To Chat with me click here

Saturday, July 14, 2012

MNYIKA AHOJI MAKANDARASI KUTOWAJIBISHWA

MBUNGE wa Ubungo, John Mnyika (CHADEMA), amehoji hatua zinazochukuliwa na serikali dhidi ya makandarasi waliofanya uzembe na kusababisha mradi wa miundombinu ya maji uliofanywa na Wachina katika maeneo mengi ya Jiji la Dar es Salaam kutofanya kazi hadi hivi sasa.
Alitoa kauli hiyo Bungeni jana wakati alipokuwa akiuliza swali la nyongeza ambapo alisema kwamba hatua hiyo imewasababishia adha wananchi. Akijibu swali hilo, Naibu Waziri wa Maji Dk. Binilith Mahenge alisema kuwa mradi huo ulikuwa na awamu nne na tayari awamu 3 zimeshapita hivyo katika utekelezaji wa awamu ya nne watahakikisha wanaangalia tatizo lililosababisha mradi huo kuchelewa kuanza kufanya kazi.
Awali katika swali la msingi la mbunge wa Viti maalum, Rita Mlaki (CCM) ambalo lililoulizwa kwa niaba yake na mbunge wa Peramiho, Jenister Mhagama alitaka kujua kama Serikali inaweza kueleza ni kwa nini kata ya mikocheni eneo TPDC karibu na viwanja vya mitambo ya TTCL halipati maji mpaka sasa. “Mradi wa miundombinu ya maji uliofanywa na Wachina katika maeneo mengi ya jijini Dar es Salaam hususan wilaya ya Kinondoni haifanya kazi hadi hivi sasa,” alisema Mbunge huyo.
Akijibu swali hilo, Dk. Mahenge alisema kata ya Mikocheni iko katika eneo linalopata maji kutoka mtambo wa Ruvu chini hivyo kutokana na mahitaji ya maji kuwa makubwa ukilinganisha na uwezo wa uzalishaji wa mtambo wa huduma ya maji katika maeneo mengi jijini hutolewa kwa mgao.
“Hii ni pamoja na eneo karibu na viwanja vyenye mitambo ya TTCL kata ya Mikocheni,” alisema Naibu Waziri huyo. Aliongeza kuwa huduma ya maji katika kata hiyo na maeneo yote yanayopata maji kutoka mtambo wa Ruvu Chini itakuwa ya uhakika zaidi baada ya kukamilika kwa mradi unaoendelea hivi sasa wa upanuzi wa mtambo wa Ruvu Chini.
Alifafanua kuwa mkandarasi anaendelea na upanuzi kuongeza uzalishaji wa asilimia 50, kutoka lita milioni 180 kwa siku za sasa hadi kufikia lita milioni 270 kwa siku. “Kazi hiyo itakamilika mwezi machi 2013 sambamba na upanuzi huo bomba kubwa litajengwa kuyatoa maji hayo kutoka eneo la mtambo kuyaleta jijini,” alisema Dk. Mahenge.
Alisema Serikali imetenga jumla ya sh bilioni 116.4 katika mwaka wa fedha 2012/2013 kwa ajili ya kazi hiyo.
Naibu Waziri huyo alitanabaisha kuwa mhandisi wa kusimamia kazi ameshateuliwa na taratibu za kumpata mkandarasi wa ujenzi katika hatua za mwisho na ataajiriwa baadaye mwezi huu na ujenzi utafanyika kwa miezi 15.
Source: Tanzania Daima

No comments:

Post a Comment