To Chat with me click here

Monday, July 16, 2012

WATU 18 WASHIKILIWA NA POLISI SINGIDA KWA TUHUMA ZA MAUAJI YA MWENYEKITI WA UMOJA WA VIJANA CCM.

Kamanda wa polisi mkoa wa Singida,Linus Vicent Sinzumwa akizungumza na waandishi wa habari (hawapo kwenye picha) kutokana na vurungu zilizotokea kati ya wafuasi wa CHADEMA na CCM huko mkoani Singida.

Jeshi la polisi mkoa wa Singida linawashikilia wakazi 18 wa kata ya Ndago jimbo la Iramba magharibi kwa tuhuma ya kumuua mwenyekiti wa umoja wa vijana CCM (UVCCM) Yohana Mpinga (30) baada ya kumpiga kwa kutumia silaha za jadi.

Kamanda wa jeshi la polisi mkoa wa Singida Linus Vicent Sinzumwa amesema tukio hilo la kusikitisha limetokea Julai 14 katika kijiji cha Ndago.

Amesema siku ya tukio, Chama Cha Maendeleo na Demokrasia (CHADEMA) kilikuwa na kibali halali cha kufanya mkutano wa hadhara katika kijiji hicho cha Ndago na mgeni rasmi katika mkutano huo alikuwa mbunge wa jimbo la Ubongo jijini Dar-es-salaam Mhe. John J. Mnyika.

Mbali na Mnyika, viongozi wengine wa Chadema waliokuwapo ni Mjumbe wa Kamati Kuu ya Chadema, Dk Kitila Mkumbo na Mkurugenzi wa Habari na Mawasiliano wa chama hicho, Mwita Waitara.

Sinzumwa amesema mara baada ya CHADEMA kuanza mkutano huo, viongozi wake walianza kuporomosha mvua ya kashifa mbalimbali dhidi ya mbune wa jimbo hilo Mwingullu Nchemba, kitendo ambacho kiliudhi baadhi ya watu waliokuwa wamehudhuria mkutano huo.

Kamanda huyo amesema kuwa vurugu hizo zilihusisha kundi la wanachama wa CHADEMA na wa CCM na zilisambaa ambapo wanachama hao walianza kurusha mawe ovyo na askari wachache wa polisi waliokuwepo, walizidiwa nguvu na makundi hayo.

Amesema katika kundi hilo ambalo wamelikamata,watawahoji na wataobainika kuhusika watafikishwa mahakamani wakati wowote.

Akizungumza na waandishi wa habari, Mwita alidai mbali na mkutano huo kuwa na baraka za Polisi, lakini pia walikuwa na taarifa juu ya mpango wa kuvurugwa mkutano huo. Alidai waliwatahadharisha askari waliokuwapo kwenye eneo hilo kuwa kuna vijana ambao walikuwa wameandaliwa kufanya fujo ili kuhakikisha kuwa mkutano huo haufanyiki.

Kwa mujibu wa madai ya Mwita, taarifa hizo zilieleza kuwa kuna kikundi cha vijana kilichokuwa kimeandaliwa na kununuliwa pombe pamoja na kukodiwa gari ili kiharibu mkutano huo kwa kuhakikisha haufanyiki. Alidai pamoja kutoa taarifa hizo, hakuna hatua yoyote ya makusudi iliyochukuliwa na Polisi waliokuwapo karibu na eneo la mkutano, hali iliyosababisha fujo kutokea mara tatu kabla ya mkutano huo kuendelea na kukamilika salama na wao kuondoka katika eneo hilo.

“Lakini kutokana na vurugu zilizokuwa zikisababishwa na kikundi cha vijana ambao tayari walishatolewa taarifa yao kwenye mkutano huo mbele ya Polisi, askari waliokuwapo hawakuthubutu kuchukua hatua kwa vijana wale,” alidai Mwita. Alidai wakati wakiendelea na mkutano huo na baada ya kutoa taarifa kwa OCD na RPC, askari waliokuwa tayari kuzuia fujo walifika, lakini tayari fujo zilishatulia na mkutano uliendelea kama kawaida.

Kutokana na fujo hizo ambazo Mwita alidai zilitokea mara tatu, waliamua kufungua jalada Polisi lenye namba NDG/RB/190/2012 na katika jalada hilo walitaja majina ya watu waliokuwa wakifanya fujo mbele ya mkutano huo kwa lengo la kufanya mkutano huo usifanyike.

Aliwataja watu aliodai waliohusishwa na fujo hizo na walionaswa na kamera zilizokuwa zikitumiwa kuchukua kumbukumbu ya mkutano huo kuwa ni Daniel Sima, Tito Nitwa, Bakili Ayubu, Yohana Makala Mpande, Ernest Kadege, Abel John, Athumani Ntimbu, Martin Manase, James Ernest, Simon Makacha, Anthon John na Frank Yesaya.
“Kwa hakika askari wa Ndago waliokuwepo mkutanoni mbali ya kutochukua hatua yoyote, fujo za sisi kupondwa mawe zilizidi, askari wote walikimbia akabaki OCS pekee ambaye naye alionekana dhahiri kutochukua hatua stahili,” alidai Mwita.

Alisema mpaka wanaondoka katike eneo la mkutano hakukuwa na taarifa yoyote juu ya fujo ilizosababisha mtu kupoteza maisha na waliendelea na mkutano mwingine katika Kijiji cha Kinampanda na waliporudi hotelini walipofikia jioni mjini Singida walianza kusikia taarifa zinazoeleza kuwa kuna mtu au watu wamepoteza maisha katika mkutano wao wa  kwanza.

Mwita alidai Chadema inalaani taarifa zilizosambazwa kuwa chama hicho kinahusika katika kupoteza maisha ya mtu huyo kwani hakikujihusisha kwa aina yoyote katika kufanya fujo na muda wote kilikuwa kikiomba msaada kutoka kwa askari ili kutuliza fujo hizo.

Alisema kutokana na habari zinazosambazwa kwa kuihusisha Chadema, kuwa kinahusika katika kupoteza maisha ya mtu huyo, chama hicho kimebaini kuwepo mbinu chafu ya kuvihusisha vyombo vya Dola katika kuwatisha wananchi ili wasikiunge mkono katika kuleta mabadiliko ya kweli ndani ya jamii.

Alisema tayari chama chake kimeshapokea taarifa kutoka Jeshi la Polisi ya kusitishwa kwa ziara yake ambayo kwa jana ingefanya mikutano miwili katika kijiji cha Shelui na Kiomboi na wanatii amri hiyo.

No comments:

Post a Comment