To Chat with me click here

Friday, July 27, 2012

MBATIA AFICHUA UFISADI WA KUTISHA TANESCO

Mwenyekiti wa NCCR-Mageuzi, James Mbatia, ameibua ufisadi mzito unaofanywa na TANESCO na kuwaomba wabunge wasimame kidete ili watuhumiwa wachuliwe hatua.
Mbatia ambaye pia ni mbunge wa kuteuliwa na Rais Kikwete, alifichua ufisadi huo mbele ya waandishi wa habari mjini hapa, akisema kuwa serikali imekuwa ikipoteza mabilioni ya fedha kulisaidia shirika hilo wakati zinaishia mikononi mwa wajanja ambao ni menejimenti na Bodi ya Wakurugenzi.

Tuhuma za Mbatia zinakuja ikiwa ni wiki mbili tangu Bodi ya Wakurugenzi ya TANESCO iwasimamishe kazi, Mkurugenzi Mtendaji wa Shirika hilo, William Mhando, na wenzake watatu kwa tuhuma za ubadhirifu na matumizi mabaya ya madaraka.
Mhando na Naibu Mkurugenzi Mtendaji wa TANESCO, Robert Shemhilu, Ofisa Mkuu wa Fedha, Lusekelo Kassanga, na Meneja Mwandamizi Ununuzi, Harun Matambo, walisimamishwa na bodi hiyo chini ya Mwenyekiti wake, Jenerali mstaafu, Robert Mboma, ili kupisha uchunguzi wa tuhuma dhidi yao.

Kwa mujibu wa Mbatia, wabunge wamekuwa wakifuatwa ndani na nje ya Bunge na hata kwenye mahoteli walikofikia wakishawishiwa kuiunga mkono TANESCO, jambo alilodai limewaingiza baadhi ya wenzao kwenye ufisadi.
Akifafanua kwa undani, Mbatia ambaye aliongozana na wabunge wote wa chama chake, alisema kuwa mpaka sasa hawana imani na Kamati ya Nishati na Madini kwa kuwa baadhi ya wajumbe wake vile vile ni wajumbe kwenye bodi ya TANESCO na wamekuwa wakitumika kuwarubuni wabunge wakingie kifua ufisadi.

“Tulipokwenda Ikulu kuonana na Rais Kikwete kama chama kuzungumzia mchakato wa Sheria ya Mabadiliko ya Katiba Januari 21 mwaka huu… tuligusia pia hali mbaya iliyokuwa ikiikabili TANESCO lakini Rais alitueleza kuwa serikali imeipa ruzuku ya sh bilioni 136 ili kuliwezesha,” alisema Mbatia.

Aliongeza kuwa kwenye bajeti ya mwaka jana, iliafikiwa kuwa TANESCO itafutiwe mkopo wa sh bilioni 408 na serikali pia ikalipa deni lake la sh bilioni 68 kwa shirika hilo pamoja na kulipatia mafuta ya sh bilioni 17.
Alisema kuwa mgogoro wa TANESCO ulianza kuibuka baada ya kuzushwa uongo kuwa nchi inaweza kuingia gizani wakati wowote kutokana na hali mbaya ya shirika, madai ambayo Mbatia alisema si ya kweli kwani ulikuwa ni ujanja wa mafisadi kuzima kwa makusudi mitambo.

“Kisha TANESCO iliingia kwenye mchakato wa kutafuta wazabuni wa kuiuzia mafuta mazito ya kuendesha mitambo yake ambapo ilifanya mazungumzo na kampuni tatu zilizoonyesha kuwa tayari kuiuzia mafuta hayo kwa sh 1,800 kwa lita,” alisema.
Katibu Mkuu wa Wizara ya Nishati na Madini, Eliakim Maswi, naye alifanya mazungumzo na Kampuni ya Puma ambako serikali ina hisa za asilimia 50 na kuafikiana kuwa inaweza kusambaza mafuta hayo kwa gharama ya sh 1,460 kwa lita, bei iliyoonekana kuwa na unafuu zaidi.

Mbatia alifafanua kuwa pamoja na kampuni ya Puma kutokuwa kwenye orodha ya zile zilizoomba zabuni hiyo, Maswi alitumia kanuni ya 42 (1) ya mamunuzi ya umma inayompa mamlaka ya kuamua vinginevyo kwenye masuala yenye maslahi ya umma kuipa zabuni hiyo hiyo.

“Kosa na kelele zote zimetoka hapo, mianya ya mafisadi imezibwa kwani walitaka kuzipa zabuni kampuni za bei kubwa ili wavune sh bilioni tatu ambazo zinaokolewa kila baada ya wiki mbili. Sasa kama kwa mwezi TANESCO inaokoa sh bilioni sita kwa nini tumnyime zabuni huyu?” alihoji.

Mbatia alisema kwa mwezi Mei pekee TANESCO ilikusanya sh bilioni 85 na matumizi yake kwa mwezi ni sh bilioni 11 ambapo kwa wastani wanapata zaidi ya sh bilioni 60 wakiwa na ziada ya sh bilioni 50 kila mwezi.

No comments:

Post a Comment