To Chat with me click here

Saturday, November 17, 2012

VITA YA UJANGILI INAELEKEA KUTUSHINDA, WATUMISHI WENYEWE NDIYO MAJANGILI – NYARANDU.


Mhe. Lazaro Nyarandu

SERIKALI imesema licha ya jitihada zinazofanywa kumaliza tatizo la ujangili kwenye hifadhi za taifa hususan mapori ya akiba, tatizo hilo linazidi kukua kutokana na baadhi ya watumishi kujihusisha na vitendo hivyo.

Akizungumza kwenye mahafali ya Chuo cha Hifadhi ya Wanyamapori na Utalii Afrika (Mweka), Naibu Waziri wa Maliasili na Utalii, Lazaro Nyalandu alisema serikali inatambua ongezeko la ujangili kwenye hifadhi na inafanya kila linalowezekana kumaliza tatizo hilo.

Nyalandu alisema imekua vigumu kumaliza haraka tatizo la ujangili kutokana na baadhi ya watumishi kutokuwa waaminifu na kuwa na tamaa, hatua inayosababisha washirikiane na majangili kuua wanyama hususan tembo ambao meno yao kwa sasa yanauzwa kwa bei kubwa bara la Ulaya na Asia.

“Bei ya meno ya tembo imepanda sana miaka ya nyuma jino moja liliuzwa dola 100 za Marekani, hivi sasa bei imepanda jino moja ni dola 1,000 hadi 1,100 na hii ndiyo imewafanya watumishi wetu kupata tamaa na kujiingiza kwenye biashara haramu,” alisema Nyalandu.

Alisema kutokana na kushamiri kwa ujangili tayari serikali imeongeza mfumo wa uchunguzi kwa kushirikiana na wananchi wanaozunguka hifadhi, ili kutoa siri na kupiga marufuku uingizaji silaha za kivita ambazo zinatumiwa kuua wanyama.

Kuhusu watalii, Nyalandu alisema hivi sasa zaidi ya watalii 800,000 wanaingia nchini kwa mwaka na kwamba, lengo ni kufikia zaidi ya watalii milion moja ifikapo mwaka 2015.

Awali, Kaimu mkuu wa chuo hicho, Freddy Manongi alisema kumekuwapo na ongezeko kubwa la wanafunzi kutoka 25 mwaka 1963 hadi 502 mwaka huu, hali ambayo imechangia kuwapo changamoto mbalimbali ikiwamo uhaba wa vifaa vya kufundishia.

Changamoto zingine ni uhaba wa vitendea kazi kama magari kwa ajili ya wanafunzi kwenda kujifunzia, miundombinu kama mabweni, madarasa, maabara na nyumba za walimu.

No comments:

Post a Comment