To Chat with me click here

Thursday, November 15, 2012

JAPAN YAKUBALI KUISAIDIATANZANIA KUBORESHA VIWANDA


Katibu Mkuu wa Wizara ya Viwanda na Biashara, Joyce Mapunjo

TANZANIA na Japan zimetiliana saini mkataba wa mradi wa makubaliano wa kuimarisha uwezo wa viwanda na uboreshaji ili kuleta tija kwenye sekta hiyo.Japan ni moja ya nchi duniani zilizopiga hatua kiviwanda tofauti na Tanzania ambayo ni changa katika sekta hiyo.

Miongoni mwa makubalinao ambayo Japan imekubali ni kutoa mbinu za kiufundi kwa Tanzania  kuboresha viwanda na kutoa mbinu za kukuza ubora wa bidhaa zinazozalishwa.

Akizungumza jana jijini Dar es Salaam wakati wa kutia saini makubaliano  hayo, Katibu Mkuu wa Wizara ya Viwanda na Biashara, Joyce Mapunjo alisema sekta ya viwanda ndio sekta inayopewa kipaumbele katika kukuza maendeleo katika nchi mbalimbali dunia.

“Tunafurahi kutambua kuwa huu ni mradi wa kwanza wa ushirikiano wa kiufundi wa aina yake unaolenga sekta ya viwanda hapa nchini, kwani  tunajua mpango huu utatufikisha mbali kwa sababu ni mambo ya kuongeza tija na ufanisi katika uzalishaji,” alisema Mapunjo.

Alisema kupitia makubaliano ya mradi huo waliupa jina la ‘Kaizen’,  utasaidia kuimarisha  sekta ya viwanda na kuboresha bidhaa zinazozalishwa hapa nchini.

“Mradi wa Kaizen unatambulika duniani kote na Shirika la Jica limekuwa likitekeleza mradi huu wa kiufundi katika nchi mbalimbali tangu ulipoanzia katika Nchi ya Singapore mwaka 1983 na tuna imani utaleta mafanikio na tija kwa wazalishaji bidhaa mbalimbali hapa nchini,”alisema .

Alisema  mradi wa Kaizen ni moja ya mikakati stahiki ya sekta kadhaa ikiwamo  sekta ya viwanda inayotokana na mpango wa kitaifa wa maendeleo ya miaka mitano kuanzia mwaka 2011 hadi 2016.

Alisema mradi huo unatarajia kuwanufaisha wafanyabiashara na wajasiriamali katika Mikoa  ya Morogoro, Dodoma na Dar es Salaam. Alisema tayari wafanyabiashara walisha shiriki katika mafunzo ya namna ya kuzalisha bidhaa kwa ubora yaliyotolewa na Shirika la Jica.

Kwa upande wake Mwakilishi  Mkuu wa Jica hapa nchini, Yukihide Katsuta alisema lengo la kuanzisha mradi huo hapa nchini ni kutoa fursa ya uzalishaji bidhaa zenye tija na ubora katika soko.

“Kaizen ni neno la Kijapani lenye maana ya kukuza uzalishaji lakini kwa sasa nene hili linatumika dunia nzima likiwa na maana ya uzalishaji katika sekta mbalimbali,”alisema

Katsuta mradi huo una lengo la kuongeza ubora na ufanisi wa utengenezaji wa bidhaa  na kuweka mazingira salama katika maeneo ya kazi ili kuuza bidhaa zenye ubora.

No comments:

Post a Comment