Ikulu imesema kwamba mgomo wa Madaktari umeisha na walioamua kuendelea na kazi ya kutibu binadamu, wamerejea kazini.
Aidha,
 imesema kwamba sasa siyo wakati wa kulumbana tena, bali ni wakati wa 
kusonga mbele badala ya kurudi nyuma kwa sababu hakuna mgomo tena wa 
kujadiliwa.
Taarifa
 ya maandishi ya Kurugenzi ya Mawasiliano ya Rais, Ikulu ilieleza hayo 
jana baada ya kutakiwa kutoa kauli kuhusu ombi la baadhi ya viongozi wa 
dini kutaka Rais Kikwete akutane nao, wanaharakati na madaktari kujadili
 mgomo wa Madaktari.
Juzi,
 baadhi ya viongozi wa dini nchini waliingilia kati mgomo huo wa 
madaktari wakimwomba Rais Kikwete aitishe kikao nao ili kufanya 
mazungumzo yatakayowashirikisha madaktari na wanaharakati kwa lengo la 
kuondoa tatizo hilo.
Aidha,
 wametaka wanaharakati na wanasiasa waache kushabikia na kuchochea mgomo
 na badala yake washiriki kutafuta suluhu ya kweli kwa faida ya 
Watanzania wote.
Mambo ya msingi
Taarifa
 ya Mkurugenzi wa Mawasiliano ya Rais, Ikulu, Salvatory Rweyemamu kujibu
 swali aliloulizwa na gazeti la HABARI LEO kuhusu ombi hilo la viongozi 
wa dini, alisema mambo ya msingi kwa sasa ni manne.
“Kwamba
 mgomo wa madaktari umeisha na walioamua kuendelea na kazi hii muhimu 
sana ya kutibu binadamu wamerudi kazini. Hili ni jambo jema sana. Sasa 
siyo wakati wa kulumbana tena bali ni wakati wa kusonga mbele badala ya 
kurudi nyuma kwa sababu hakuna mgomo tena wa kujadiliwa.
“Kwamba tokea madaktari walipoanza kudai maslahi zaidi, Serikali ilifanya jitihada kubwa za kukutana na madaktari hao.
Mbali
 na Kamati ya Majadiliano ya Serikali, Madaktari pia wamekutana na Rais 
wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mheshimiwa Jakaya Mrisho Kikwete na 
Waziri Mkuu Mheshimiwa Mizengo Pinda. Kamwe, Serikali haijapata kukataa 
kukutana na viongozi wa madaktari,” alieleza Mkurugenzi huyo.
Alieleza
 kuwa mara ya mwisho madaktari hao walipoitwa kukutana na Waziri wa Afya
 na Ustawi wa Jamii, Dkt. Hussein Mwinyi walikataa wakidai kuwa Waziri 
hakuwa na jambo jipya la kuwaambia.
“Huu ni ushahidi mwingine kuwa kamwe Serikali haijapata kukataa kukutana na kuzungumza na madaktari,” alieleza. 
“Kwamba
 mara zote walipoomba kukutana na viongozi wa Serikali, akiwemo Rais, 
hawakupitia kwa mtu yeyote isipokuwa waliomba moja kwa moja na 
wakakubaliwa. Hivyo, hawana sababu ya kupitia kwa watu wengine kuomba 
kukutana na viongozi wa Serikali,” Mkurugenzi huyo aliutaja msingi 
mwingine.
Moja
 ya hoja za madaktari hao waliogoma ni kutaka kulipwa mshahara zaidi na 
Serikali na katika mapendekezo yao walitaka kulipwa Sh. milioni 3.5 kwa 
mwezi kwa daktari anayeanza kazi; kiwango ambacho ukijumuisha na madai 
mengine ya posho kinafikia Sh. milioni 7.7.
Rais
 Kikwete katika hotuba yake ya mwisho ya mwezi Juni, aliwaeleza 
madaktari hao kwamba Serikali haina uwezo wa kulipa kiwango hicho, na 
kwamba wako huru kutafuta mwajiri mwingine anayeweza kuwalipa, na hivyo 
hawana sababu ya kugoma.
“Kama
 daktari anaona kuwa hawezi kufanya kazi Serikalini bila ya kulipwa 
mshahara huo (Sh. milioni 7.7) awe huru kuacha kazi na kwenda kwa 
mwajiri anayeweza kumlipa kiasi hicho,” alisema Rais Kikwete.
Kutokana
 na ukweli huo, aliwatakia kila la heri wasioweza kufanya kazi 
serikalini, lakini akaongeza kuwa “hana sababu ya kugoma ili ashinikize 
kulipwa mshahara huo. Asisumbuke, hatalipwa mshahara huo.” “Isitoshe, 
hana sababu ya kuendelea kuwa na mgogoro na mwajiri ambaye hana uwezo wa
 kumlipa anachokitaka. Huna sababu ya kumpa usumbufu mwajiri wa 
kukuandikia barua ya kujieleza au kukuachisha kazi. Kwa nini upate 
usumbufu wa kupata barua hizo na kuzijibu. Kwa nini upate usumbufu wa 
kuachishwa kazi na kutakiwa kuondoka kwenye nyumba ya Serikali ndani ya 
saa 24?,” alihoji.
Rais
 Kikwete pia aliwaonya Madaktari hao kwa kuingia katika mgogoro na 
Mahakama ambayo iliwapa amri kurudi kazini wakaikataa na mgogoro 
mwingine na waajiri wao isivyostahili.

 
 
No comments:
Post a Comment