To Chat with me click here

Monday, December 3, 2012

CHUO CHA MAENDELEO YA JAMII RUAHA IRINGA CHAINGIA KTK KASHFA NZITO YA RUSHWA YA NGONO


Mkuu wa Chuo cha Ruaha, Gasper Msigalla
TUHUMA za baadhi ya walimu kuwafelisha kwa makusudi wanafunzi na wengine wa kiume kutumia mwanya huo kuwaomba wanafunzi wa kike kufanya nao ngono, zinakikabili Chuo cha Maendeleo ya Jamii Ruaha kilichopo Ipogolo, mjini Iringa.

Mkuu wa Chuo hicho Gasper Msigalla (pichani) alikiri kuwepo kwa tuhuma hizo zinazoendelea kuchunguzwa ili haki itendeke.

“Ni kweli kuna madai hayo ya wanafunzi kufelishwa ambayo pia yamefikishwa kwenye Bodi ya chuo hicho inayoongozwa na Katibu Tawala wa Mkoa wa Iringa,” alisema.

Alisema jumla ya wanafunzi 139 kati ya wanafunzi 682 wa mwaka wa pili walifeli mitihani yao ya Februari, mwaka huu.

Msigalla alisema uongozi wake na wa Wizara ya Maendeleo ya Jamii, Jinsia na Watoto inayosimamia chuo hicho ilitilia shaka matokeo hayo.

Hata hivyo alisema wanafunzi hao walifeli mtihani huo baada ya kushindwa kupata alama zinazostahili katika tahimini ya kila siku (continuous assessment) yenye maksi 50.

 “Alama hizi na zile wanzotakiwa kupata katika mitihani yao ya darasani ambazo nazo ni hamsini ndizo zinazopima ufaulu wa mwanafunzi baada ya kupata wastani wa alama hamsini,” alisema.

Alisema wanafunzi hao walifeli mtihani huo baada ya kupigwa penati na mwalimu mmoja aliyetajwa kwa jina la Betha Lukasi kwasababu za kuchanganya zilizoelezwa na wanafunzi hao.

Wanafunzi hao walisema mwalimu huyo alikuwa akiuza chakula chuoni hapo kinyume na taratibu za zabuni na alipoondolewa na uongozi wa chuo akatumia nafasi yake kulipa kisasi.

Jitihada za kumpata mwalimu Lukasi kutoa ufafanuzi wake kuhusiana na madai ya wanafunzi hao hazikuweza kuzaa matunda na taarifa kutoka kwa Mkuu wa Chuo hicho zilidai kwamba amelazwa katika hospitali ya Lushino, mjini Iringa.

Atakapotoka hospitalini mtandao huu utamtafuta mwalimu huyo ili kwa upande wake atoe sababu za wanafunzi 139 kufeli mitihani huo.

Katika mazingira ya kutatanisha wakati wanafunzi hao wakidaiwa kufeli mitihani hiyo kumekuwepo na madai kutoka kwa baadhi yao kutakwa kimapenzi na walimu wa kiume wa chuo hicho ili wawasaidie kukabiliana na mazingira hayo.

Mkuu wa chuo hicho hakuweza kuthibitisha madai hayo, hata hivyo alisema yatafanyiwa uchunguzi na ikibainika yana ukweli walimu watakahusishwa watatolewa mapendekezo ya kuondolewa chuoni hapo.

No comments:

Post a Comment