MBUNGE wa 
Ubungo, John Mnyika (CHADEMA), amehoji hatua zinazochukuliwa na serikali
 dhidi ya makandarasi waliofanya uzembe na kusababisha mradi wa 
miundombinu ya maji uliofanywa na Wachina katika maeneo mengi ya Jiji la
 Dar es Salaam kutofanya kazi hadi hivi sasa.
Alitoa kauli
 hiyo Bungeni jana wakati alipokuwa akiuliza swali la nyongeza ambapo 
alisema kwamba hatua hiyo imewasababishia adha wananchi. Akijibu 
swali hilo, Naibu Waziri wa Maji Dk. Binilith Mahenge alisema kuwa mradi
 huo ulikuwa na awamu nne na tayari awamu 3 zimeshapita hivyo katika 
utekelezaji wa awamu ya nne watahakikisha wanaangalia tatizo 
lililosababisha mradi huo kuchelewa kuanza kufanya kazi.
Awali katika
 swali la msingi la mbunge wa Viti maalum, Rita Mlaki (CCM) ambalo 
lililoulizwa kwa niaba yake na mbunge wa Peramiho, Jenister Mhagama 
alitaka kujua kama Serikali inaweza kueleza ni kwa nini kata ya 
mikocheni eneo TPDC karibu na viwanja vya mitambo ya TTCL halipati maji 
mpaka sasa. “Mradi wa 
miundombinu ya maji uliofanywa na Wachina katika maeneo mengi ya jijini 
Dar es Salaam hususan wilaya ya Kinondoni haifanya kazi hadi hivi sasa,”
 alisema Mbunge huyo.
Akijibu 
swali hilo, Dk. Mahenge alisema kata ya Mikocheni iko katika eneo 
linalopata maji kutoka mtambo wa Ruvu chini hivyo kutokana na mahitaji 
ya maji kuwa makubwa ukilinganisha na uwezo wa uzalishaji wa mtambo wa 
huduma ya maji katika maeneo mengi jijini hutolewa kwa mgao. 
“Hii ni pamoja na eneo karibu na viwanja vyenye mitambo ya TTCL kata ya Mikocheni,” alisema Naibu Waziri huyo. Aliongeza 
kuwa huduma ya maji katika kata hiyo na maeneo yote yanayopata maji 
kutoka mtambo wa Ruvu Chini itakuwa ya uhakika zaidi baada ya kukamilika
 kwa mradi unaoendelea hivi sasa wa upanuzi wa mtambo wa Ruvu Chini.
Alifafanua 
kuwa mkandarasi anaendelea na upanuzi kuongeza uzalishaji wa asilimia 
50, kutoka lita milioni 180 kwa siku za sasa hadi kufikia lita milioni 
270 kwa siku. “Kazi hiyo 
itakamilika mwezi machi 2013 sambamba na upanuzi huo bomba kubwa 
litajengwa kuyatoa maji hayo kutoka eneo la mtambo kuyaleta jijini,” 
alisema Dk. Mahenge.
Alisema Serikali imetenga jumla ya sh bilioni 116.4 katika mwaka wa fedha 2012/2013 kwa ajili ya kazi hiyo.
Naibu Waziri
 huyo alitanabaisha kuwa mhandisi wa kusimamia kazi ameshateuliwa na 
taratibu za kumpata mkandarasi wa ujenzi katika hatua za mwisho na 
ataajiriwa baadaye mwezi huu na ujenzi utafanyika kwa miezi 15.
Source: Tanzania Daima 


 
 
No comments:
Post a Comment