Mwenyekiti wa NCCR-Mageuzi, James Mbatia, ameibua ufisadi mzito 
unaofanywa na TANESCO na kuwaomba wabunge wasimame kidete  ili 
watuhumiwa wachuliwe hatua.
  Mbatia ambaye pia ni mbunge wa kuteuliwa na Rais Kikwete, alifichua 
ufisadi huo mbele ya waandishi wa habari mjini hapa, akisema kuwa 
serikali imekuwa ikipoteza mabilioni ya fedha kulisaidia shirika hilo 
wakati zinaishia mikononi mwa wajanja ambao ni menejimenti na Bodi ya 
Wakurugenzi.
  Tuhuma za Mbatia zinakuja ikiwa ni wiki mbili tangu Bodi ya 
Wakurugenzi ya TANESCO iwasimamishe kazi, Mkurugenzi Mtendaji wa Shirika
 hilo, William Mhando, na wenzake watatu kwa tuhuma za ubadhirifu na 
matumizi mabaya ya madaraka.
  Mhando na Naibu Mkurugenzi Mtendaji wa TANESCO, Robert Shemhilu, Ofisa
 Mkuu wa Fedha, Lusekelo Kassanga, na Meneja Mwandamizi Ununuzi, Harun 
Matambo, walisimamishwa na bodi hiyo chini ya Mwenyekiti wake, Jenerali 
mstaafu, Robert Mboma, ili kupisha uchunguzi wa tuhuma dhidi yao.
  Kwa mujibu wa Mbatia, wabunge wamekuwa wakifuatwa ndani na nje ya 
Bunge na hata kwenye mahoteli walikofikia wakishawishiwa kuiunga mkono 
TANESCO, jambo alilodai limewaingiza baadhi ya wenzao kwenye ufisadi.
  Akifafanua kwa undani, Mbatia ambaye aliongozana na wabunge wote wa 
chama chake, alisema kuwa mpaka sasa hawana imani na Kamati ya Nishati 
na Madini kwa kuwa baadhi ya wajumbe wake vile vile ni wajumbe kwenye 
bodi ya TANESCO na wamekuwa wakitumika kuwarubuni wabunge wakingie kifua
 ufisadi.
  “Tulipokwenda Ikulu kuonana na Rais Kikwete kama chama kuzungumzia 
mchakato wa Sheria ya Mabadiliko ya Katiba Januari 21 mwaka huu… 
tuligusia pia hali mbaya iliyokuwa ikiikabili TANESCO lakini Rais 
alitueleza kuwa serikali imeipa ruzuku ya sh bilioni 136 ili 
kuliwezesha,” alisema Mbatia.
  Aliongeza kuwa kwenye bajeti ya mwaka jana, iliafikiwa kuwa TANESCO 
itafutiwe mkopo wa sh bilioni 408 na serikali pia ikalipa deni lake la 
sh bilioni 68 kwa shirika hilo pamoja na kulipatia mafuta ya sh bilioni 
17.
  Alisema kuwa mgogoro wa TANESCO ulianza kuibuka baada ya kuzushwa 
uongo kuwa nchi inaweza kuingia gizani wakati wowote kutokana na hali 
mbaya ya shirika, madai ambayo Mbatia alisema si ya kweli kwani ulikuwa 
ni ujanja wa mafisadi kuzima kwa makusudi mitambo.
  “Kisha TANESCO iliingia kwenye mchakato wa kutafuta wazabuni wa 
kuiuzia mafuta mazito ya kuendesha mitambo yake ambapo ilifanya 
mazungumzo na kampuni tatu zilizoonyesha kuwa tayari kuiuzia mafuta hayo
 kwa sh 1,800 kwa lita,” alisema.
  Katibu Mkuu wa Wizara ya Nishati na Madini, Eliakim Maswi, naye 
alifanya mazungumzo na Kampuni ya Puma ambako serikali ina hisa za 
asilimia 50 na kuafikiana kuwa inaweza kusambaza mafuta hayo kwa gharama
 ya sh 1,460 kwa lita, bei iliyoonekana kuwa na unafuu zaidi.
  Mbatia alifafanua kuwa pamoja na kampuni ya Puma kutokuwa kwenye 
orodha ya zile zilizoomba zabuni hiyo, Maswi alitumia kanuni ya 42 (1) 
ya mamunuzi ya umma inayompa mamlaka ya kuamua vinginevyo kwenye masuala
 yenye maslahi ya umma kuipa zabuni hiyo hiyo.
  “Kosa na kelele zote zimetoka hapo, mianya ya mafisadi imezibwa kwani 
walitaka kuzipa zabuni kampuni za bei kubwa ili wavune sh bilioni tatu 
ambazo zinaokolewa kila baada ya wiki mbili. Sasa kama kwa mwezi TANESCO
 inaokoa sh bilioni sita kwa nini tumnyime zabuni huyu?” alihoji.
  Mbatia alisema kwa mwezi Mei pekee TANESCO ilikusanya sh bilioni 85 na
 matumizi yake kwa mwezi ni sh bilioni 11 ambapo kwa wastani wanapata 
zaidi ya sh bilioni 60 wakiwa na ziada ya sh bilioni 50 kila mwezi.

 
 
No comments:
Post a Comment