To Chat with me click here

Monday, December 31, 2012

LEMA KUJITWISHA ZIGO LA MABILIONI YA USWISI


MBUNGE wa Arusha Mjini, Godbless Lema (CHADEMA), amesema atamshawishi mbunge mwenzake wa Kigoma Kaskazini, Zitto Kabwe, ili ampatie majina ya vigogo walioficha fedha Uswisi awataje bungeni.

Zitto ndiye aliibua hoja hiyo bungeni na kuwasilisha hoja binafsi akitaka Bunge liazimie kwa kauli moja na kuunda kamati teule ya kuchunguza tuhuma hizo na kuwachukulia hatua, vinginevyo serikali ikishindwa atawataja.

Akizungumza kwenye mkutano wa hadhara mjini Kahama mkoani Shinyanga, alipopata mapokezi ya kifalme akiwa na Mwenyekiti wa BAVICHA Taifa, John Heche na kada mwingine, James Ole Millya, alisema kuwa atataja majina hayo bungeni.

Lema alisema kuwa Watanzania wamekuwa na shauku ya kuwafahamu viongozi wao mafisadi waliopora fedha zao na kwenda kuzificha katika nchi za ughaibuni kama Uswisi, Mauritania, Dubai na Morocco.

Alisema tangu hoja hiyo ifikishwe bungeni na serikali kuahidi kufuatilia, hadi sasa kumekuwa na ukimya ambao unazua maswali juu ya ukweli wa suala hilo kutoka kwa wananchi.

“Nitamuomba Kamanda Zitto anipatie majina hayo nami Bunge lijalo niyaanike ili kukata kiu ya Watanzania walio na haja kubwa ya kuwafahamu, hata kama hatua hiyo itanisababishia kifo, mimi siogopi kufa,” alisema Lema.
Aliwataka wakazi wa Kahama kuondokana na woga pindi linapofikia suala la kupigania haki zao na akasema wasiwaachie viongozi na wanachama wa CHADEMA pekee.

Lema aliishutumu Serikali ya CCM akidai imeshindwa kuwajengea miundombinu mizuri na kuwakopesha mitaji mikubwa wachimbaji wadogowadogo pindi wanapovumbua maeneo yenye madini.

Alisema kuwatimua wachimbaji hao ni kupanua wigo wa watu wasiokuwa na ajira, ombwe ambalo linaweza kuigharimu nchi hata kuingia katika machafuko.

Wakati huo huo, kada mashuhuri wa CCM, Frank Mwaisumbe, aliyeitikisa ngome ya upinzani katika uchaguzi mkuu wa mwaka 2010 akiwania ubunge katika Jimbo la Mbeya Mjini, amehamia CHADEMA.

Mwaisumbe aliyewahi kuwa Mhadhiri Msaidizi wa Kitivo cha Uchumi na Biashara katika Chuo Kikuu cha Tumaini-Iringa, kabla ya kuachana na kazi hiyo, ametangaza kujiunga na CHADEMA juzi.

Alisema CCM imeshindwa kushughulikia kero na matatizo ya wananchi ikiwemo rushwa na makundi yanayowania madaraka.

Jimbo hilo la Mbeya Mjini kwa sasa linaongozwa na Mbunge wa CHADEMA, Joseph Mbilinyi maarufu kama Sugu baada kumshinda aliyekuwa mbunge wa jimbo hilo kwa tiketi ya CCM, Benson Mpesya.

Katika hatua nyingine, vijana wametakiwa kutokuwa na fikra mgando katika kupambana na matumizi mabovu ya rasilimali yanayofanywa na baadhi ya watu wachache ili kuliokoa taifa linaloangamia.

Kauli hiyo ilitolewa juzi na Mwenyekiti wa BAVICHA Mkoa wa Iringa, Joseph Lyata katika mkutano wa hadhara uliofanyika katika Kijiji cha Luganga wilayani Kilolo.

Lyata alisema ili taifa liweze kusonga mbele, lazima liwe na watu wenye uchungu na rasilimali zilizopo na kujali matumizi ya pamoja.

No comments:

Post a Comment