To Chat with me click here

Thursday, November 15, 2012

WANAKIJIJI WANAVYOUZA ARDHI KWA KIBABA CHA UNGA NA SODA


Moja ya maeneo ya Wilaya ya Rufiji, mkoani Pwani ambako ardhi imekuwa ikiuzwa kwa kibaba cha unga. Picha na maktaba. 

WAKATI mwingine unaweza usiamini kabisa kwamba ardhi imekuwa ikichukuliwa na wawekezaji kutokana na wananchi kutojua umuhimu wa kumiliki ardhi. Ardhi imebaki kuwa rasilimali pekee kwa watu maskini, lakini imekuwa ikitolewa kiholela kwa vigezo vya uwekezaji.

Uingiaji wa mikataba kati ya wananchi na wawekezaji hasa wa maeneo ya vijijini mara nyingi umekuwa ni wa kushangaza kwa sababu mikataba mingi imekuwa haizingatii uwiaano na usawa kati ya pande mbili.

Katika Wilaya ya Rufiji, mkoani Pwani wamekuwa wakiuza ardhi au kukubali kuigawa kwa wawekezaji baada ya kupewa unga kilo mbili.

Upande wa wananchi umekuwa ukielemewa na mzigo mkubwa wa mikataba mibovu kutokana na kukosa uelewa wa kutosha kuhusu thamani ya ardhi na jinsi atakavyonufaika na bidhaa au huduma za mwekezaji baada ya kuingia mkataba husika.

Wanaotushawishi ni viongozi.
Kwa mfano, hivi karibuni wananchi wa Kijiji cha Chumbi C, kilichopo Kata ya Chumbi, Tarafa ya Mohoro Wilaya ya Rufiji, mkoani Pwani wameridhia kugawa  ekari 2,300 za ardhi kwa wawekezaji  kutoka familia ya mfalme wa Saudia Arabia baada ya kila mwana kijiji kugawiwa kilo mbili za unga.

Unga huo uligawiwa kwa mwana kijiji aliyehudhuria mkutano wa makubaliano ya kuuza ardhi hiyo na kwa wengine ambao siku hiyo hawakupata fursa kuhudhuria ‘deal’ hilo kubwa.

Wananchi waliohudhuria mkutano huo wanasema waliitwa na viongozi wa vijiji ambao waliwaambia kwamba kama watakubali kutoa ekari hizo watapewa unga.

Mmoja wa wananchi hao Juma Saidi anasema wana kijiji waligawiwa unga huo kwenye mkutano mkuu wa kijiji Oktoba 5, mwaka huu baada ya kuridhia kuigawa ardhi hiyo kwa wanakijiji.

Saidi anasema walipelekewa viroba 120 vya unga kutoka jijini Dar es Salaama ambako wawekezaji hao wanaishi na wengine wilayani hapo. Anasema wawekezaji hao hawajaahidi kutekeleza jambo lolote zaidi ya kuahidi kutoa unga na misaada mingine itakayohitajika katika kijiji hicho.

Kabla wawekezaji hao hawajapewa ardhi hiyo waliwaeleza wana kijiji hao kwamba wanatoka katika familia ya kifalme ya mfalme wa Saudi Arabia na kwamba  kwao kuna fedha na suala la kutoa misaada siyo tatizo kwao.

Mwenyekiti wa Kijiji cha Chumbi C,  Salum Mtimbuko alikiri kupokea msaada huo wa unga na kusema wananchi wote walikubaliana na suala hilo na kwamba uamuzi huo haukuwa wa kwake peke yake.

Mtimbuko anasema wananchi walikubali kutoa ardhi hiyo kwa mwekezaji huyo kwa kuwa wanakabiliwa na tatizo la njaa. Anasema kabla kufikia uamuzi huo alijitahidi kutafuta msaada wa chakula na kwamba alipokutana na waarabu hao walikubali kutoa unga huo kwa wana kijiji, lakini sharti kubwa likiwa ni kupatiwa ardhi kwa ajili ya uwekezaji.

“Hao wanaosema kwamba ardhi imeuzwa ni maadui wa kijiji na watashindwa kwa kuwa suala hilo tumelifanya kwa pamoja mimi na Serikali na wananchi kwa ujumla,”anaeleza Mtimbuko. Mtimbuko anasema waarabu hao ni Watanzania na wana haki ya kuomba ardhi katika ardhi ya Tanzania na kwamba wameahidi kutekeleza mradi wa  Kilimo Kwanza.

Wengine wauza ardhi kwa kupewa soda
Mbali na kijiji hicho kugawa ardhi kwa kutumia kibaba cha unga, wenzao wa Halmashauri ya Kijiji cha Kivinja A, wilayani hapa wamekubali ‘kuuza’ ekari 50 za ardhi kwa taasisi moja inayojishughulisha na uhifadhi wa mazingira, ufugaji wa samaki na mifugo baada ya kushawishiwa kwa soda na biskuti.

Baadhi ya wajumbe kutoka katika kijiji hicho wamesema walilotoa ardhi hiyo baada ya kuambiwa kuwa watafaidika na mradi huo wa kuhifadhi mazingira katika kijiji hicho kwa kutoa ajira kwa vijana.

Mmoja wa wajumbe anabainisha kwamba elimu duni kuhusu thamani ya ardhi na umaskini ni moja ya sababu kubwa inayochangia wauze ardhi kwa kudanganyika kwa soda, unga na biskuti.

Kutokana na hali hiyo wana kijiji hao wanahitaji elimu zaidi ambayo itawasaidia kujua umuhimu wa ardhi kwa maisha yao ya sasa na vizazi vijavyo. Mwenyekiti wa kijiji hicho Salum Ngulangwa anasema ni kweli walipewa soda na biskuti katika kikao cha Halmashauri wakati wa kujadili maombi hayo.

Ngulangwa anasema baada ya kujadiliana, wajumbe wa kijiji hicho walikubali kutoa ekari hizo kwa wawekezaji hao. Anasema wawekezaji hao hawajawahi kupata hati, wala kufanya tathmini ya mazingira katika eneo hilo ambalo ni sehemu ya ardhi ya kijiji hicho.

Mwenyekiti huyo anabainisha kwamba walikubaliana kama mwekezaji hayo atashindwa kuanza kutekeleza mradi huo ndani ya mwaka mmoja, watamnyang’anya eneo hilo.

Kumekuwa na wimbi kubwa la watu wanaojiita wawekezaji wanaoingia wilayani hapa kuchukua maeneo makubwa ya ardhi kwa lengo la uwekezaji, lakini maeneo mengi waliyochukua yamekuwa mapori na wananchi wamebaki maskini.

Taasisi ya Hakiardhi imekuwa ikitoa mafunzo kwa wanavijiji namna ya kukabiliana na wawekezaji hao, lakini baadhi ya wenyeviti wa vijiji wamekuwa wakinunuliwa kwa kupewa rushwa ama kwa kuahidiwa kujengewa nyumba baada ya kukamilisha mipango yao.

Ahadi za wawekezaji hazitekelezwi
Lakini ahadi hizo kati ya mwekezaji na viongozi hao zimekuwa hazitekelezwi na imebainika kwamba wawekezaji wamekuwa wakifanya hivyo ili kutumia hati kukopa mabilioni ya fedha katika taasisi za fedha nchini.

Ofisa Mtendaji wa kijiji hicho Ashura Jongo anasema baadhi ya ahadi ambazo wawekezaji wamekuwa wakizitoa kwa wanakijiji wakati wakitafuta ardhi ni kutoa ajira, kuongeza kipato kwa wananchi, kuleta maendeleo vijijini na kuboresha utaalamu wa kilimo, ujenzi wa shule, barabara, zahnati, kuchimba visima vya maji, na nishati ya umeme.

Jongo anasema ahadi hizo zimekuwa hazitekelezwi kwa kuwa siyo sehemu ya masharti ya kugawa au kuuza ardhi kwa mwekezaji. 

Ofisa huyo anasema uzoefu unaonyesha kuwa wana vijiji wamekuwa wakiweka masharti hayo wakiamini kwamba masharti hayo yatakuwa sehemu ya mkataba ambao unafanywa na Serikali kuu kupitia kwa kamishna wa ardhi au kituo cha uwekezaji.

No comments:

Post a Comment