To Chat with me click here

Tuesday, December 18, 2012

BABA GASTON NA KAKOELE VIVA KRISMAS



KILA mwaka katika kipindi kama hiki cha Majirio, yaani kuelekea siku ya kuzaliwa Kristo Masihi, Yesu Kristo (Krismas), kote duniani huwa kuna furaha kubwa mitaani na makanisani, majumba yakiwa yamepambwa kwa miti ya Krismas inayonukia, maua na vikorombwezo anuai kuikaribisha siku hiyo muhimu kwa wanadamu wote.

Zawadi mbalimbali huandaliwa kwa ajili ya kuwapatia ndugu na jamaa, Father Christmas naye akiwaandalia watoto zawadi, huku muziki mwororo ukitawala anga zote kupitia kwenye redio au televisheni.

Ni wakati huu ambapo muziki unaotawala huwa ni wa yule mkongwe wa muziki laini, marehemu Jim Reeves wa Marekani, ambaye vibao vyake 12 kikiwemo cha Jingle Bells pamoja na kundi la Boney M vibao vyao vinatamba duniani kote ikiwa ni pamoja na hapa Tanzania, ambako pia hukolezwa na kibao cha Komandoo Hamza Kalala kisemacho Noel-Krimas.

Lakini mbali na vibao hivyo, kwa ukanda mzima wa Afrika kibao ambacho hutamba zaidi na kuchukua chati ya juu ni kile kinachojulikana kama Kakoele, ama Viva Christmas au Noel Krismas, kwa vyovyote utakavyokiita.

Nasi kwa kuwatakia heri na baraka za kusherehekea sikukuu hiyo ya Krismas pamoja na Mwaka Mpya, kwa nia njema kabisa, leo tumeamua kuwaletea kibao hicho ambacho kimeimbwa kwa lugha ya Kilingala.

Wimbo huo umetungwa na kuimbwa na marehemu Ilunga Chenji Kamanda wa Kamanda Gaston Omer maarufu Baba Gaston Ilunga wa Ilunga, mwanamuziki kutoka Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo (zamani ikiitwa Zaire) ambaye alikuwa maarufu katika ukanda mzima wa Afrika Mashariki na Kati kwa ujumla.

Kibao hicho kilichomo kwenye albam yake ijulikanayo kwa majina niliyoyasema hapo juu kilifyatuliwa takriban miaka 35 iliyopita nchini Kenya, lakini bado kinaendelea kutamba na kitaendelea kutamba kwa mashabiki na wafuasi wote wa dini ya Kikristo kutokana na ujumbe uliomo ndani.

Wimbo huo unaosikika kila ikaribiapo sikukuu ya Krismas na Mwaka Mpya uliweza kumjengea jina na sifa kubwa mkongwe huyo ingawa hakuwa mashuhuri kama walivyokuwa akina Joseph Kabasele ‘Le Grand Kalle’, Dk. Nico Kassanda ‘Kassanda Nicalay’, L’Okanga La Ndju Pene Luambo Luanzo Makiadi (Francis Makiadi) ama Franco na wengineo kutoka Zaire.

Aliifyatua albam hiyo kwa ajili ya nyimbo za Krismas tu kama alivyofanya Jimmy Reeves, ambapo ina jumla ya nyimbo tano ukiwemo huo wa Kakoele au Krismas. Nyingine ni Nakumbuka Krismas, Bewela Krismas, Super Krismas na Topele Krismas. 

Kakoele anayeimbwa na Baba Gaston ni msichana wa kileo, yaani ‘Sister Duu’, mkorofi na mchoyo wa mapenzi, lakini ni mzuri ajabu. Baba Gaston kwa kuwa anafahamu Krismas ni siku ya kuzaliwa Masihi aliyekuja kufundisha pendo la kweli kwa wanadamu wote, anamwendea Kakoele siku hiyo hiyo kumkumbusha kwamba Krismas ni siku ya ‘Mfalme wa Pendo’ (Yesu Kristo).

Kwa hiyo anamtaka ajaribu kujivua uchoyo wake na kuwa mkarimu siku hiyo kisha amwonyeshe angalau pendo linalotakiwa kwa binadamu badala ya lile la ‘Chuna Buzi’.

Hali kadhalika, katika ushauri huo kwa Kakoele, anatukumbusha wanadamu wote kuwa tunawajibika wakati huu kushinda udhaifu wetu na kudhihirisha pendo la kweli ambalo limeletwa na Bwana Yesu Kristo.

Ni kibao kilichopambwa na maneno ya kumweleza muhibu wako, lakini kikiwa kimelenga hasa kuwataka wanadamu wote wapendane kama lilivyokuwa kusudi la Bwana Yesu, ambaye wanadamu wote tunaamini kwamba hata wakati anapaa aliwaambia wanafunzi wake kuwa, Wapendane, kama Mungu alivyowapenda wanadamu na kumtuma Yeye ili auokoe ulimwengu na vilivyomo!

Baba Gaston alizaliwa Julai 5, 1936 mjini Lubumbashi kusini-mashariki mwa Zaire na kujipatia elimu yake ya msingi katika shule ya St. Gabriel, Kapolowe katika Jimbo la Shaba na baadaye akafanikiwa kuendelea na masomo ya juu katika shule ya Benedict Catholic Fathers ya mjini Likasi.

Alijitosa katika ulimwengu wa muziki akiwa na miaka 20 katika Jiji la Kinshasa kwa kuanza kuimba kwaya kanisani kabla ya kuingia kwenye muziki wa Jazz akiwa na bendi yake mpya ya Orchestra Baba Nationale na wimo wake wa kwanza ukiwa ‘Barua kwa Mpenzi Gaston’.

Mwaka 1972 gwiji huyo aliamua kuja Tanzania ambapo onyesho lake la kwanza lilikuwa katika ukumbi maarufu wakati huo wa White House, Kimara jijini Dar es Salaam, ambako pia ndiko kulikuwa maskani ya bendi ya Marquiz du Zaire (OMACO), bendi ambayo sasa ni marehemu!

Miaka mitatu baadaye mwanamuziki huyo akiwa na mkewe na watoto wake kadhaa aliamua kuchanja mbuga na kwenda Kenya ambako aliendelea kuimba kabla ya kwenda Arusha alikozindua kibao chake kingine maarufu cha Talaka Mpakani Yanitoa Jasho na kuongeza raha pale alipozingua na kibao kingine cha Mapendo Kizunguzungu.

Baadaye mwaka 1994 akiwa na familia yake alihamishia maskani yake mjini Arusha akitokea Nairobi, Kenya, ambapo alikuwa ameachana na muziki na alitegemea zaidi biashara zake za duka la kuuza vyakula mbalimbali katika eneo la Majengo katika barabara ya Sokoine.

Mwanamuziki huyo alifariki dunai Jumamosi Machi 18, 1997 katika Hospitali ya KCMC mjini Moshi kutokana na kusumbuliwa na ugonjwa wa moyo. Alifariki akiwa anakaribia kabisa kufikisha miaka 61. Akaenda kuzikwa katika makaburi ya Lang’ata jijini Nairobi.

No comments:

Post a Comment