To Chat with me click here

Friday, July 13, 2012

MADAKTARI WAANDAA MAANDAMANO MAKUBWA NCHINI

•  Wataka iundwe tume huru ya kuchunguza sakata zima

CHAMA cha Madaktari Tanzania (MAT), kimepanga kufanya maandamano makubwa ya amani jijini Dar es Salaam ili kupinga dhuluma na uonevu dhidi ya taaluma muhimu ya udaktari na madaktari wenyewe.

Akizungumza na waandishi wa habari jana jijini Dar es Salaam, Katibu wa MAT, Dk. Rodrick Kabangila pichani, alisema maandamano hayo yatatanguliwa na mkutano mkubwa wa madaktari wote utakaofanyika leo kujadili mustkabali na mwenendo wa taaluma ya udaktari.

Kwa mujibu wa Dk. Kabangila, MAT inasikitishwa na dhuluma hiyo kwa kuzingatia uwiano duni wa madaktari hapa nchini ambapo daktari mmoja hutibu wagonjwa 30,000 kwa mwaka chini ya viwango vya kimataifa.

Alisema jumla ya madaktari 400 walio chini ya usimamizi wa madaktari bingwa, wamesitishiwa usajili wao na wengine kusimamishwa kazi bila kujali umuhimu wao kwa mustakabali wa taifa na wananchi wake.

“Tutafanya maandamano ya amani, madaktari wote na wadau wa sekta hii wenye mapenzi mema tunawaomba washiriki… madaktari tutavaa makoti yetu meupe na watakaoshiriki nasi wavae vitambaa vyeupe.

Maandamano yataanzia nje ya Hospitali ya Taifa Muhimbili, tutaishia kwenye geti la Wizara ya Afya na Ustawi wa Jamii, tukiwa na mabango ya kulaani kitendo cha kutekwa, kupigwa na kutelekezwa kwenye msitu wa Pande alichofanyiwa Dk. Steven Ulimboka,” alisema.

Dk. Kabangila alisema kuwa wataishinikiza serikali iunde tume huru kwa ajili ya kuchunguza suala la Dk. Ulimboka itakayofanya kazi haraka na wahusika wote wafikishwe kwenye vyombo vya sheria.

Awali, katibu huyo alieleza kushangazwa kwake na wanaojiita viongozi wa dini ambao huwakatisha tamaa kwa kuwanena mabaya bila kujali mazingira magumu wanayofanyia kazi madaktari.

Mgogoro kati ya madaktari na serikali ulianza mwaka 2005 ambapo madai ya wataalam hao ni mazingira bora ya kazi, vitendeakazi bora, mashine za kisasa na nyongeza ya posho na mishahara.

Kushindwa kumalizika kwa mgogoro huo kulisababisha Jumuiya ya Madaktari nchini, kuitisha mgomo mwanzoni mwa mwaka huu ili kuishinikiza serikali kutimiza madai yao.

No comments:

Post a Comment