kulikomesha kabisa hili na iwe fundisho kwa wengine", alisema Nape.

Nape alisema CCM inawapongeza watendaji wakuu wa Wizara ya Nishati na Madini wakiongozwa na Waziri wao Prof. Sospeter Muhongo, Manaibu wake, Massele na Simbachawene na Katibu Mkuu, Maswi kwa uzalendo, ujasiri na umahiri wao mkubwa waliouonyesha kwa muda mfupi waliokaa kwenye wizara hiyo.
"Tunaamini uzalendo walioonyesha katika kusimamia wizara hii,utaigwa na watumishi wengine wa umma katika kuhakikisha matumizi mazuri ya rasilimali za nchi zinalindwa ili kuhakikisha maisha bora kwa kila Mtanzania yanatimia. Tunaunga mkono jitihada zao", alisema Nape.

Alisema, pia CCM inalipongeza bunge kwa kuendelea kusimamia serikali na rasilimali za nchi katika kuhakikisha nchi inapiga hatua kubwa ya maendeleo.

"Tunawaomba waheshimiwa wabunge wazidi kutanguliza masilahi ya taifa mbele na uzalendo mkubwa katika shughuli zao za kila siku", alimalizia.

MKOBA AKIONYESHA FOMU YA VITISHO ILIYOTOLEWA NA SERIKALI DHIDI YA WALIMU ILI WASITISHE MGOMO!

MKOBA AKIONYESHA FOMU YA VITISHO ILIYOTOLEWA NA SERIKALI DHIDI YA WALIMU ILI WASITISHE MGOMO LAKIN MKOBA KASEMA MGOMO UMEANZA LEO NAWALIM WASIOGOPE MPAKA KIELEWEKE.

WALIMU HAWAPO DARASANI WATOTO FULL KUCHEZA! 

 MGOMO WA WALIMU RUANGWA-LINDI hali ni tete watoto full kucheza,hakuna waalimu madarasani.

Monday, July 30, 2012

RAIS KIKWETE AFUTURU NA VIONGOZI WA MADHEHEBU MBALIMBALI YA DINI IKULU JIJINI DAR ES SALAAM

Baadhi ya viongozi na wawakilishi wa madhehebu mbalimbali ya dini wakishiriki katika futari aliyoiandaa Rais Jakaya Kikwete kwa viongozi wa dini ikulu jijini Dar es Salaam jana jioni.

RAIS KIKWETE AHUDHURIA MAZISHI YA SHEMEJI YAKE MJINI LINDI LEO


Rais Jakaya Mrisho Kikwete leo amehudhuria mazishi ya shemeji yake, Marehemu Amani Kinyozi (45), aliyefariki Jumamosi iliyopita jijini Dar es salaam, na kuzikwa katika makaburi ya Mitandi mjini Lindi.Pichani ni Rais Kikwete akishiriki katika swala ya kumuombea marehemu mjini Lindi leo.

Rais Kikwete akiweka udongo kaburini wakati wa mazishi ya shemeji yake, Marehemu Amani Kinyozi, katika makaburi ya Mitandi mjini Lindi leo Julai 30, 2012. PICHA NA IKULU.

SERIKALI YALIFUNGIA GAZETI LA MWANAHALISI

TAMKO LA SERIKALI LA KULIFUNGIA GAZETI LA MWANAHALISI


Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania imelifungia kutochapishwa gazeti la MwanaHalisi kuanzia 30 Julai, 2012 kwa muda usiojulikana kutokana na mwenendo wake wa kuandika habari na makala za uchochezi, uhasama na uzushi likiwa na nia ya kusababisha wananchi kukosa imani na vyombo vya dola hali inayoweza kuhatarisha amani na mshikamano uliopo nchini.

Katika matoleo yake hivi karibuni, gazeti la MwanaHalisi toleo Na. 302 la Jumatano Julai, 11 – 18, 2012 na toleo Na. 303 la Jumatano Julai 18 – 24, 2012 na toleo Na. 304 la Jumatano Julai 25 hadi 01 Agosti, 2012 na mengine yaliyotangulia yamekuwa yakichapisha habari na makala zenye kueneza na kujenga hofu kwa jamii. Mhariri wa gazeti la MwanaHalisi, ameitwa na kuonywa mara nyingi, lakini hataki kukiri kuwa maudhui ya makala zake hazina tija kwa jamii, pia hazifuati weledi na maadili ya taaluma ya uandishi wa habari.

Mhariri, mara zote katika utetezi wake amekuwa akinukuu kifungu cha 18 cha Katiba ya nchi yetu ambacho kinatoa uhuru wa kutoa maoni na kwa makusudi kutonukuu kifungu cha 30 cha Katiba hiyo kinachoweka ukomo wa uhuru.

Uamuzi wa Serikali 
Serikali imeamua kulifungia kutochapishwa kwa muda usiojulikana gazeti la MwanaHalisi, kwa mujibu wa Sheria ya Magazeti ya mwaka 1976, kifungu Na. (25) (i), adhabu hiyo itaanza tarehe 30 Julai, 2012 kwa mujibu wa Tangazo la Serikali (Government Notice) Na. 258 lililochapishwa katika Gazeti la Serikali na kutolewa jijini Dar Es Salaam tarehe 27 Julai, 2012.
Serikali inawataka wamiliki, wahariri na wanahabari kuzingatia sheria, uzalendo, weledi na maadili ya taaluma ya uandishi wa habari katika kutekeleza wajibu wa kuhabarisha, kuelimisha na kutoa burudani kwa wananchi.

Kama ilivyoelezwa Bungeni wakati wa kuwasilisha Bajeti ya Wizara ya Habari, Vijana, Utamaduni na Michezo hivi karibuni waandishi na watangazaji wa habari wanatakiwa kuhakikisha kuwa habari wanazoziandika na vipindi wanavyoandaa vinazingatia taaluma na kuweka mbele maslahi ya Taifa letu na uzalendo. Uhuru na haki ya vyombo vya habari uendane na wajibu.

Kuanzia sasa Serikali haitasita kuchukua hatua dhidi ya vyombo vya habari ambavyo kwa maksudi vitatoa taarifa za uchochezi ambazo zitahatarisha hali ya amani na utulivu uliopo nchini mwetu.

Imetolewa na:
OFISI YA MSAJILI WA MAGAZETI WIZARA YA HABARI, VIJANA, UTAMADUNI NA MICHEZO
30 Julai, 2012  


CCM, CHADEMA WAWATANGAZIA KIAMA WABUNGE MAFISADI

 VYAMA vya CCM na Chadema vimetoa onyo kali kwa wabunge wanaotuhumiwa kwa kashfa ya kuhongwa na baadhi ya kampuni za mafuta na kulihujumu Shirika la Umeme Tanzania (Tanesco), vikisema havitasita kuwawajibisha pindi tuhuma hizo zitakapothibitika.

Kauli ya vyama hivyo imekuja siku moja baada ya wabunge watano, watatu wa CCM na wawili wa upinzani kudaiwa kuhusika na vitendo hivyo vya rushwa, ambavyo vimesababisha Spika wa Bunge, Anne Makinda kuivunja Kamati ya Bunge ya Nishati na Madini na kuagiza uchunguzi wa kina ufanyike ili majina ya wahusika yawekwe hadharani.
Wakizungumza kwa nyakati tofauti jana, viongozi wa juu wa vyama hivyo walisema wanasubiri kwa hamu taarifa rasmi kutoka bungeni.

CCM: Rushwa adui wa haki
Makamu Mwenyekiti wa CCM Bara, Pius Msekwa alisema chama hicho kimewaapiza wanachama wake wote kutotoa wala kupokea rushwa.
Alisema rushwa ni kosa la jinai hivyo anaamini vyombo husika vya dola vitachukua hatua zinazofaa kwa mujibu wa sheria za nchi.

RUSHWA BUNGENI MOTO - MBATIA SASA ATISHIA KUWATAJA WAKATI WOWOTE


SAKATA la wabunge kuhongwa kwa nia ya kuyatetea makampuni ya mafuta na menejimenti ya Shirika la Ugavi wa Umeme Nchini (TANESCO) linazidi kuchukua sura mpya kadiri siku zinavyosonga mbele.

Siku moja baada ya Waziri wa Nishati na Madini, Profesa Sospeter Muhongo, kuvurumisha makombora dhidi ya wabunge hao pasipo kuwataja kwa majina, Mbunge wa Kuteuliwa, James Mbatia, ameibuka na jipya kuhusu sekeseke hilo.
Mbatia ambaye pia ni Mwenyekiti wa Taifa wa Chama cha NCCR-Mageuzi amesema wakati wowote kuanzia sasa atawataja kwa majina wabunge wote waliopokea rushwa kwa lengo la kuwalinda viongozi wakuu wa TANESCO wanaokabiliwa na tuhuma za kulihujumu shirika hilo.

Mbali ya hilo, Mbatia amemshutumu Spika wa Bunge, Anne Makinda, kwa kuwalinda wabunge hao aliodai wamehongwa na mafisadi hao wa TANESCO.
Kauli hiyo aliitoa jana mkoani hapa alipokuwa akizungumza na waandishi wa habari kuhusu uamuzi wa Spika Makinda kuridhia kuivunja Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Nishati na Madini na kuiagiza Kamati ya Maadili, Haki na Madaraka ya Bunge kuwachunguza watuhumiwa.
Mbatia alisema Spika anao ushahidi wa kutosha wa majina ya wabunge waliohongwa kwani Waziri wa Nishati na Madini, Profesa Sospeter Muhongo, aliliambia Bunge kuwa wana ushahidi wote.
Alibainisha kuwa ushahidi huo ndiyo uliomfanya Spika Makinda akaridhia kuivunja kamati husika na kuipa kazi Kamati ya Maadili, Haki na Madaraka ya Bunge kuwachunguza watuhumiwa.

Kiongozi huyo pia alisema hawana imani na kamati iliyopewa jukumu la kuwachunguza wabunge watuhumiwa wa rushwa kwa sababu inaundwa na baadhi ya watuhumiwa.
“Tunamtaka Spika ajitakase kwanza kwa kuwaengua wajumbe ambao ni watuhumiwa, kinyume na hapo hatuna imani na kamati hiyo,” alisema.

Alisema Bunge ni chombo kitukufu na ili utukufu huo uonekane ni lazima maamuzi yanayofanywa huko yaheshimiwe, hivyo akapendekeza kuwa mbali na Bunge kutumia kanuni zake kuwahukumu wabunge watuhumiwa au linaweza kuiga maamuzi ya baadhi ya mabunge ya Jumuiya ya Madola.

Alitolea mfano mabunge ya Uingereza na India, ambapo Bunge la Uingereza limewahi kuwatimua na kuwavua ubunge wabunge 57 na India imefanya hivyo kwa wabunge 11 kutokana na kujihusisha na vitendo vya rushwa.
“Hivyo basi tunatoa wito kuwa mbunge yeyote wa chama chochote anayeamini kwa dhamira yake kwamba ni mjumbe wa Kamati ya Nishati na Madini na anafanya biashara na TANESCO kwa njia ya maslahi binafsi halafu anatumia rushwa kuwashawishi wabunge wengine au amepokea rushwa kutetea uovu ni bora akajiondoa mwenyewe kwenye ubunge kabla ya kuabishwa na Bunge,” alisema.

Mbatia aliongeza kuwa wanamtaka Spika awe amewataja kwa majina wabunge waliopokea rushwa si zaidi ya wiki moja ili Bunge liwachukulie hatua, huku akiwaomba wabunge wenzake bila kujali itikadi za vyama vyao wafanye azimio la Bunge ili wahusika mbali na kuvuliwa ubunge wafungwe jela miaka mitano.
“Kwa mujibu wa sheria namba 3 kifungu cha 32 ya Haki, Kinga na Madaraka ya Bunge ya mwaka 1988, mbunge anakatazwa kuzungumza, kuhoji, kupiga kura au kutetea jambo lolote bungeni ambalo litakuwa na ushawishi wa maslahi yake binafsi kutoka nje na kwamba adhabu yake ni kifungo kisichopungua miaka mitano jela,” alisema Mbatia.

Mwenyekiti huyo ambaye alifuatana na mbunge mwingine wa chama hicho wa Kasulu Mjini, Moses Machali, alimtaka Spika kuzitaja kamati nyingine ambazo wajumbe wake wanatuhumiwa kwa rushwa.
Mbali na Kamati ya Nishati na Madini iliyovunjwa, kamati nyingine zinazodaiwa baadhi ya wabunge wake kujihusisha na vitendo vya rushwa ni ile ya Hesabu za Mashirika ya Umma (POAC) chini ya Zitto Kabwe na Hesabu za Serikali za Mitaa (LAAC) inayoongozwa na Augustine Mrema.

Nyingine ni ya Miundombinu chini ya Peter Serukamba, Viwanda na Biashara ya Mahmoud Mgimwa na Ardhi, Maliasili na Mazingira chini ya James Lembeli.
“Tatizo la nchi yetu ni kuchelewa kufanya maamuzi wakati muafaka. Tukilitakasa Bunge kwa kuwashughulikia wabunge waliokula rushwa ni wazi hata serikali itaanza kuwachukulia hatua wale ambao tumekuwa tukiwalalamikia kujihusisha na rushwa,”
Mbatia aliwatahadharisha wabunge wa chama chake kuwa kama kuna yeyote aliyechukua rushwa katika sakata hilo, ajiengue mapema.

Mbatia pia alitumia mwanya huo kuwatia matumaini wabunge waadilifu wenye misimamo mikali ya kuikosoa serikali kuwa wasiogopeshwe na sakata hilo ambalo alidai serikali italitumia kuwanyamazisha wabunge kwa vile walikuwa wakiikosoa.
Ingawa Mbatia hakuwataja kwa majina wabunge hao, habari ambazo Tanzania Daima inazo zinaeleza kuwa wabunge zaidi ya sita wanatajwa kuwa katika kundi la wale wanaotuhumiwa kuwatetea mafisadi wa TANESCO.

Inadaiwa wabunge hao walipewa fedha na kampuni za mafuta ili washinikize kung’olewa kwa Waziri wa Nishati na Madini pamoja na Katibu Mkuu wa Wizara hiyo Eliakim Maswi wanaodaiwa kuipa zabuni ya kusambaza mafuta kwa TANESCO kampuni ya Puma Energy.
Habari zinaeleza kuwa, wabunge hao wako katika Kamati ya Hesabu za Mashirika ya Umma (POAC), Hesabu za Serikali za Mitaa (LAAC) Kamati ya Miundombinu, Kamati ya Viwanda na Biashara na Ardhi, Maliasili na Mazingira.

Vyanzo vya habari hili vimedokezwa kwamba wabunge takriban wote isipokuwa mmoja tu, walioko katika orodha hiyo wanatokana na Chama Cha Mapinduzi (CCM).