To Chat with me click here

Tuesday, July 17, 2012

HUDUMA YA “FAST TRACK” MUHIMBILI YALALAMIKIWA



Huduma ya Fast Track kwa kina mama wajawazito katika hospitali ya Taifa Muhimbili imeingia dosari baada ya kulalamikiwa na wateja wake ambao ni wakina mama wajawazito kama ilivyoripotiwa na vyanzo vyetu vya habari.

Wakizungumza na mwandishi wetu, wakina mama hao ambao walifika hospitalini hapo tangu saa 12 asubuhi, wamesema kuwa tatizo kubwa ni rushwa na ubaguzi uliokithiri katika kutoa huduma hospitalini hapo kwa baadhi ya wauguzi wa zamu wa huduma hiyo. 

Akivielezea vyanzo vyetu vya habari hospitalini hapo, mama mmoja ambaye hakutaka jina lake litajwe alisema,  imekuwa ni desturi kwa wahudumu hao kuweka, kuzuia au kuficha namba za mwanzo za foleni za wakina mama kwa nia ya kuziuza namba hizo kwa wajawazito wengine ambao huchelewa kufika hospitalini hapo ingawa hupenda kutibiwa mapema au kuzificha kwa ajili ya ndugu na jamaa zao ambao huja baadaye sana. 

“Sisi tunajihimu kuamka asubuhi sana, na tunahakikisha saa 12 tuko hapa kuwahi foleni, lakini cha kushangaza, wahudumu wanafika saa 2 mpaka saa 3 asubuhi na kutukuta sisi tukiwa tumefika, ila tunapoitwa kwenda kupewa namba huwa tunapewa namba kuanzia 10 na kuendelea tena nazo hurukwa rukwa, kwa kweli hili hutushangaza sana”. 

Mama huyo amesema, tena bila aibu, watu hao ambao huuziwa nafasi hizo za kwanza hata kama wamechelewa, huja hospitali muda wanaotaka lakini wakitoa elfu mbili tuu, wao huwekwa wa kwanza, hivyo alihoji hii rushwa itaisha lini? Na mbona inafanyika peupe kabisa, ina maana vyombo husika havioni utovu huu wa nidhamu kimaadili ambao hutia aibu wauguzi na hospitali kwa ujumla wake? 

Baadhi ya wamama wengine wamesema huduma hiyo ya fast track ni ya malipo hivyo haileti mantiki kuona kuwa wote hulipa kiwango kile kile cha pesa (TZS. 20,000/= kwa anayeanza na TZS. 10,000/= kila unapokwenda kumuona daktari) lakini hubaguliwa kwa kuwa hawakutoa rushwa ya Tshs. 2000 kwa wauguzi. Na wao pia walohoji, je umuhimu au utofauti wa huduma hiyo na ile ya kliniki ya kawaida ni nini? Ikiwa mtu huja tangu alfajiri na kuondoka jioni tena kwa kunyanyapaliwa kiasi hicho?

Hivyo waliomba serikali na mamlaka husika kuingilia kati swala hili ili kukomesha rushwa za waziwazi hospitalini hapo.  Juhudi za kuutafuta utawala wa hospitali hiyo ili kutoa ufafanuzi juu ya jambo hili ziligonga mwamba baada ya wahusika kukataa kuliongelea jambo hili kwa waandishi wetu. 
 Moja kati ya wauguzi wa huduma ya Fast Track - Muhimbili akitoa huduma kama alivyokutwa leo asubuhi na wanahabari wetu.

Baadhi ya kina mama wakiwa kwenye foleni wakisubiri kumwona daktari kwa muda mrefu huku wakiwa na nyuso za masikitiko.

1 comment:

  1. Nakubaliana nawe 100%,mimi mwenyewe ni shuhuda,hao wanaokuja saa nne wanakuwa wa kwanza kuwaona madk,manesi na watu wa usafi wanakuwa wamewawekea namba,despite ya manesi hao kuja saa mbili,na watu tuliowahi tumefika saa 12 asubuhi,nilishawahi kuhoji kwa manesi nikaulizwa kwani wewe ni staff? Hao wanaokuja wamechelewa wengi ni ndugu zao,marafiki etc,na nilisha complain hii issue kwa dk akasema amejaribu kuingilia kati utaratibu akashindwa,tunaomba ieleweke maana ya first truck,first in,first out,unless ni emergency case

    ReplyDelete