To Chat with me click here

Wednesday, December 12, 2012

JET YAFICHUA MATUMIZI MABAYA YA ARDHI KILWA




Uwazi katika mikataba ya ardhi utawezesha kuondoa migogoro kati ya wawekezaji na wamiliki zikiwemo serikali za vijiji.

Hayo yameibuliwa wakati wa ziara ya waandishi wa habari waliotembelea wilaya za Kilwa na Rufiji kwa ajili ya kufanya uchunguzi wa matumizi ya ardhi, hususan katika uwekezaji katika kuzalisha nishati mimea.

Ziara hiyo iliyoratibiwa na Chama cha Waandishi wa Habari za Mazingira (Jet), ilifanyika katika vijiji vya Mavuji, Migeregere, Nainokwe na Liwiti (Kilwa) na Rungungu, Mangwi na Chumbi C wilayani Rufiji.

Mwenyekiti wa Jet, Johnson Mbwambo, aliwaambia waandishi wa habari jijini Dar es Salaam jana kuwa wimbi la uwekezaji mkubwa katika nishati mimea, limewaacha wanavijiji hao bila ardhi iliyotumika awali kwa kilimo na shughuli za maendeleo.

“Wanavijiji wengi hawana ardhi baada ya serikali kuingia mikataba na wawekezaji kukodisha ardhi kwa miaka mingi bila kujua masharti wala kuelimishwa na halmashauri za wilaya husika,” alisema.

Mbwambo alisema katika vijiji vya Mavuji, Migeregere, Nainokwe na Liwiti, wanavijiji walidai kushinikizwa na viongozi wa wilaya na mkoa, kukodisha jumla ya ekari 160,000 kwa mwekezaji mmoja ambaye hata hivyo hivi sasa hajulikani alipo.

“Wanavijiji hao walidai kuwa mwanasheria wa mkoa, alisimamia mikataba hiyo kati ya mwaka 2006 na 2007 iliyoandikwa kwa Kiingereza pasipo kufafanulia haki na wajibu wao,” alisema.

Kwa mujibu wa Mbwambo, madai ya wanavijiji hao yaliungwa mkono na viongozi wao waliothibitisha kutokuwa na nakala za mikataba husika.

Pia walisema jitihada za kuzifuatilia nakala hizo ofisi za halmashauri ya wilaya na Kituo cha Uwekezaji cha Taifa (TIC) jijini Dar es Salaam, hazijafanikiwa.

Mbwambo alimnukuu Mwanasheria wa Wilaya ya Kilwa, Godfrey Jafar, akithibitisha ofisi yake kutokuwa na nakala ya mkataba wa ukodishwaji wa ardhi hiyo.

Ilielezwa kuwa kutoonekana kwa mikataba hiyo kumejenga hisia ya kuwapo mabadiliko, hasa yanayohusu muda wa umiliki. Mbwambo alisema uchunguzi uliofanywa na Jet ulibaini kuwa eneo hilo lililokodishwa kwa ajili ya kilimo cha miboni, halikutumika ilivyokusudiwa badala yake wawekezaji walikata miti, kutengeneza mbao na kuzisafirisha nje ya nchi.

“Baadaye alisitisha shughuli zote na maofisa wake kuondoka wilayani Kilwa kwa sababu ya kile kilichoelezwa iliishiwa fedha kwa sababu ya mtikisiko wa uchumi duniani, alisema.

Aliongeza: “Kwa maana hiyo eneo hilo halijaendelezwa na vijiji havina haki kisheria ya kulitumia.”

Mbwambo alisema wanavijiji hao walipendekeza mambo kadhaa, ikiwamo kuitaka halmashauri za wilaya kuwajibika katika kuwaelimisha kuhusu masuala ya ardhi na mipata yake.

Pia walipendekeza kuondolewa kwa sheria inayowaruhusu wawekezaji kukodishwa ardhi kwa miaka 99, badala yake (ardhi) itumike kwa ubia na wamiliki (kijiji) kwa kipindi kisichozidi miaka 15.

No comments:

Post a Comment