To Chat with me click here

Friday, July 27, 2012

MZOZO NISHATI NA MADINI: PINDA AMUOKOA JK

WAZIRI Mkuu Mizengo Pinda juzi jioni alifanya kazi ya ziada kuzima hasira za wabunge waliokuwa wakitaka kuona Waziri wa Nishati na Madini, Pofesa Sospeter Muhongo, na Katibu Mkuu wake, Eliakim Maswi, wakiwajibika kwa kujiuzulu nyadhifa zao vinginevyo wangekwamisha bajeti ya wizara hiyo.
Habari ambazo Tanzania Daima, imezipata zinadai kuwa wabunge hao walidhamiria kukwamisha bajeti ya Wizara ya Nishati na Madini kwa mwaka 2012/2013 inayotarajiwa kusomwa bungeni leo.

Chanzo cha habari hizo kilidai wabunge walifikia hatua hiyo baada ya vigogo hao kuripotiwa kuwa waliruhusu ukiukwaji wa sheria ya manunuzi ya umma kwa kuipa zabuni kampuni ya Puma Energy (T) Ltd zamani BP.
Kampuni hiyo ilipewa zabuni ya kununua mafuta ya kuendesha mitambo ya kuzalisha umeme ya Independent Power Tanzania Limited (IPTL) na kuziweka kando kampuni zilizokuwa zimechaguliwa kupitia mchakato halali wa zabuni ya TANESCO.

Suala hilo linahusishwa na kusimamishwa kwa Mkurugenzi Mkuu wa TANESCO, William Mhando, kwamba alichukuliwa hatua baada ya kukataa kutii maelekezo ya wizara.
Katika kikao cha juzi usiku cha wabunge wa CCM, kilichoongozwa na Waziri Mkuu Mizengo Pinda, wabunge hao walikuwa na msimamo wa kumuwajibisha Muhongo na Maswi. Wakati wabunge wakiwa na msimamo huo, Pinda aliingia akiwa na lengo la kuilinda serikali na chama kinachotawala (CCM).

Pinda alidai kuwa kumshinikiza Rais Kikwete amuwajibishe waziri aliyemteua miezi mitatu iliyopita ni kutomtendea haki na kuuonyesha umma kuwa hakufanya chaguo sahihi.
Tanzania Daima, ilidokezwa kuwa wajumbe wote walikubaliana kwamba Katibu Mkuu wa Nishati na Madini alifanya makosa na alivunja sheria.
Wabunge wa CCM walitaka Maswi na Muhongo watoswe ili kujenga heshima ya serikali na kusimika utawala wa sheria.

Inadaiwa kuwa kulikuwa na wabunge waliopangwa kimkakati kushawishi wenzao wasiisulubu serikali kwa kukwamisha Bajeti ya Nishati na Madini leo.
Miongoni mwa wabunge wanaotajwa ni Waziri Mkuu Pinda, William Lukuvi, Jenista Mhagama na Mbunge wa Muleba Kaskazini, Charles Mwijage. Inadaiwa kuwa Mwijage ana maslahi katika Puma Energy iliyopewa zabuni ya kuiuzia mafuta IPTL na Maswi.
Mbunge wa Simanjiro Christopher Ole Sendeka, anadaiwa kutaka iundwe kamati teule ya Bunge kuchunguza uozo ulio ndani ya wizara na TANESCO.

Baadhi ya wabunge wakasema wazo lake ni sawa, lakini katika mazingira ya sasa ya kisiasa ya CCM, tume itaibua uchafu mwingi ambao utaimaliza serikali mbele ya umma.
Sendeka alisema: “Mbona katika sakata la Richmond iliundwa kamati iweje hivi sasa isiundwe wakati kosa la Maswi linafanana na la Lowassa?”
Mbunge wa Same Mashariki, Anne Kilango, inasemekana alijenga hoja kuwa CCM na serikali walifanya makosa kwenye sakata la Richmond ambalo lilimfanya aliyekuwa Waziri Mkuu Edward Lowassa, kuachia ngazi.

“Tulimtosa Lowassa, baadaye ukweli umejulikana, na sasa makosa yetu yanaigharimu serikali na CCM. Tusirudie makosa yale yale, tuwaache hawa kwa maslahi ya CCM,” alisema.
Hata hivyo baadhi ya wajumbe walishikilia msimamo wa kuwajibishwa kwa Muhongo na Maswi kwa madai kuwa endapo wataachwa, wataimaliza serikali ya CCM.
Walisema kuwaacha ni sawa na kulitangazia taifa kwamba wao ni wavunjaji wa sheria walizozitunga wenyewe.

Tanzania Daima imeelezwa kuwa hata hivyo hatimaye wabunge hao walikubaliana kwa shingo upande kuwa msimamo wa wabunge wa CCM ni kulinda chama na serikali.

No comments:

Post a Comment