To Chat with me click here

Saturday, November 17, 2012

CHADEMA: UVUMILIVU SASA BASI, WASEMA WIZI WA KURA SASA MWISHO




WAKATI kauli ya Mwenyekiti wa Chama Cha Mapinduzi (CCM), Rais Jakaya Kikwete ya kuwataka viongozi na wanachama wa chama hicho kuacha kulitegemea Jeshi la Polisi katika kukabiliana na wapinzani wao ikiibua upya machungu ya mauaji ya raia, Chama cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA) kimesema uvumilivu wake umefika kikomo.

Badala yake CHADEMA kimesema kitachukua hatua zote za kulinda haki zake za msingi, ikiwemo uhuru wa kuendesha mambo ya siasa kwa mujibu wa katiba na sheria na zaidi kupambana na hujuma zote, zikiwemo za wizi wa kura wakati wa uchaguzi.

Msimamo huo ulitolewa juzi usiku na Mbunge wa Ilemela, Ezekiel Wenje ambaye alisema CHADEMA, kimevumilia vya kutosha kile alichokiita unyanyasaji, uonevu na wizi wa kura ambao alidai umekuwa ukifanywa waziwazi na viongozi wa CCM katika chaguzi kadhaa hapa nchini.

Akizungumza katika kipindi cha ‘Malumbano ya Hoja’ kinachorushwa na kituo cha runinga cha ITV, Wenje alisema viongozi wa CHADEMA wamejitahidi kwa muda mrefu kuwa waungwana na kulazimishwa kukubali udhalimu huo kwa nia ya kuokoa nchi isiingie katika machafuko.

Huku akiungwa mkono na washiriki wengine wa mdahalo huo, Wenje alisema serikali imekuwa ikitumia vibaya madaraka yake na rasilimali za nchi kukandamiza vyama vya upinzani, ama wale wote wanaoonekana kuwa mstari wa mbele kuikosoa.

“Kuanzia sasa hatutakubali tena uonevu huu. Wapinzani wameibia kura zao waziwazi, na tunapojaribu kusema ukweli, tunashambuliwa na kupigwa.
“Hakuna amani katika nchi inayoendeshwa kwa uonevu, maana demokrasia ya kweli ni kutenda haki na usawa kwa wote,” alisema Wenje.

Alidai kuwa CCM wamekuwa wakichelewesha kwa makusudi na kuamuru kutangazwa kwa matokeo yaliyochakachuliwa katika sehemu ambazo inajua imeshindwa vibaya, jambo ambalo limesababisha vurugu, maandamano na hata watu kupoteza maisha.

“Wakati katika uchaguzi wa Marekani matokeo yote yalitangazwa kikamilifu, utashangaa kuona pale Ilemela, msimamizi wa uchaguzi alishikwa kigugumizi kutangaza matokeo kwa siku tatu,” alisema.

JK kikaangoni
Mbali na msimamo huo uliotolewa na Wenje, CHADEMA pia kimemshukia Rais Kikwete na kumtaka awawajibishe mara moja maofisa wa serikali waliohusika kutekeleza amri za viongozi wa CCM za kuwapiga na kusababisha vifo vya wananchi.

Katika taarifa yake kwa vyombo vya habari jana, Mkurugenzi wa Ulinzi na Usalama wa CHADEMA, Wilfred Lwakatare amesema kauli ya Kikwete mjini Dodoma wakati akifunga mkutano mkuu wa CCM, imebainisha na kuweka wazi kuwa vyombo vya dola viliwakamata, kuwatesa na kuwaua wananchi hususan viongozi na wanachama wa upinzani kwa amri ya chama tawala.

Lwakatare alisema hoja ya Rais Kikwete ni jibu tosha kwa Watanzania kwamba CCM imekuwa ikilitumia Jeshi la Polisi kutimiza matakwa yao kisiasa.

“Kwa kuangalia muktadha wa mtiririko wa matukio ya kudhibiti upinzani kwa kuvuruga kazi za kisiasa za vyama vya upinzani yanayofanywa na vyombo vya dola, kwa kuua Watanzania wasiokuwa na hatia, kauli hiyo ya Kikwete imetufikisha kwenye kilele cha ushahidi kuwa Jeshi la Polisi linatumika kisiasa kukabiliana na hoja na shughuli halali za kisiasa zinazofanywa na CHADEMA.

“Kikwete amethibitisha pasi na shaka kuwa CCM waliwatumia polisi katika kumuua kijana Ally Singano Zona wakati wanachama na wapenzi wa CHADEMA walipofanya mapokezi ya viongozi wao wa kitaifa Agosti 27, 2012, mjini Morogoro,” ilisema sehemu ya taarifa ya Lwakatare.

CHADEMA pia kimedai kuwa kauli hiyo ya Kikwete imefumbua fumbo la kwa nini polisi mkoani Iringa, chini ya usimamizi wa RPC Michael Kamuhanda waliamua kutumia nguvu kubwa kuingilia shughuli halali ya CHADEMA kufanya mikutano ya ndani, ikiwemo ufunguzi wa matawi katika Kijiji cha Nyololo, mkoani Iringa, na hatimaye wakamuua mwandishi wa habari, Daudi Mwangosi, Septemba 2, 2012.

“Kwa kuangalia mtiririko wa matukio ya huko nyuma kama ambavyo tumewahi kuyatolea kauli na taarifa huko nyuma na kuangalia ripoti za uchunguzi wa tukio la Nyololo, hasa uchunguzi uliofanywa na Baraza la Habari Tanzania na Tume ya Utawala Bora na Haki za Binadamu (TUBHB), sasa ni wazi kila mmoja anaweza kuona kulikuwa na kila aina ya dalili ya maelekezo ya kisiasa kutumia polisi kuidhibiti CHADEMA.

“Kikwete pia amewasaidia Watanzania kuanza kutafuta majawabu kwa nini watuhumiwa wa kesi ya mauaji ya aliyekuwa Kiongozi wa CHADEMA, Kata ya Usa River, Msafiri Mbwambo, ambao katika tuhuma zao walishirikiana na viongozi wa CCM kuua, waliweza kutoroka mikononi mwa polisi na hadi sasa hakuna hatua yoyote iliyochukuliwa,” alisema Lwakatare.

Pamoja na kukumbusha vurugu za Ndago huko Iringa, CHADEMA kimezidi kudai kuwa kauli ya Mwenyekiti wa CCM, Rais Kikwete imefumbua fumbo juu ya mazingira ya utata yanayozunguka kifo cha kada wa CHADEMA, Mbwana Masoud, kilichotokea Igunga baada ya uchaguzi mdogo, aliyekutwa ameuawa kinyama baada ya kutekwa na kuteswa na vijana wa CCM waliopewa mafunzo ya kufanya kazi hizo katika makambi ya Ulemo, Iramba, Singida.

“Upo uthibitisho mkubwa, kuwa CCM kimeingiza silaha za moto bila kibali na kuwapatia vijana wake katika mafunzo kwenye makambi maeneo mbalimbali nchini.

“Tangu utolewe ushahidi huo, kwa kutaja aina ya bunduki, namba yake, uwezo wa kubeba risasi na ilikotengenezwa, mbali ya polisi kushindwa kufanya uchunguzi ili kuwaambia Watanzania kwa nini CCM wanaingiza silaha nchini, Mwenyekiti wa CCM, Rais Kikwete ambaye pia ni Amiri Jeshi Mkuu, ameshindwa kutoa ufafanuzi wowote, hali ambayo inahatarisha ulinzi na usalama wa nchi,” alisema.

Lwakatare alizidi kuishambulia kauli ya Rais Kikwete akidai imefunua ukurasa mpya wa kilele cha ushahidi wa namna ambavyo kuna ushirika kati ya CCM, serikali yake na vyombo vya dola, hasa Jeshi la Polisi, kushughulikia vyama vya upinzani, hususan CHADEMA kwa kuteka, kutesa na kuua raia wasiokuwa na hatia, lengo kubwa ikiwa ni kutimiza matakwa ya propaganda za CCM kuwa CHADEMA ni chama cha vurugu.

Kutokana na hali hiyo, CHADEMA kimemtaka Rais Kikwete kutekeleza barua ya Mwenyekiti wa CHADEMA, Freeman Mbowe, aliyemwandikia kutaka matukio yote ambayo vyombo vya dola, vimetumika kuteka, kutesa na kuua kwa malengo ya kisiasa ya kupambana na wakosoaji wa CCM na serikali yake, vifanyiwe uchunguzi huru, kwa kuunda Tume ya Kimahakama/Kijaji ili ukweli ujulikane na haki ionekane ikitendeka badala ya kutoa lugha ya kisiasa kwa nia ya kujikosha mbele ya umma.

Aidha, wakati uchunguzi huo ukifanyika, watuhumiwa wote, wakiwemo viongozi wa CCM, serikali na watendaji wa Jeshi la Polisi waliokubali kutumiwa na CCM, hata kuvunja haki za binadamu, katiba na sheria, wanawajibika kwa wao kujiuzulu au kufukuzwa kazi na Rais Kikwete.

No comments:

Post a Comment